Alhamisi, Julai 17
Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.—Met. 17:17.
Maria, mama ya Yesu, alihitaji kutiwa nguvu. Angekuwa mjamzito, ingawa hakuwa amefunga ndoa. Hakuwa na uzoefu wa kulea watoto wake mwenyewe, lakini angemtunza mvulana ambaye baadaye angekuwa Masihi. Na kwa kuwa hakuwa amefanya ngono, Maria angemwelezaje jambo hilo Yosefu, mchumba wake? (Luka 1:26-33) Maria alipataje nguvu alizohitaji? Alitafuta msaada kutoka kwa watu wengine. Kwa mfano, alimwomba malaika Gabrieli ampe habari zaidi kuhusu mgawo huo. (Luka 1:34) Muda mfupi baada ya hapo, alisafiri kwenda kwenye “eneo lenye milima” la Yuda ili kumtembelea Elisabeti, mtu wake wa ukoo. Elisabeti alimpongeza Maria na aliongozwa na Yehova kusema unabii wenye kutia moyo kumhusu mwana wa Maria ambaye bado hakuwa amezaliwa. (Luka 1:39-45) Maria alisema kwamba Yehova alikuwa “amefanya mambo makuu kwa mkono wake.” (Luka 1:46-51) Kupitia malaika Gabrieli na Elisabeti, Yehova alimwimarisha Maria. w23.10 14-15 ¶10-12
Ijumaa, Julai 18
Alitufanya tuwe ufalme, makuhani kwa Mungu na Baba yake.—Ufu. 1:6.
Idadi hususa ya wanafunzi wa Kristo wametiwa mafuta kwa roho takatifu, nao wana uhusiano wa pekee pamoja na Yehova. Wakristo hao 144,000 watatumikia wakiwa makuhani mbinguni pamoja na Yesu. (Ufu. 14:1) Patakatifu pa hema la ibada panafananisha hali yao ya kuzaliwa kwa roho na kuwa wana wa Mungu wakiwa bado duniani. (Rom. 8:15-17) Patakatifu Zaidi pa hema la ibada panafananisha mbinguni, ambako Yehova anaishi. “Pazia” lililotenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi lilifananisha mwili wa kibinadamu wa Yesu ambao ulikuwa kizuizi cha kuingia mbinguni akiwa Kuhani Mkuu sana wa hekalu la kiroho. Kwa kuutoa uhai wake wa kibinadamu uwe dhabihu kwa ajili ya wanadamu, Yesu alifungua njia ya uhai wa mbinguni kwa ajili ya Wakristo watiwa-mafuta. Ili wapokee thawabu yao ya mbinguni, ni lazima wao pia wavue miili yao ya kibinadamu.—Ebr. 10:19, 20; 1 Kor. 15:50. w23.10 28 ¶13
Jumamosi, Julai 19
Nitakosa wakati nikiendelea kusimulia kuhusu Gideoni.—Ebr. 11:32.
Gideoni alijibu kwa upole Waefraimu walipomkosoa. (Amu. 8:1-3) Hakujibu kwa hasira. Alionyesha unyenyekevu wa akili kwa kusikiliza mahangaiko yao, na kwa busara alifaulu kutuliza hali hiyo. Wazee wenye hekima wanamwiga Gideoni kwa kusikiliza kwa makini na kujibu kwa upole wanapokosolewa. (Yak. 3:13) Wanapofanya hivyo, wanachangia amani kutanikoni. Gideoni aliposifiwa kwa kuwashinda Wamidiani, alimwelekezea Yehova sifa. (Amu. 8:22, 23) Wazee wanawezaje kumwiga Gideoni? Wanapaswa kumsifu Yehova kwa mambo wanayotimiza. (1 Kor. 4:6, 7) Kwa mfano, mzee anaposifiwa kwa sababu ya uwezo wake wa kufundisha, anaweza kusema kwamba chanzo cha mwongozo huo ni Neno la Mungu, na sisi sote tunapata mazoezi katika tengenezo la Yehova. Nyakati nyingine, wazee wanaweza kujichunguza ili kuona kama wanajielekezea fikira. w23.06 4 ¶7-8