Nyinyi Ni “Tamasha”!
1 Mtume Paulo aliandika hivi: “Tumekuwa tamasha mbele ya ulimwengu wote, mbele ya malaika na watu.” (1 Kor. 4:9, Biblia Habari Njema) Hiyo yamaanisha nini, na yaathirije huduma yetu leo?
2 Yaelekea usemi “tamasha” ulimkumbusha Mkorintho tukio la mwisho la mashindano ya kupigana ya Waroma ambayo watu waliohukumiwa walisimamishwa mbele ya maelfu ya watazamaji kabla ya kuuawa kikatili. Vivyo hivyo, watazamaji wengi sana—wanadamu na malaika—walitazama mateso ambayo Wakristo wa karne ya kwanza walipata kwa kuhubiri Ufalme. (Ebr. 10:32, 33) Uaminifu wao uliathiri watazamaji wengi, kama vile uvumilivu wetu unavyotazamwa kana kwamba ni katika uwanja wa michezo wa kisasa. Sisi ni tamasha kwa akina nani?
3 Kwa Ulimwengu na kwa Watu: Nyakati nyingine vyombo vya habari huripoti kuhusu utendaji wa watu wa Yehova. Ijapokuwa sisi huthamini ripoti nzuri ambazo ni za kweli na zisizo na ubaguzi kuhusu kazi yetu, pia sisi hutazamia ripoti mbaya zisambazwe na wachongezi wetu mara kwa mara. Hata hivyo, lazima twendelee kujipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu “kupitia ripoti mbaya na ripoti njema.” (2 Kor. 6:4, 8) Watazamaji wenye mioyo minyofu huona wazi kwamba sisi ndio wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo.
4 Kwa Malaika: Pia viumbe wa kiroho hututazama. Ibilisi na malaika zake hututazama—lakini kwa “hasira kubwa,” wakitafuta kuzuia “kazi ya kutoa ushahidi kuhusu Yesu.” (Ufu. 12:9, 12, 17) Malaika waaminifu wa Mungu hutazama na kufurahia wakati ambapo hata mtenda-dhambi mmoja tu anatubu. (Luka 15:10) Twapaswa kuimarishwa kujua kwamba malaika huiona huduma yetu kuwa kazi ya uharaka zaidi, yenye kunufaisha inayofanywa duniani leo!—Ufu. 14:6, 7.
5 Unapopatwa na upinzani au unapofikiri kwamba huduma yako haina matokeo, kumbuka kwamba unatazamwa na ulimwengu wote. Uvumilivu wako waonyesha jinsi ulivyo mwaminifu. Mwishowe, ‘pigano lako bora la imani’ litakusaidia ‘ushike imara uhai udumuo milele.’—1 Tim. 6:12.