Wapiga-Mbiu ya Ufalme Waripoti
Alifuata Dhamiri Yake Iliyozoezwa na Biblia
MFALME Daudi wa Israeli alisali apate msaada wa Yehova aliposema hivi: “Ila mimi nitakwenda kwa ukamilifu [uaminifu wa maadili, NW] wangu, unikomboe, unifanyie fadhili.” (Zaburi 26:11) Mungu alimwonyesha fadhili kwa vile alidumisha uaminifu wake wa maadili. Yehova pia alimbariki Yesu kwa sababu alifanya mapenzi ya Baba yake wa kimbingu, Naye akambariki kijana mmoja nchini Kolombia aliyefuata dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia na aliyeazimia kufanya mapenzi ya Mungu. Kijana huyo aeleza hivi:
“Nilipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, nilikuwa mwanafunzi katika shule moja ya Katoliki. Lakini, dhamiri yangu ilinisumbua nilipohudhuria Misa, kwa hiyo nilienda kumwona mkuu wa shule (aliyekuwa padri), mshauri wa wanafunzi, na kiongozi wa kikundi chetu na kuomba ruhusa nisihudhurie Misa. Ingawa nilipewa ruhusa, watu fulani walijaribu kunilazimisha nihudhurie. Mkazo huo uliendelea hata baada tu ya ubatizo wangu kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Baba yangu alitisha kunifukuza nyumbani kama ningefukuzwa shuleni. Yeye alikusudia nisome mpaka chuo kikuu na kufuata kazi fulani ya maisha.
“Mkuu wa shule alionya mara kadhaa juu ya yeyote ambaye angekataa kufuata masharti ya Kikatoliki. Wakati ulipofika wa kuwa na Misa ya kwanza katika mwaka, nilijificha mpaka ikaisha. Kisha nikampa mwalimu (padri) nakala ya broshua Shule na Mashahidi wa Yehova nami nikamweleza kwamba nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, sikuweza kuhudhuria Misa. Yeye alisema hivi: ‘Afadhali uanze kutafuta shule nyingine.’ Nilijiua kwamba kama ningalifukuzwa shuleni baba yangu angalinifukuza nyumbani. Lakini nilisali kwa Yehova nami nikaendelea kuhubiria sana wanafunzi wenzangu.
“Likizo ikaja. Kisha nikarudi shuleni baada ya likizo, ukawa wakati mwingine tena wa Misa. Mkuu wa shule na mapadri wengine walikuwa mbele ya kanisa, wakiwa tayari kusikia maungamo. Karibu nishindwe sana na woga. Niliingia ndani na kuketi, lakini dhamiri yangu ilinisumbua. Wimbo ulipoanza, nikawaza hivi, ‘Ninafanya nini hapa? Yehova ndiye Mungu wangu. Siwezi kuwa mwoga na kukosa uaminifu-mshikamanifu. Siwezi kumwacha. Yeye hataniacha.’ Nikasali nipate ujasiri. Kisha nikaondoka kanisani na kusimama katika foleni ya wale waliokuwa wakienda kuungama dhambi zao. Nilipomfikia mkuu wa shule, nilimwambia hivi: ‘Mwalimu, sijakuja kuungama dhambi zangu.’ Yeye akasema: ‘Nilifikiria hivyo.’ Nikamwambia kwamba nilikuwa tayari kukabili yale yatakayotokea lakini dhamiri yangu haikuniruhusu nishiriki katika Misa. Siwezi kutenda kinyume cha mambo ambayo nilikuwa nimejifunza katika Biblia.
“Aliniangalia, akatabasamu, naye akasema: ‘Nakustahi sana. Nyinyi nyote mlio Mashahidi mnastahili kustahiwa. Kwenu, Mungu ndiye wa kwanza, na mko tayari kutii sheria zake chini ya hali zozote zile. Endeleeni kufanya hivyo. Mnafanya vizuri sana. Laiti Wakatoliki wote wangekuwa kama nyinyi, wakionyesha bidii, na upendo kama huo kuelekea Mungu. Tokea sasa hamlazimishwi kuhudhuria ibada zetu za kidini.’ Nilifurahi kama nini! Yehova alikuwa amebariki azimio langu la kutii dhamiri yangu iliyozoezwa na Biblia.
“Siku iliyofuata mkuu wa shule alieleza wanafunzi hivi: ‘Dini nyingine zinatushinda. Ni kwa nini sisi si kama wao, kuwa wenye bidii, kumpenda sana Mungu na kuwa na tamaa ya kumtumikia kuliko jambo jingine lolote? Hili ni jambo ambalo ni lazima litoke mioyoni mwetu.’
“Hatimaye mkuu huyo alihamishwa kikazi kwenda Rome, na mkuu mpya hakushughulika na hali yangu ya kutohudhuria ibada hizo. Baba yangu akahama nyumbani, nikibaki huru kutimiza mradi wangu wa huduma ya wakati wote baada tu ya kuhitimu.”
Yehova alimbariki huyo kijana aliyefuata dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia. Yeye atabariki vilevile wale wote wanaojaribu kufanya mapenzi yake.—Mithali 3:5, 6.