Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 7/8 kur. 8-11
  • Jinsi ya Kudumisha Mtazamo wa Akili Unaofaa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi ya Kudumisha Mtazamo wa Akili Unaofaa
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sumu kwa Ubongo
  • Chagua Vitumbuizo kwa Hekima
  • Tafuta Mwelekezo wa Mungu
  • Jinsi ya Kuchagua Burudani Inayofaa
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Waweza Kupata Vitumbuizo Vifaavyo
    Amkeni!—1997
  • Jinsi ya Kuchagua Burudani
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Je! Televisheni Imekubadili Wewe?
    Amkeni!—1991
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 7/8 kur. 8-11

Jinsi ya Kudumisha Mtazamo wa Akili Unaofaa

AFYA yetu ya kimwili hutegemea kwa kiasi kikubwa kile tunachokula. Mtu akitegemea chakula kisichojenga mwili kwa ukawaida, hatimaye afya yake itaathirika. Kanuni hiihii hutumika kuhusu afya yetu ya akili.

Kwa kielelezo, unaweza kulinganisha mambo tunayolisha akili yetu na aina ya chakula cha akili. Chakula cha akili? Naam, habari tunayopata kutoka kwa vitabu, magazeti, maonyesho ya televisheni, vidio, michezo ya vidio, Internet, na maneno ya nyimbo yaweza kuathiri kufikiri kwetu na utu wetu kama vile chakula halisi huathiri mwili wetu. Jinsi gani?

Aliyekuwa mkurugenzi wa utangazaji Jerry Mander aliandika hivi kuhusu jinsi ambavyo televisheni huathiri maisha yetu: “Zaidi ya athari nyingine yoyote, televisheni huingiza picha ndani ya ubongo wetu.” Hata hivyo, picha hizo za akili hufanya mengi zaidi ya kutuburudisha. Gazeti The Family Therapy Networker lasema: “Ile lugha, picha, sauti, mawazo, nyutu za waigizaji, hali, kanuni, nadharia za vyombo vya habari huwa habari muhimu tunazofikiria, kuhisi na kuwazia.”

Naam, tuwe twatambua au la, mawazo na hisia zetu zaweza kuyumbishwa kwa njia ya werevu na kile tunachoona kwenye televisheni na namna nyinginezo za viburudisho. Na hapo ndipo panapo hatari. Kama asemavyo Mander, “pole kwa pole sisi binadamu hubadilika kuwa kama picha tulizo nazo akilini mwetu.”

Sumu kwa Ubongo

Watu wengi ambao huenda wakawa waangalifu sana kuhusu chakula chao cha kimwili hula kwa pupa bila kuchagua chakula chochote kile cha akili kinachoandaliwa na vyombo vya habari. Kwa mfano, je, umewahi kumsikia mtu fulani akisema: “Hakuna kitu cha maana cha kutazama kwenye televisheni!” Wengine hufadhaika bila kuchoka, wakibadili idhaa moja hadi nyingine wakitumaini kupata jambo fulani linalofaa. Wazo la kuzima televisheni haliji akilini mwao kamwe!

Kwa kuongezea kutumia muda mwingi sana, maonyesho mengi yana mambo ambayo Wakristo wengi wangependa kuyaepuka. “Mbali na lugha chafu,” asema mwandishi wa sanaa Gary Koltookian, “habari zenye ubishi na za kingono ni nyingi zaidi leo kwenye televisheni kuliko wakati uliopita.” Kwa kweli, uchunguzi wa hivi majuzi huko Marekani ulipata kwamba picha zenye habari za kingono huonekana kwa wastani wa mara 27 kwa saa wakati ambapo watu wengi sana wanatazama televisheni.

Jambo hili lingemfanya mtu afikiri juu ya jinsi linavyoathiri kufikiri kwa watu. Huko Japani drama moja ya televisheni inayopendwa sana ilivutia watu wengi sana hivi kwamba vyombo vya habari vya taifa hilo vilisema ilichochea “ongezeko la haraka la uzinzi.” Zaidi ya hayo, waandishi wa kitabu Watching America wanasema: “Leo namna nyingi za tabia za kingono . . . huonwa kuwa machaguo yanayokubalika ya mtindo wa maisha wa kibinafsi.”

Hata hivyo, programu za televisheni ambazo hutukuza habari za kingono ni sehemu tu ya tatizo hilo. Picha zenye mambo mengi na zilizo wazi zinazohusu jeuri pia ni za kawaida. Jambo lenye kuhangaisha hasa ni madhara mabaya sana ambayo programu za televisheni na sinema zenye jeuri zinaweza kuleta kwa akili changa zinazoweza kuvutiwa kwa urahisi. “Watoto wachanga wanapoona mtu amepigwa risasi, amechomwa kisu, amebakwa, ametendwa kikatili, ameshushwa, au kuuawa kwenye televisheni,” asema David Grossman, afisa wa kijeshi mstaafu na mtaalamu wa saikolojia ya kuua, “kwao mambo hayo huwa kana kwamba yanatokea kihalisi.” Likitoa maelezo juu ya tatizo hilihili, jarida la The Journal of the American Medical Association lilisema: “Kufikia umri wa miaka 3 na 4, watoto wengi hawawezi kutofautisha mambo hakika na fantasia katika programu za televisheni na hushindwa kufanya hivyo licha ya kuzoezwa na mtu mzima.” Yaani, hata ingawa huenda mzazi akamwambia mtoto, ‘Watu wale hawakufa kihalisi; walikuwa wanajifanya tu,’ akili ya mtoto bado haiwezi kupambanua mambo hayo. Kwa mtoto mchanga, jeuri ya televisheni ni halisi kabisa.

Likitoa muhtasari wa athari ya “jeuri ya vyombo vya habari,” gazeti Time lilisema: “Ni watafiti wachache wanaojisumbua kubishana kwamba umwagikaji wa damu katika televisheni na kwenye sinema huathiri watoto wanaouona.” Una athari ya aina gani? “Miongo mingi ya vitumbuizo vyenye jeuri imefaulu kubadili maoni na maadili ya umma,” asema mchambuzi wa sinema Michael Medved. Aongezea hivi: “Si maendeleo yanayofaa hata kidogo wakati jamii inapokosa kuhisi hofu kuu.” Si ajabu kwamba mwandikaji mmoja alisema kwamba kumpeleka mtoto mwenye umri wa miaka minne kwenye sinema zenye jeuri “ni kutia sumu katika ubongo [wake].”

Bila shaka, hii haimaanishi kwamba programu zote za televisheni ni mbaya. Vivyo hivyo, na vitabu, magazeti, vidio, michezo ya kompyuta, na vitumbuizo vya namna nyinginezo. Hata hivyo, ni wazi kwamba vingi vya vile vinavyojulikana kuwa vitumbuizo haviwafai watu wanaotaka kudumisha mtazamo wa akili unaofaa.

Chagua Vitumbuizo kwa Hekima

Picha zinazoingizwa kwenye akili yetu kupitia kwa macho huathiri sana mawazo na matendo yetu. Kwa kielelezo, ikiwa tungelisha akili yetu vitumbuizo visivyo vya kiadili, azimio letu la kutii amri ya Biblia ya ‘kukimbia uasherati’ lingedhoofishwa. (1 Wakorintho 6:18) Kwa namna kama hiyo, ikiwa tunafurahia vitumbuizo ambavyo vinaonyesha “watu watendao maovu,” tungeona ugumu wa kuwa “wenye kufanya amani na watu wote.” (Zaburi 141:4; Waroma 12:18) Ili kuepuka jambo hilo, ni lazima tuzuie macho yetu yasitazame “chochote kiovu.”—Zaburi 101:3, Zaire Swahili Bible; Mithali 4:25, 27.

Ni kweli, kwa sababu ya kurithi kutokamilika, sote twahitaji kupambana kufanya lililo sawa. Mtume Paulo alikiri hivi waziwazi: “Kwa kweli napendezwa na sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani, lakini mimi naona katika viungo vyangu sheria nyingine ikifanya vita dhidi ya sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu.” (Waroma 7:22, 23) Je, hii yamaanisha kwamba Paulo alishindwa na udhaifu wake wa kimwili? Sivyo hata kidogo! Alisema: “Napiga-piga mwili wangu ngumi na kuuongoza kama mtumwa, ili . . . mimi mwenyewe nisiwe mwenye kukataliwa kwa njia fulani.”—1 Wakorintho 9:27.

Hali kadhalika, hatungependa kamwe kutumia kutokamilika kwetu kuwa udhuru wa kutenda dhambi. Mwandikaji wa Biblia Yuda alisema: “Wapendwa, . . . niliona ni lazima niwaandikie ili kuwahimiza kwa bidii mfanye pigano kali kwa ajili ya imani ambayo ilikabidhiwa mara moja kwa wakati wote kwa watakatifu.” (Yuda 3, 4) Naam, tunahitaji “kufanya pigano kali” na kujiepusha na vitumbuizo vinavyotuchochea kufanya lililo baya.a

Tafuta Mwelekezo wa Mungu

Sikuzote si rahisi kusitawisha mtazamo wa akili unaofaa katika huu mfumo wa mambo. Hata hivyo, Biblia hutuhakikishia kwamba inawezekana kubaki tukiwa safi kiakili na kiadili. Jinsi gani? Kwenye Zaburi 119:11, twasoma: “Moyoni mwangu nimeliweka neno lako, nisije nikakutenda dhambi.”

Kuweka moyoni maneno ya Mungu kwamaanisha kuyaona kuwa yenye thamani au kuyastahi sana. Bila shaka, ingekuwa vigumu kuthamini Biblia ikiwa hatujui inachosema. Kwa kutwaa ujuzi sahihi kutoka kwa Neno la Mungu, tunajishughulisha sana na mawazo ya Mungu. (Isaya 55:8, 9; Yohana 17:3) Jambo hilo hututajirisha kiroho na kukuza kufikiri kwetu.

Je, kuna mwongozo wenye kutegemeka wa kuamua jambo linalofaa kiroho na kiakili? Ndiyo! Mtume Paulo alishauri: “Mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaikio zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yaliyo ya kusemwa vema, wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa likiwako, endeleeni kufikiria mambo haya.”—Wafilipi 4:8.

Lakini ili tupokee baraka halisi, mengi yanahitajiwa zaidi ya kutwaa ujuzi juu ya Mungu. Chini ya upulizio, nabii Isaya aliandika hivi: “BWANA, mkombozi wako, mtakatifu wa Israeli, asema hivi; Mimi ni BWANA Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.” (Isaya 48:17, italiki ni zetu.) Naam, hatuhitaji tu kutafuta mwongozo wa Mungu bali pia tunahitaji kutenda kupatana na ujuzi huo.

Njia nyingine ya kunufaika kiadili na kiroho ni kwa kumwitia Yehova, “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2; 66:19 NW) Tukimfikia Muumba wetu tukiwa na weupe wa moyo na unyenyekevu, atasikia kusihi kwetu. Na ‘tukimtafuta ataonekana kwetu.’—2 Mambo ya Nyakati 15:2.

Hivyo, je, inawezekana kudumisha afya yetu ya akili katika ulimwengu huu wenye jeuri na ukosefu wa adili? Kwa kweli, inawezekana! Tunaweza kudumisha mtazamo wa akili unaofaa kwa kutoruhusu akili zetu zitiwe ganzi na vitumbuizo vya ulimwengu huu, kwa kuimarisha uwezo wetu wa kufikiri kupitia kujifunza Neno la Mungu, na kwa kutafuta mwelekezo wa Mungu!

[Maelezo ya Chini]

a Kwa habari zaidi kuhusu kuteua vitumbuizo vinavyofaa, ona gazeti la Amkeni!, la Mei 22, 1997, ukurasa wa 8-10.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Watoto wengi hawawezi kutofautisha mambo hakika na fantasia katika programu za televisheni”

[Picha katika ukurasa wa 11]

“Miongo mingi ya vitumbuizo vyenye jeuri imefaulu kubadili maoni na maadili ya umma”

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

Kupunguza Hatari ya Kupatwa na Maradhi ya Moyo

Kichapo Nutrition Action Healthletter chadokeza hatua zifuatazo kukusaidia kupunguza hatari ya kupatwa na maradhi ya moyo.

• Acha kuvuta sigareti. Kuacha leo kwaweza kupunguza hatari za kupatwa na maradhi ya moyo katika mwaka mmoja, hata ikiwa utaongeza uzito.

• Punguza uzito. Ikiwa u mnene kupita kiasi, kupunguza kilo chache kama vile mbili na nusu hadi tano kwaweza kufanyiza tofauti.

• Fanya mazoezi. Kufanya mazoezi kwa ukawaida (angalau mara tatu kwa juma) husaidia kupunguza kolesteroli isiyofaa (LDL), kuzuia msongo wa damu usiongezeke, na kuzuia uzito unaopita kiasi.

• Kula mlo wenye mafuta kidogo. Ikiwa LDL yako ni ya kiwango cha juu, badili kwa kutumia nyama isiyokuwa na mafuta na kujaribu maziwa yenye mafuta kidogo au yasiyokuwa na mafuta badala ya maziwa yenye mafuta mengi.

• Punguza matumizi ya vileo. Kuna dalili kwamba wale wanaokunywa divai nyekundu kwa kiasi waweza kupunguza hatari ya maradhi ya moyo.

• Kula matunda zaidi, mboga, na vyakula vingine vilivyo na nyuzinyuzi zinazoyeyuka.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Jeuri ya televisheni ni kama kutia sumu ubongo wa mtoto

[Picha katika ukurasa wa 9]

Nyakati nyingine watoto huiga jeuri wanayoona kwenye televisheni

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao kwa kuwaandalia habari za namna nyingi zinazofaa kusoma

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki