Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kitulizo Kinachofaa cha Mkazo
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Desemba 15
    • Njia ya Kupata Burudisho

      16, 17. (a) Unaweza kupata wapi baadhi ya mafundisho makuu ya Yesu? (b) Ni nini kinachohitajiwa ili kupata burudisho kwa kufuata mafundisho ya Yesu?

      16 Katika masika ya mwaka wa 31 W.K., Yesu alitoa hotuba ambayo inajulikana sana hata leo. Hotuba hiyo inaitwa Mahubiri ya Mlimani. Imeandikwa kwenye kitabu cha Mathayo sura ya 5 hadi 7 na kitabu cha Luka sura ya 6. Sura hizo zinaeleza kwa ufupi mengi ya mambo aliyofundisha. Unaweza kupata mafundisho mengine ya Yesu katika sura nyinginezo za vitabu vya Injili. Mengi ya mambo ambayo Yesu alisema ni rahisi kueleweka, ingawa inaweza kuwa vigumu kuyatenda. Mbona usisome sura hizo kwa makini? Nguvu za mawazo ya Yesu na ziongoze fikira na mtazamo wako.

      17 Ni wazi kwamba mafundisho ya Yesu yanaweza kupangwa katika njia mbalimbali. Na tupange mafundisho makuu ili tuwe na fundisho moja kila siku katika mwezi, tukiwa na lengo la kuyafuata maishani. Jinsi gani? Usiyapitie kijuujuu tu mafundisho hayo. Kumbuka yule mtawala tajiri aliyemwuliza Yesu Kristo hivi: “Ni kwa kufanya nini mimi nitarithi uhai udumuo milele?” Yesu alipotaja matakwa muhimu ya Sheria ya Mungu, mtu huyo alijibu kwamba tayari alikuwa anayatimiza. Hata hivyo, alitambua kwamba alihitaji kufanya mengi zaidi. Yesu alimwambia ajitahidi zaidi kufuata kanuni za Mungu kwa matendo na awe mwanafunzi mwenye bidii. Yaonekana mwanamume huyo hakutaka kufanya hivyo. (Luka 18:18-23) Hivyo, yeyote anayetaka kujua mafundisho ya Yesu leo anahitaji kukumbuka kwamba kuna tofauti kati ya kukubali, na kufuata mafundisho hayo na hivyo kupunguza mkazo.

      18. Onyesha jinsi unavyoweza kutumia kwa manufaa sanduku lililoonyeshwa.

      18 Kama hatua ya kwanza ya kuchunguza na kufuata mafundisho ya Yesu, tazama fundisho la kwanza kwenye sanduku lililoonyeshwa. Fundisho hilo larejezea Mathayo 5:3-9. Naam, yeyote kati yetu anaweza kutafakari kwa muda mrefu ushauri mzuri unaotolewa kwenye mistari hiyo. Hata hivyo, unapotazama mistari hiyo kwa ujumla, unaweza kusema nini kuhusu mtazamo? Iwapo kwa kweli unataka kushinda madhara ya mkazo unaopita kiasi katika maisha yako, ni nini kitakachokusaidia? Unaweza kufaidikaje kwa kukazia uangalifu zaidi mambo ya kiroho? Je, kuna jambo linalokuhangaisha maishani ambalo unahitaji kulipuuza na badala yake kukazia uangalifu zaidi mambo ya kiroho? Ukifanya hivyo, utakuwa mwenye furaha zaidi sasa.

      19. Unaweza kufanya nini ili upate ufahamu na uelewevu zaidi?

      19 Kuna jambo jingine unaloweza kufanya. Mbona usizungumzie mistari hiyo na mtumishi mwingine wa Mungu, labda mwenzi wako wa ndoa, jamaa wa karibu, au rafiki? (Mithali 18:24; 20:5) Kumbuka kwamba mtawala huyo tajiri alimwuliza mtu mwingine—Yesu—juu ya jambo lililohusiana na habari waliyokuwa wakizungumzia. Jibu alilopata lingezidisha matarajio yake ya kupata furaha na uhai wa milele. Mwamini mwenzako unayezungumza naye kuhusu mistari hiyo hatakuwa sawa na Yesu; lakini, mazungumzo kuhusu mafundisho ya Yesu yatawanufaisha nyote wawili. Jaribu kufanya hivyo haraka iwezekanavyo.

      20, 21. Unaweza kufuata programu gani ili kujua mafundisho ya Yesu, na unawezaje kupima maendeleo yako?

      20 Tazama tena sanduku, “Mafundisho ya Kukusaidia.” Mafundisho hayo yamepangwa ili angalau uweze kufikiria fundisho moja kwa siku. Kwanza unaweza kusoma mambo aliyosema Yesu kwenye mistari iliyoonyeshwa. Kisha fikiria maneno yake. Tafakari jinsi unavyoweza kuyatumia maishani mwako. Ukiwa unahisi kwamba tayari unafanya hivyo, tafakari uone ni mambo gani zaidi unayoweza kufanya ili uishi kupatana na fundisho hilo la Mungu. Jaribu kutumia fundisho hilo siku hiyo. Ukiona ni jambo gumu kulielewa au kujua jinsi ya kulitumia, litafakari siku nyingine. Hata hivyo, kumbuka kwamba si lazima ulielewe kabisa ndipo utafakari fundisho jingine. Unaweza kufikiria fundisho jingine siku inayofuata. Mwishoni mwa juma, unaweza kuangalia uone jinsi ambavyo umefanikiwa kuyatumia mafundisho manne au matano ya Yesu. Juma la pili fikiria mafundisho zaidi, siku kwa siku. Ukiona kwamba umeshindwa kutumia mafundisho fulani, usivunjike moyo. Kila Mkristo atahisi hivyo. (2 Mambo ya Nyakati 6:36; Zaburi 130:3; Mhubiri 7:20; Yakobo 3:8) Endelea kufanya hivyo katika juma la tatu na la nne.

      21 Baada ya mwezi mmoja hivi, huenda ukafaulu kuchunguza mafundisho yote 31. Vyovyote vile, utahisije? Je, hutakuwa mwenye furaha zaidi, labda mwenye kustarehe zaidi? Hata kama hali yako itakuwa imeboreka kidogo, yaelekea mkazo utapungua, au angalau utashughulika na mkazo huo vizuri zaidi, na utajua jinsi ya kuendelea kufanya hivyo. Usisahau kwamba kuna mafundisho mengine mazuri ya Yesu ambayo hayakuorodheshwa kwenye sanduku. Kwa nini usitafute baadhi ya mafundisho hayo na kujaribu kuyafuata?—Wafilipi 3:16.

  • Kitulizo Kinachofaa cha Mkazo
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Desemba 15
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12, 13]

      Mafundisho ya Kukusaidia

      Ni mambo gani mazuri unayoweza kupata katika Mathayo sura ya 5 hadi 7? Sura hizo zina mafundisho yaliyotolewa na Mwalimu Stadi, Yesu, akiwa kwenye ubavu wa kilima cha Galilaya. Tafadhali soma mistari inayoonyeshwa chini katika Biblia yako mwenyewe, kisha ujiulize maswali yanayohusiana na mistari hiyo.

      1. 5:3-9 Mistari hii inaniambia nini kuhusu mtazamo wangu kwa ujumla? Ninawezaje kujitahidi kupata furaha zaidi? Ninawezaje kukazia uangalifu zaidi mahitaji yangu ya kiroho?

      2. 5:25, 26 Ni afadhali kufanya nini kuliko kuiga roho ya ubishi inayoonyeshwa na watu wengi?—Luka 12:58, 59.

      3. 5:27-30 Maneno ya Yesu yanakazia nini kuhusu kuwaziawazia mambo ya kingono? Kuepuka kufanya hivyo kutanisaidiaje kuwa na furaha na amani ya akili?

      4. 5:38-42 Kwa nini nijitahidi kuepuka sifa ya watu wa siku hizi ya kushikilia maoni yao kupita kiasi?

      5. 5:43-48 Nitanufaikaje kwa kufahamiana zaidi na watu ambao huenda niliwaona kuwa adui? Yaelekea kufanya hivyo kutanisaidiaje kupunguza au kuondoa mkazo?

      6. 6:14, 15 Iwapo nyakati nyingine ninakuwa na mwelekeo wa kutosamehe, je, huenda ikawa ni kwa sababu nina wivu au kinyongo? Ninawezaje kubadili hali hiyo?

      7. 6:16-18 Je, nina mwelekeo wa kujishughulisha zaidi na sura yangu ya nje kuliko nilivyo moyoni? Ninapaswa kuwa mwangalifu zaidi kuhusu nini?

      8. 6:19-32 Matokeo yanaweza kuwa nini nikihangaikia zaidi pesa au mali? Nitadumisha usawaziko katika jambo hilo kwa kufikiria nini?

      9. 7:1-5 Ninahisije ninapokuwa karibu na watu wenye kushutumu na kuchambua, ambao sikuzote hutafuta-tafuta makosa? Kwa nini ni muhimu niepuke kuwa hivyo?

      10. 7:7-11 Ikiwa inafaa kuendelea kumwomba Mungu jambo fulani, mbona nisiwe na mtazamo kama huo katika hali nyingine maishani?—Luka 11:5-13.

      11. 7:12 Ingawa ninajua ile Kanuni Bora, ninaitumia mara nyingi kadiri gani ninaposhughulika na wengine?

      12. 7:24-27 Kwa kuwa maisha yangu yamo mikononi mwangu, ninawezaje kujitayarisha vizuri zaidi kwa ajili ya magumu na matatizo? Kwa nini nifikirie mambo hayo sasa?—Luka 6:46-49.

      Mafundisho mengine ninayoweza kufikiria:

      13. 8:2, 3 Ninawezaje kuwaonyesha huruma wale walio katika hali ngumu, kama Yesu alivyofanya mara nyingi?

      14. 9:9-38 Je, mimi huonyesha huruma, na ninaweza kuionyeshaje hata zaidi?

      15. 12:19 Ninapojifunza kutokana na unabii kumhusu Yesu, je, ninajitahidi kuepuka mabishano?

      16. 12:20, 21 Ninaweza kuwanufaishaje wengine kwa kutowaumiza kwa maneno au kwa matendo?

      17. 12:34-37 Mimi hutumia wakati mwingi nikizungumzia nini? Ninajua kwamba ninapokamua chungwa, ninapata maji ya chungwa, hivyo basi, kwa nini nifikirie yaliyo moyoni mwangu?—Marko 7:20-23.

      18. 15:4-6 Ninajifunza nini kutokana na maelezo ya Yesu kuhusu kuwatunza kwa upendo walio wazee?

      19. 19:13-15 Ninahitaji kuchukua wakati kufanya nini?

      20. 20:25-28 Kwa nini hainufaishi kutumia mamlaka isivyofaa. Ninawezaje kumwiga Yesu katika jambo hilo?

      Mafundisho mengine yaliyoandikwa na Marko:

      21. 4:24, 25 Kwa nini ni muhimu kufikiria jinsi ninavyowatendea wengine?

      22. 9:50 Ikiwa mambo ninayosema na kufanya yanafaa, inaelekea kutakuwa na matokeo gani mazuri?

      Hatimaye, mafundisho kadhaa yaliyoandikwa na Luka:

      23. 8:11, 14 Matokeo yatakuwa nini ikiwa wasiwasi, mali, au anasa zitatawala maisha yangu?

      24. 9:1-6 Yesu alitanguliza nini ingawa alikuwa na uwezo wa kuponya wagonjwa?

      25. 9:52-56 Je, ninaudhika upesi? Je, ninaepuka roho ya kutaka kulipiza kisasi?

      26. 9:62 Nioneje daraka langu la kuzungumza kuhusu Ufalme wa Mungu?

      27. 10:29-37 Ninaweza kuthibitishaje kwamba mimi ni jirani, wala si mtu asiyejali?

      28. 11:33-36 Ninapaswa kufanya mabadiliko gani ili maisha yangu yawe sahili zaidi?

      29. 12:15 Kuna uhusiano gani kati ya uhai na mali?

      30. 14:28-30 Iwapo ninachukua wakati kuchanganua maamuzi kwa makini, ninaweza kuepuka nini na matokeo yawe nini?

      31. 16:10-12 Ninaweza kupata manufaa gani kwa kudumisha uaminifu-maadili?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki