Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • es25 kur. 98-108
  • Oktoba

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Oktoba
  • Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025
  • Vichwa vidogo
  • Jumatano, Oktoba 1
  • Alhamisi, Oktoba 2
  • Ijumaa, Oktoba 3
  • Jumamosi, Oktoba 4
  • Jumapili, Oktoba 5
  • Jumatatu, Oktoba 6
  • Jumanne, Oktoba 7
  • Jumatano, Oktoba 8
  • Alhamisi, Oktoba 9
  • Ijumaa, Oktoba 10
  • Jumamosi, Oktoba 11
  • Jumapili, Oktoba 12
  • Jumatatu, Oktoba 13
  • Jumanne, Oktoba 14
  • Jumatano, Oktoba 15
  • Alhamisi, Oktoba 16
  • Ijumaa, Oktoba 17
  • Jumamosi, Oktoba 18
  • Jumapili, Oktoba 19
  • Jumatatu, Oktoba 20
  • Jumanne, Oktoba 21
  • Jumatano, Oktoba 22
  • Alhamisi, Oktoba 23
  • Ijumaa, Oktoba 24
  • Jumamosi, Oktoba 25
  • Jumapili, Oktoba 26
  • Jumatatu, Oktoba 27
  • Jumanne, Oktoba 28
  • Jumatano, Oktoba 29
  • Alhamisi, Oktoba 30
  • Ijumaa, Oktoba 31
Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025
es25 kur. 98-108

Oktoba

Jumatano, Oktoba 1

Hekima inayotoka juu . . . [iko] tayari kutii.—Yak. 3:17.

Je, wakati mwingine ni vigumu kwako kutii? Mfalme Daudi alikabili changamoto hiyo naye alisali hivi kwa Mungu: “Chochea ndani yangu utayari wa kukutii.” (Zab. 51:12) Daudi alimpenda Yehova. Hata hivyo, wakati mwingine ilikuwa vigumu kwake kutii, na inakuwa hivyo pia kwetu. Kwa nini? Kwanza, tumerithi mwelekeo wa kutotii. Pili, sikuzote Shetani anajaribu kutuchochea tuasi, kama yeye alivyofanya. (2 Kor. 11:3) Tatu, tumezungukwa na ulimwengu huu wenye roho ya uasi, “roho ambayo sasa inafanya kazi katika wana wa kutotii.” (Efe. 2:2) Tunapaswa kujitahidi kushinda mwelekeo wetu wa kutenda dhambi na pia kupinga mkazo wa kutotii unaotoka kwa Ibilisi na ulimwengu huu. Tunapaswa kujitahidi kumtii Yehova na wale ambao amewapatia mamlaka. w23.10 6 ¶1

Alhamisi, Oktoba 2

Lakini wewe umehifadhi divai nzuri mpaka sasa.—Yoh. 2:10.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na muujiza wa Yesu wa kugeuza maji kuwa divai? Tunajifunza somo kuhusu unyenyekevu. Yesu hakujigamba kuhusu muujiza huo; kwa kweli, hakujigamba kamwe kuhusu mambo aliyotimiza. Kinyume chake, kwa unyenyekevu, tena na tena alimpa sifa na utukufu Baba yake. (Yoh. 5:​19, 30; 8:28) Ikiwa tutamwiga Yesu kwa kuwa wanyenyekevu, hatutajigamba kuhusu mambo tunayotimiza. Acheni tujigambe si kujihusu sisi wenyewe, bali kumhusu Mungu mwenye kustaajabisha ambaye tuna pendeleo la kumtumikia. (Yer. 9:​23, 24) Acheni tumpe sifa anazostahili. Isitoshe, hatuwezi kamwe kutimiza jambo lolote zuri bila msaada wa Yehova? (1 Kor. 1:​26-31) Tunapokuwa wanyenyekevu, hatujitafutii sifa kwa mambo mazuri tunayowafanyia wengine. Tunaridhika kujua kwamba Yehova anaona na kuthamini mambo tunayofanya. (Linganisha Mathayo 6:​2-4; Ebr. 13:16) Kwa kweli, tunamfurahisha Yehova tunapomwiga Yesu kwa kuonyesha unyenyekevu.—1 Pet. 5:6. w23.04 4 ¶9; 5 ¶11-12

Ijumaa, Oktoba 3

Mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.—Flp. 2:4.

Akiongozwa na roho, mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo waangalie faida za wengine. Tunaweza kutumiaje shauri hilo kwenye mikutano? Kwa kukumbuka kwamba kama sisi, wengine pia wanataka kutoka maelezo. Fikiria jambo hili. Unapokuwa na mazungumzo pamoja na rafiki zako, je, unazungumza sana hivi kwamba wanakosa nafasi ya kuzungumza? La hasha! Unataka washiriki katika mazungumzo. Vivyo hivyo, kwenye mikutano, tungependa kuwapa wengi iwezekanavyo fursa ya kutoa maelezo. Kwa kweli, mojawapo ya njia bora zaidi ya kuwatia moyo ndugu na dada zetu, ni kuwapa nafasi ya kueleza imani yao. (1 Kor. 10:24) Toa maelezo mafupi, na hivyo utawapa watu wengi zaidi muda wa kushiriki. Hata unapotoa maelezo mafupi, epuka kuzungumzia mambo mengi sana. Ukizungumzia kila jambo linalotajwa kwenye fungu, wengine watakosa jambo la kusema. w23.04 22-23 ¶11-13

Jumamosi, Oktoba 4

Ninafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili niishiriki pamoja na wengine.—1 Kor. 9:23.

Tunapaswa kukumbuka kwamba ni jambo muhimu kuendelea kuwasaidia wengine, hasa kupitia huduma yetu ya Kikristo. Katika huduma yetu, tunahitaji kunyumbulika. Tunakutana na watu wenye imani na mitazamo mbalimbali na wanaotoka katika malezi mbalimbali. Mtume Paulo alibadilikana kulingana na hali na tunaweza kuiga mfano wake. Yesu alimweka rasmi Paulo kuwa “mtume kwa mataifa.” (Rom. 11:13) Akiwa na jukumu hilo, Paulo aliwahubiria Wayahudi, Wagiriki, watu wenye elimu, wakulima, watu walioheshimiwa, na wafalme. Ili kugusa mioyo ya watu hao mbalimbali, Paulo alikuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote.” (1 Kor. 9:​19-22) Alizingatia utamaduni, malezi, na imani ya wasikilizaji wake, na kubadilisha njia yake ya kuhubiri ili iwafae. Sisi pia tunaweza kupata matokeo mazuri katika huduma ikiwa tutakuwa tayari kubadili mazungumzo yetu ili yalingane na mahitaji ya wasikilizaji wetu. w23.07 23 ¶11-12

Jumapili, Oktoba 5

Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote.—2 Tim. 2:24.

Sifa ya upole si udhaifu, bali inaonyesha kwamba mtu ana nguvu. Tunahitaji kuwa na nguvu za kujidhibiti ili kuendelea kuwa watulivu tunapokabili hali ngumu. Upole ni moja kati ya sifa za “tunda la roho.” (Gal. 5:​22, 23) Neno fulani la Kigiriki ambalo lilitafsiriwa kuwa “upole,” wakati mwingine lilitumiwa kufafanua farasi wa mwituni ambaye alizoezwa na kuwa mnyama wa kufugwa. Wazia farasi wa mwituni ambaye anakuwa mpole. Mnyama huyo ni mpole lakini ana nguvu. Tukiwa wanadamu, tunawezaje kusitawisha sifa ya upole na wakati huohuo kuwa wenye nguvu? Hatuwezi kufanya hivyo kwa nguvu zetu. Tunahitaji kumwomba Mungu atupe roho yake na kumwomba atusaidie kusitawisha sifa hii maridadi. Mambo yaliyoonwa yanathibitisha kwamba hilo linawezekana. Mashahidi wengi wamejibu kwa upole wanapokabiliana na wapinzani na hilo limewafanya wengi wawe na maoni yanayofaa kutuhusu.—2 Tim. 2:​24, 25. w23.09 15 ¶3

Jumatatu, Oktoba 6

Nilisali nipate mvulana huyu, naye Yehova akanipa nilichoomba.—1 Sam. 1:27.

Katika maono yenye kustaajabisha, mtume Yohana aliwaona wazee 24 mbinguni wakimwabudu Yehova. Walimsifu Mungu na kusema kwamba anastahili kupokea “utukufu na heshima na nguvu.” (Ufu. 4:​10, 11) Pia, malaika waaminifu wana sababu nyingi za kumsifu na kumtukuza Yehova. Wanaishi pamoja naye mbinguni na wanamjua vizuri. Wanaona sifa zake kupitia mambo anayofanya. Wanapomwona Yehova akitenda, wanachochewa kumsifu. (Ayu. 38:​4-7) Sisi pia tungependa kumsifu Yehova katika sala zetu, tukitaja mambo tunayopenda na kuthamini kumhusu. Unaposoma na kujifunza Biblia, jaribu kutambua sifa za Yehova ambazo hasa unavutiwa nazo. (Ayu. 37:23; Rom. 11:33) Kisha umwambie Yehova jinsi unavyohisi kuhusu sifa hizo. Pia, tunaweza kumsifu Yehova kwa sababu ya jinsi ambavyo ametusaidia na kuwasaidia ndugu na dada zetu wote Wakristo.—1 Sam. 2:​1, 2. w23.05 3-4 ¶6-7

Jumanne, Oktoba 7

Mtembee kwa kumstahili Yehova.—Kol. 1:10.

Mwaka wa 1919, watu wa Mungu waliwekwa huru kutoka katika Babiloni Mkubwa. Mwaka huo, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” alianza kufanya kazi ili watu wenye mioyo minyoofu waanze kutembea katika ‘Njia hiyo mpya ya Utakatifu’ iliyofunguliwa. (Mt. 24:​45-47; Isa. 35:8) Kazi iliyofanywa na “watengeneza-barabara” waliotangulia, iliwasaidia wale walioanza kutembea katika barabara hiyo kuu wajifunze mengi zaidi kumhusu Yehova na makusudi yake. (Met. 4:18) Pia, wangeweza kupatanisha maisha yao na viwango vya Yehova. Yehova hakutarajia watu wake wafanye marekebisho yote yaliyohitajika kwa wakati mmoja. Badala yake, amekuwa akiwasafisha watu wake hatua kwa hatua. Tutafurahi sana wakati ambapo tutaweza kumfurahisha Mungu wetu katika kila jambo tunalofanya! Kila barabara inahitaji kudumishwa kwa ukawaida. Tangu mwaka wa 1919, kazi ya kutengeneza “Njia ya Utakatifu” imekuwa ikiendelea, ili kufanya iwezekane kwa watu wengi zaidi kuondoka katika Babiloni Mkubwa. w23.05 17 ¶15; 19 ¶16

Jumatano, Oktoba 8

Sitakuacha kamwe.—Ebr. 13:5.

Washiriki wa Baraza Linaloongoza wamekuwa wakiwazoeza kibinafsi wasaidizi katika halmashauri mbalimbali za Baraza Linaloongoza. Kwa sasa wasaidizi hao wanashughulikia majukumu mazito kwa uaminifu. Wako tayari kabisa kuendeleza kazi ya kuwatunza kondoo wa Kristo. Watiwa-mafuta wa mwisho watakapochukuliwa na kwenda mbinguni mwishoni mwa ile dhiki kuu, ibada safi itaendelea hapa duniani. Kwa sababu ya uongozi mzuri wa Yesu Kristo, waabudu wa Mungu hawatakosa chochote. Ni kweli kwamba wakati huo tutakuwa tukishambuliwa na Gogu wa Magogu, muungano wa mataifa yenye chuki. (Eze. 38:​18-20) Lakini shambulizi hilo fupi halitafaulu; halitawafanya watu wa Mungu waache kumwabudu Yehova. Bila shaka atawaokoa! Katika maono, mtume Yohana aliona “umati mkubwa” wa kondoo wengine wa Kristo. Yohana aliambiwa kwamba ‘umati huo mkubwa’ unatoka “katika ile dhiki kuu.” (Ufu. 7:​9, 14) Naam, tuna uhakika kwamba watakuwa salama! w24.02 5-6 ¶13-14

Alhamisi, Oktoba 9

Msiuzime moto wa roho.—1 The. 5:19.

Tunaweza kufanya nini ili tupokee roho takatifu? Tunaweza kusali ili tupate roho takatifu, kujifunza Neno la Mungu lililoongozwa na roho, na kushirikiana na tengenezo lake linaloongozwa na roho. Kufanya hivyo, kutatusaidia kusitawisha sifa za “tunda la roho.” (Gal. 5:​22, 23) Mungu huwapa roho yake wale tu ambao wanadumisha mawazo safi na mwenendo safi. Hataendelea kutupatia roho yake ikiwa tutaendelea kuwa na mawazo yasiyo safi na kutenda kulingana na mawazo hayo. (1 The. 4:​7, 8) Ili tuendelee kupokea roho takatifu, pia hatupaswi ‘kuutendea unabii kwa dharau.’ (1 The. 5:20) Hapa “unabii” unamaanisha ujumbe uliotokezwa na roho ya Mungu, kutia ndani ujumbe kuhusu siku ya Yehova na uhitaji wa kutenda haraka katika nyakati zetu. Hatuahirishi siku hiyo katika akili zetu na kufikiri kwamba Har–​Magedoni haitakuja tukiwa hai. Badala yake, tunaiweka karibu akilini kwa kudumisha mwenendo unaofaa na kuendelea kuwa na bidii katika “vitendo vya ujitoaji-kimungu.”—2 Pet. 3:​11, 12. w23.06 12 ¶13-14

Ijumaa, Oktoba 10

Kumwogopa Yehova ndio mwanzo wa hekima.—Met. 9:10.

Tukiwa Wakristo, tunapaswa kufanya nini ikiwa picha ya ponografia itatokea bila kutarajia kwenye kifaa chetu cha kielektroni? Tunapaswa kuacha mara moja kutazama picha hiyo. Itakuwa rahisi kufanya hivyo ikiwa tutakumbuka kwamba uhusiano wetu pamoja na Yehova ndilo jambo lenye thamani zaidi kwetu. Hata baadhi ya picha ambazo hazionwi kuwa za ponografia zinaweza kuchochea hamu ya ngono. Kwa nini tunapaswa kuziepuka? Kwa sababu hatungependa hata kuwazia kufanya uasherati katika moyo wetu. (Mt. 5:​28, 29) David, mzee wa kutaniko anayeishi nchini Thailand, anasema hivi: “Mimi hujiuliza: ‘Ingawa picha hizo si ponografia, je, nitamfurahisha Yehova ikiwa nitaendelea kuzitazama?’ Kufikiria kwa njia hiyo hunisaidia kutenda kwa hekima.” Tutatenda kwa hekima ikiwa tutasitawisha woga unaofaa kwa kuepuka kufanya jambo linalomchukiza Yehova. Kumwogopa Mungu ndio “mwanzo,” au msingi, “wa hekima.” w23.06 23 ¶12-13

Jumamosi, Oktoba 11

Nendeni, watu wangu, ingieni katika vyumba vyenu vya ndani.—Isa. 26:20.

Huenda ‘vyumba vya ndani’ vinarejelea makutaniko yetu. Wakati wa dhiki kuu, tutapata ulinzi ambao Yehova ametuahidi ikiwa tutadumisha umoja na waabudu wenzetu. Kwa hiyo, tunapaswa kujitahidi sasa, si kuwavumilia tu ndugu na dada zetu, bali kuwa na upendo mwingi kuwaelekea. Huenda wokovu wetu utategemea jambo hilo! “Ile siku kuu ya Yehova” itawasababishia wanadamu taabu. (Sef. 1:​14, 15) Watu wa Yehova pia watapatwa na mateso. Lakini ikiwa tutajitayarisha sasa tutafaulu kuendelea kuwa watulivu na kuwasaidia wengine. Tutavumilia matatizo yoyote ambayo tutakabili. Waabudu wenzetu wakiteseka, tutajitahidi kuwasaidia kwa kuwaonyesha huruma na kwa kuwaandalia mahitaji yao. Na tutakaa karibu na ndugu na dada zetu ambao tayari tumesitawisha upendo kuwaelekea. Kisha Yehova atatuthawabisha kwa kutupatia uzima wa milele katika ulimwengu ambao hautakuwa na msiba wala dhiki yoyote.—Isa. 65:17. w23.07 7 ¶16-17

Jumapili, Oktoba 12

[Yehova] atawafanya muwe imara, atawatia nguvu, atawapa msingi imara.—1 Pet. 5:10.

Mara nyingi, Neno la Mungu huwafafanua wanaume waaminifu kuwa wenye nguvu. Lakini hata wale waliokuwa na nguvu zaidi miongoni mwao hawakuhisi kwamba wana nguvu sikuzote. Kwa mfano, pindi fulani Mfalme Daudi alihisi kwamba alikuwa “imara kama mlima,” lakini katika pindi nyingine ‘aliogopa.’ (Zab. 30:7) Ingawa Samsoni alikuwa na nguvu nyingi zisizo za kawaida alipochochewa na roho ya Mungu, alitambua kwamba bila kupata nguvu zinazotoka kwa Mungu, angekuwa dhaifu kama wanadamu wengine wote. (Amu. 14:​5, 6; 16:17) Wanaume hao waaminifu walikuwa na nguvu kwa sababu tu Yehova aliwapa nguvu. Mtume Paulo alisema kwamba yeye pia alihitaji nguvu kutoka kwa Yehova. (2 Kor. 12:​9, 10) Alipambana na matatizo ya kiafya. (Gal. 4:​13, 14) Pia, wakati mwingine ilikuwa vigumu kwake kufanya mambo yaliyo sawa. (Rom. 7:​18, 19) Na wakati mwingine alikuwa na wasiwasi na hakuwa na uhakika kuhusu mambo ambayo yangempata. (2 Kor. 1:​8, 9) Ingawa hivyo, Paulo alipokuwa dhaifu, alikuwa mwenye nguvu. Jinsi gani? Yehova alimpa Paulo nguvu alizohitaji. Alimwimarisha Paulo. w23.10 12 ¶1-2

Jumatatu, Oktoba 13

Yehova huona ndani ya moyo.—1 Sam. 16:7.

Ikiwa pindi fulani tunapambana na hisia za kujiona hatufai, tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova mwenyewe anatuvuta kwake. (Yoh. 6:44) Anaona sifa nzuri tulizo nazo ambazo huenda sisi wenyewe hatuzioni na anaujua moyo wetu. (2 Nya. 6:30) Hivyo, tunaweza kumwamini anaposema sisi ni wenye thamani. (1 Yoh. 3:​19, 20) Kabla ya kujifunza kweli, baadhi yetu tulifanya mambo ambayo huenda bado yanafanya tujihisi tukiwa na hatia. (1 Pet. 4:3) Hata Wakristo waaminifu wanapambana na mwelekeo wa kutenda dhambi. Je, moyo wako unakuhukumu? Ikiwa ndivyo, unaweza kutiwa moyo kujua kwamba watumishi wengine waaminifu wa Yehova wamekabiliana na hisia hizo pia. Kwa mfano, mtume Paulo alijihisi vibaya alipofikiria kuhusu udhaifu wake. (Rom. 7:24) Paulo alikuwa ametubu dhambi zake na kubatizwa. Hata hivyo, alijirejelea kuwa “mdogo zaidi kati ya mitume” na mtenda dhambi “wa kwanza kabisa.”—1 Kor. 15:9; 1 Tim. 1:15. w24.03 27 ¶5-6

Jumanne, Oktoba 14

Waliiacha nyumba ya Yehova.—2 Nya. 24:18.

Somo moja ambalo tunaweza kujifunza kutokana na uamuzi mbaya wa Mfalme Yehoashi ni kwamba tunahitaji kuchagua marafiki ambao watatuchochea kufanya mambo mazuri—marafiki ambao wanampenda Yehova na wanaotaka kumfurahisha. Hatuhitaji kuchagua tu marafiki wenye umri kama wetu. Kumbuka kwamba Yehoashi alikuwa na umri mdogo sana kuliko rafiki yake, Yehoyada. Jiulize hivi kuhusu marafiki unaochagua: ‘Je, wananisaidia kuimarisha imani yangu kwa Yehova? Je, wananitia moyo kuishi kulingana na viwango vya Mungu? Je, wanazungumza kumhusu Yehova na kweli zake zenye thamani? Je, wanaheshimu viwango vya Mungu? Je, wananiambia tu mambo ambayo ninapenda kusikia au je, wana ujasiri wa kunirekebisha ninapokosea?’ (Met. 27:​5, 6, 17) Kwa kweli, ikiwa rafiki zako hawampendi Yehova, huwahitaji. Lakini ikiwa una marafiki ambao wanampenda Yehova, shikamana nao—watakusaidia kufanya mambo yanayofaa!—Met. 13:20. w23.09 9-10 ¶6-7

Jumatano, Oktoba 15

Mimi ndiye Alfa na Omega.—Ufu. 1:8.

Herufi alfa ndiyo ya kwanza katika alfabeti ya Kigiriki, na herufi omega ndiyo ya mwisho. Kwa kusema kwamba yeye ndiye “Alfa na Omega,” Yehova anatusaidia kuelewa kwamba anapoanza kufanya jambo fulani, lazima alikamilishe kwa mafanikio. Baada ya kuwaumba Adamu na Hawa, Yehova alisema hivi: “Zaeni, muwe wengi, muijaze dunia na kuitiisha.” (Mwa. 1:28) Wakati huo ni kama Yehova alikuwa akisema “Alfa.” Alieleza waziwazi kusudi lake kwamba wakati utafika ambapo dunia itajaa wazao wa Adamu na Hawa walio wakamilifu na watiifu, ambao wataigeuza dunia kuwa paradiso. Wakati huo ujao, kusudi lake litakapotimia, ni kana kwamba atasema “Omega.” Baada ya kukamilisha uumbaji wa “mbingu na dunia na kila kitu kilichomo,” Yehova alitoa uhakikisho huu. Alitoa uhakikisho kwamba atatimiza kusudi lake kwa ajili ya wanadamu na dunia. Lingetimizwa kikamili mwishoni mwa ile siku ya saba.—Mwa. 2:​1-3. w23.11 5 ¶13-14

Alhamisi, Oktoba 16

Fungueni njia ya Yehova! Tengenezeni barabara kuu iliyonyooka inayopitia jangwani kwa ajili ya Mungu wetu.—Isa. 40:3.

Safari ngumu kutoka Babiloni kwenda Israeli ingechukua miezi minne hivi, lakini Yehova aliahidi kwamba kizuizi chochote ambacho kingeonekana kuwa kinazuia safari hiyo kingeondolewa. Wayahudi waaminifu walijua kwamba ikiwa wangerudi katika nchi ya Israeli wangepata baraka nyingi kuliko jambo lolote ambalo wangedhabihu. Baraka kuu zaidi ilihusiana na ibada yao. Hakukuwa na hekalu la Yehova katika jiji la Babiloni. Hakukuwa na madhabahu ambayo Waisraeli wangetoa dhabihu zilizotajwa katika Sheria ya Musa, na hakukuwa na mpango wa makuhani ambao wangetoa dhabihu hizo. Isitoshe watumishi wa Yehova walikuwa wachache kwa kulinganishwa na idadi kubwa sana ya watu ambao waliabudu miungu ya uwongo, na ambao hawakumheshimu Yehova na viwango vyake. Basi, maelfu ya Wayahudi waliomwogopa Mungu, walitazamia kwa hamu kurudi katika nchi yao ambako wangerudisha ibada safi. w23.05 14-15 ¶3-4

Ijumaa, Oktoba 17

Endeleeni kutembea kama watoto wa nuru.—Efe. 5:8.

Tunahitaji msaada wa roho takatifu ya Mungu ili tuweze kuendelea kujiendesha “kama watoto wa nuru.” Kwa nini? Kwa sababu si rahisi kuendelea kuwa safi katika ulimwengu huu uliopotoka kimaadili. (1 The. 4:​3-5, 7, 8) Roho takatifu inaweza kutusaidia kupambana na mawazo ya ulimwengu, kutia ndani falsafa zake na maoni yake yanayopingana na mawazo ya Mungu. Roho takatifu pia inaweza kutusaidia kutokeza “kila namna ya wema na uadilifu.” (Efe. 5:9) Njia moja tunayoweza kupata roho takatifu ni kwa kumwomba Yehova. Yesu alisema kwamba Yehova ‘atawapa roho takatifu wale wanaomwomba.’ (Luka 11:13) Na tunapomsifu Yehova pamoja kwenye mikutano ya Kikristo, tunapokea pia roho takatifu. (Efe. 5:​19, 20) Na roho takatifu ya Mungu itatuchochea tuishi kwa njia inayompendeza Mungu. w24.03 23-24 ¶13-15

Jumamosi, Oktoba 18

Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa.—Luka 11:9.

Je, unahitaji kuwa mwenye subira zaidi? Ikiwa ndivyo, sali ili uwe mwenye subira zaidi. Subira ni moja kati ya sifa za tunda la roho. (Gal. 5:​22, 23) Basi, tunaweza kusali ili tupate roho takatifu na kumwomba Yehova atusaidie kusitawisha sifa za tunda la roho. Tunapokabili hali inayofanya iwe vigumu kwetu kuwa wenye subira, ‘tunaendelea kuomba’ tupewe roho takatifu ili itusaidie kuwa wenye subira. (Luka 11:13) Pia, tunaweza kumwomba Yehova atusaidie kuona mambo kulingana na maoni yake. Kisha, baada ya kusali, tunapaswa kujitahidi kabisa kuonyesha subira kila siku. Kadiri tunavyosali ili tuwe na subira na kujitahidi kuwa wenye subira, ndivyo sifa hiyo itakavyozidi kutia mizizi katika mioyo yetu na kuwa sehemu ya utu wetu. Kutafakari mifano iliyo katika Biblia kutatusaidia pia. Biblia ina mifano ya watu wengi ambao walikuwa na subira. Tunapotafakari kuhusu masimulizi hayo, tunaweza kujifunza njia za kuonyesha subira. w23.08 22 ¶10-11

Jumapili, Oktoba 19

Mshushe nyavu zenu, mvue samaki.—Luka 5:4.

Yesu alimhakikishia mtume Petro kwamba Yehova angemtegemeza. Yesu aliyefufuliwa alimsaidia Petro na mitume wenzake kuvua tena samaki kimuujiza. (Yoh. 21:​4-6) Bila shaka, muujiza huo ulimhakikishia Petro kwamba Yehova angemwandalia mahitaji yake ya kimwili. Labda mtume huyo alikumbuka maneno ya Yesu kwamba Yehova angewaandalia wale ambao wanaendelea “kuutafuta kwanza Ufalme.” (Mt. 6:33) Hilo lilimsaidia Petro kutanguliza huduma maishani badala ya kazi ya kuvua samaki. Alitoa ushahidi kwa ujasiri siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K., na kuwasaidia maelfu kukubali habari njema. (Mdo. 2:​14, 37-41) Baadaye, aliwasaidia Wasamaria na Watu wa Mataifa kuwa Wakristo. (Mdo. 8:​14-17; 10:​44-48) Bila shaka, Yehova alimtumia Petro kwa njia kubwa kuwasaidia watu wa kila namna wajiunge na kutaniko. w23.09 20 ¶1; 23 ¶11

Jumatatu, Oktoba 20

Msiponiambia ndoto yangu na kunieleza maana yake, mtakatwa vipandevipande.—Dan. 2:5.

Karibu miaka miwili baada ya Wababiloni kuharibu jiji la Yerusalemu, Mfalme Nebukadneza wa Babiloni aliota ndoto yenye kutisha kuhusu sanamu kubwa sana. Alitishia kuwaua wanaume wake wote wenye hekima, kutia ndani Danieli, ikiwa hawangemwambia ndoto aliyoota na pia ufafanuzi wake. (Dan. 2:​3-5) Danieli alihitaji kutenda haraka; la sivyo, watu wengi wangekufa. Alienda “na kumwomba mfalme ampe muda ili amweleze maana ya ndoto yake.” (Dan. 2:16) Hilo lilihitaji ujasiri na imani. Biblia haina habari zozote zinazoonyesha kwamba Danieli alikuwa amewahi kufafanua ndoto kabla ya wakati huo. Aliwaomba rafiki zake “wasali ili Mungu wa mbinguni awaonyeshe rehema na kuwajulisha siri hiyo.” (Dan. 2:18) Yehova alijibu sala hizo. Kwa msaada wa Mungu, Danieli alifafanua ndoto ya Nebukadneza. Uhai wa Danieli na rafiki zake uliokolewa. w23.08 3 ¶4

Jumanne, Oktoba 21

Yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.—Mt. 24:13.

Fikiria manufaa ya kuonyesha subira. Tunapoonyesha subira, tunakuwa wenye furaha na watulivu zaidi. Hivyo, subira inaweza kutusaidia tuwe na hali nzuri kiakili na kimwili. Tunapowaonyesha wengine subira, tunakuwa na uhusiano mzuri zaidi pamoja nao. Kutaniko letu linakuwa na umoja zaidi. Ikiwa mtu fulani atatuudhi, hatutakasirika upesi na hivyo tutazuia hali isiwe mbaya zaidi. (Zab. 37:​8, maelezo ya chini; Met. 14:29) Lakini jambo muhimu zaidi, tunamwiga Baba yetu wa mbinguni na kumkaribia hata zaidi. Subira ni sifa yenye kupendeza na ambayo inatunufaisha sana! Ingawa huenda isiwe rahisi sikuzote kuonyesha subira, kwa msaada wa Yehova tunaweza kuendelea kusitawisha sifa hiyo. Na tunapoendelea kuungoja ulimwengu mpya kwa subira, tunaweza kuwa na uhakika kwamba “jicho la Yehova linawalinda wale wanaomwogopa, wale wanaongojea upendo wake mshikamanifu.” (Zab. 33:18) Acheni sisi sote tuazimie kuendelea kujivika subira. w23.08 22 ¶7; 25 ¶16-17

Jumatano, Oktoba 22

Imani bila matendo imekufa.—Yak. 2:17.

Yakobo alionyesha kwamba huenda mtu akadai kwamba ana imani, lakini matendo yake hayathibitishi hilo. (Yak. 2:​1-5, 9) Yakobo pia anamtaja mtu aliyemwona ‘ndugu au dada asiye na nguo au chakula’ lakini hakumsaidia. Hata ikiwa mtu huyo alidai kwamba ana imani, hakuionyesha kwa matendo; hivyo, imani yake ni bure. (Yak. 2:​14-16) Yakobo alimrejelea Rahabu kuwa mfano mzuri wa mtu aliyeonyesha imani kwa matendo. (Yak. 2:​25, 26.) Rahabu alikuwa amesikia kumhusu Yehova na alitambua kwamba alikuwa akiwategemeza Waisraeli. (Yos. 2:​9-11) Rahabu alionyesha imani yake kwa matendo—aliwalinda wapelelezi wawili Waisraeli, maisha yao yalipokuwa hatarini. Kwa sababu hiyo, mwanamke huyo asiye Mwisraeli ambaye hakuwa mkamilifu, alitangazwa kuwa mwadilifu kama Abrahamu. Mfano alioweka unakazia umuhimu wa kuonyesha imani kwa matendo. w23.12 5-6 ¶12-13

Alhamisi, Oktoba 23

Iweni na mizizi na kuimarishwa juu ya ule msingi.—Efe. 3:17.

Tukiwa Wakristo, haturidhiki kujua mambo ya msingi tu kuhusu Biblia. Kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu, tunatamani kujifunza “hata mambo mazito ya Mungu.” (1 Kor. 2:​9, 10) Kwa nini usianze mradi wa kujifunza kibinafsi ambao utakusaidia kumkaribia Yehova hata zaidi? Kwa mfano, unaweza kuchunguza jinsi alivyowaonyesha upendo watumishi wake wa zamani na jinsi hilo linavyothibitisha kwamba anakupenda wewe pia. Unaweza kuchunguza mpango wa ibada ambao Yehova aliweka katika Israeli la kale na jinsi tunavyomwabudu leo tukiwa Wakristo. Au labda unaweza kujifunza kwa undani unabii mbalimbali ambao Yesu alitimiza wakati wa maisha na huduma yake hapa duniani. Unaweza kupata shangwe nyingi kwa kujifunza habari hizo kwa msaada wa Fahirisi au Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova. Kujifunza Biblia kwa kina kunaweza kuimarisha imani yako na kukusaidia upate “ujuzi kumhusu Mungu.”—Met. 2:​4, 5. w23.10 18-19 ¶3-5

Ijumaa, Oktoba 24

Zaidi ya mambo yote, pendaneni sana, kwa sababu upendo hufunika dhambi nyingi.—1 Pet. 4:8.

Neno linalotafsiriwa kuwa “sana” ambalo mtume Petro ametumia, kihalisi linamaanisha “kujinyoosha” au “kuvutika.” Sehemu ya pili ya mstari huo inafafanua matokeo ya kupendana sana. Tukiwapenda sana ndugu zetu tutafunika dhambi zao. Tunaweza kuwazia hali hiyo kwa njia hii: Tunaushika upendo wetu kwa mikono miwili, kana kwamba tumeshika kitambaa kinachovutika, na tunakivuta zaidi na zaidi hadi kinafunika, si dhambi moja au mbili, bali “dhambi nyingi.” Kufunika kunamaanisha kusamehe. Kama kitambaa kinavyoweza kufunika doa, upendo unaweza kufunika udhaifu na kutokamilika kwa wengine. Upendo wetu kwa wengine unapaswa kuwa na nguvu sana hivi kwamba tunaweza kusamehe kutokamilika kwa waabudu wenzetu—hata ikiwa ni vigumu kufanya hivyo. (Kol. 3:13) Tunapowasamehe wengine, tunaonyesha kwamba upendo wetu ni wenye nguvu na tunataka kumfurahisha Yehova. w23.11 11-12 ¶13-15

Jumamosi, Oktoba 25

Shafani akaanza kukisoma mbele ya mfalme.—2 Nya. 34:18.

Alipokuwa na umri wa miaka 26, Mfalme Yosia alianza kazi ya kurekebisha hekalu. Kazi hiyo ilipokuwa ikiendelea, “kitabu cha Sheria ya Yehova kilichotolewa kupitia Musa” kilipatikana. Mfalme aliposikia kikisomwa, alichochewa kuchukua hatua na kutenda kulingana na mambo yaliyoandikwa humo. (2 Nya. 34:​14, 19-21) Je, ungependa kusoma Biblia kwa ukawaida? Ikiwa tayari unafanya hivyo je, unafurahia? Je, unaweka kumbukumbu ya mistari ambayo inaweza kukusaidia kibinafsi? Yosia alipokuwa na umri wa miaka 39, alifanya uamuzi mbaya uliomsababishia kifo. Alijitegemea mwenyewe badala ya kumwomba Yehova mwongozo. (2 Nya. 35:​20-25) Tunapata somo fulani hapa. Hata iwe tuna umri gani au tumekuwa tukijifunza Biblia kwa muda mrefu kadiri gani, tunapaswa kuendelea kumtafuta Yehova. Hilo linatia ndani kusali kwake kwa ukawaida ili kupata mwongozo, kujifunza Neno lake, na kusikiliza ushauri wa Wakristo wakomavu. Tukifanya hivyo, tutapunguza uwezekano wa kufanya makosa mazito na tutakuwa wenye furaha zaidi.—Yak. 1:25. w23.09 12 ¶15-16

Jumapili, Oktoba 26

Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.—Yak. 4:6.

Biblia inawataja wanawake wengi wa pekee waliompenda Yehova na kumtumikia. Wanawake hao walikuwa “wenye kiasi katika mazoea” na “waaminifu katika mambo yote.” (1 Tim. 3:11) Kwa kuongezea, akina dada vijana wanaweza kupata katika kutaniko lao wanawake Wakristo wakomavu ambao ni mfano mzuri wa kuigwa. Akina dada vijana, je, mnaweza kutafuta kutanikoni wanawake Wakristo wakomavu ambao mnaweza kuiga mfano wao? Chunguzeni sifa zao zinazovutia; kisha mfikirie jinsi mnavyoweza kuonyesha sifa hizo. Sifa muhimu ya kuwa Mkristo mkomavu ni unyenyekevu. Ikiwa mwanamke ni mnyenyekevu, atafurahia uhusiano mzuri na Yehova na watu wengine pia. Kwa mfano, mwanamke anayempenda Yehova, kwa unyenyekevu anachagua kuunga mkono kanuni ya ukichwa ambayo Baba yake wa mbinguni alianzisha. (1 Kor. 11:3) Kanuni hiyo inatumika kwa njia hususa katika kutaniko na katika familia pia. w23.12 18-19 ¶3-5

Jumatatu, Oktoba 27

Waume wanapaswa kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.—Efe. 5:28.

Yehova anatarajia mume ampende mke wake na kumtunza kimwili, kihisia, na kiroho. Kusitawisha uwezo wa kufikiri, kuwaheshimu wanawake, na kuwa mwenye kutegemeka, kutakusaidia ukiwa mwenzi wa ndoa. Baada ya kufunga ndoa, unaweza kuwa baba. Unaweza kujifunza nini kutoka kwa Yehova kuhusu kuwa baba mzuri? (Efe. 6:4) Yehova alimwambia waziwazi Mwana wake, Yesu, kwamba anampenda na kumkubali. (Mt. 3:17) Ikiwa utakuwa baba, hakikisha kuwa unawahakikishia kwa ukawaida watoto wako kwamba unawapenda. Wapongeze mara kwa mara kwa mambo mazuri wanayofanya. Akina baba wanaoiga mfano wa Yehova wanawasaidia watoto wao kuwa wanaume na wanawake Wakristo wakomavu. Unaweza kujitayarisha sasa kwa ajili ya jukumu hilo kwa kuwajali kwa upendo watu katika familia yenu na katika kutaniko na kwa kujifunza kuwaambia kwamba unawapenda na unawathamini.—Yoh. 15:9. w23.12 28-29 ¶17-18

Jumanne, Oktoba 28

[Yehova] ndiye tegemeo imara la nyakati zako.—Isa. 33:6.

Ingawa sisi ni watumishi waaminifu wa Yehova, tunakabili hali ngumu na magonjwa kama watu wengine. Huenda pia tukahitaji kuvumilia upinzani au mateso kutoka kwa watu wanaowachukia watu wa Mungu. Ingawa Yehova hatukingi tusipatwe na hali hizo ngumu, anaahidi kutusaidia. (Isa. 41:10) Kwa msaada wake, tunaweza kudumisha shangwe yetu, kufanya maamuzi mazuri, na kuendelea kuwa waaminifu licha ya kukabili hali ngumu. Yehova anaahidi kutupatia kile ambacho Biblia inakiita “amani ya Mungu.” (Flp. 4:​6, 7) Amani ya Mungu inarejelea utulivu na amani ya akilini na moyoni tunayopata kwa sababu ya kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Amani hiyo ‘inazidi uelewaji wote’; inastaajabisha sana kuliko tunavyoweza kuwazia. Kwa mfano, umewahi kuhisi umepata utulivu sana baada ya kusali kwa bidii kwa Yehova? Utulivu huo ni “amani ya Mungu.” w24.01 20 ¶2; 21 ¶4

Jumatano, Oktoba 29

Nafsi yangu na imsifu Yehova; kila kitu kilicho ndani yangu na kilisifu jina lake takatifu.—Zab. 103:1.

Kwa kuwa wanampenda Mungu, watu waaminifu wanachochewa kulisifu jina lake kwa moyo wote. Mfalme Daudi alielewa kwamba kulisifu jina la Yehova ni sawa na kumsifu Yehova mwenyewe. Jina la Yehova linahusisha sifa yake nzuri, hivyo linatukumbusha sifa zake zote maridadi na matendo yake yenye kustaajabisha. Daudi aliliona jina la Baba yake kuwa takatifu na alitamani kulisifu. Alitaka kufanya hivyo na “kila kitu kilicho ndani” yake—yaani, kwa moyo wote. Vivyo hivyo, Walawi waliongoza katika kumsifu Yehova. Kwa unyenyekevu, walikubali kwamba maneno yao hayangeweza kamwe kueleza kikamili sifa ambayo jina hilo takatifu linastahili. (Neh. 9:5) Hapana shaka kwamba sifa hizo za kutoka moyoni zilimletea shangwe Yehova. w24.02 9 ¶6

Alhamisi, Oktoba 30

Kwa kadiri ambavyo tumefanya maendeleo, na tuendelee kutembea kwa utaratibu katika mwendo huohuo.—Flp. 3:16.

Yehova hataona kwamba umeshindwa kwa kukosa kutimiza lengo ambalo linapita uwezo wako. (2 Kor. 8:12) Ona kipingamizi hicho kuwa fursa ya kujifunza. Kumbuka mambo ambayo tayari umetimiza. Biblia inasema hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi [yako].” (Ebr. 6:10) Basi wewe pia hupaswi kusahau. Fikiria kuhusu mambo ambayo tayari umetimiza—iwe ni kusitawisha urafiki pamoja na Yehova, kuwaambia wengine kumhusu, au kubatizwa. Kama vile ulivyofanya maendeleo na kutimiza malengo ya kiroho wakati uliopita, unaweza kuendelea kufanya maendeleo ili kutimiza lengo lako sasa. Kwa msaada wa Yehova, unaweza kutimiza lengo lako. Unapoendelea kufanyia kazi lengo lako la kiroho, usisahau kufurahia kuona jinsi Yehova anavyokusaidia na kukubariki unapojitahidi kutimiza lengo lako. (2 Kor. 4:7) Usipokufa moyo, utapata baraka kubwa hata zaidi.—Gal. 6:9. w23.05 31 ¶16-18

Ijumaa, Oktoba 31

Baba mwenyewe anawapenda ninyi, kwa sababu mmenipenda na mmeamini kwamba nilikuja nikiwa mwakilishi wa Mungu.—Yoh. 16:27.

Yehova anafurahi kuwaonyesha kibali chake wale anaowapenda. Maandiko yanataja pindi mbili ambapo Yehova alimwambia Yesu kwamba yeye ni Mwana wake mpendwa, anayemkubali. (Mt. 3:17; 17:5) Je, ungependa kumsikia Yehova akikuhakikishia kwamba una kibali chake? Yehova hazungumzi nasi moja kwa moja, lakini anazungumza nasi kupitia Neno lake. Tunaposoma katika vitabu vya Injili maneno yenye upendo ya Yesu aliyowaambia wanafunzi wake, ni kana kwamba tunamsikia Yehova akizungumza nasi. Yesu aliiga kikamilifu utu wa Baba yake. Hivyo, tunaposoma kwamba Yesu aliwaambia wafuasi wake waaminifu ambao si wakamilifu kwamba amewakubali, tunaweza kuwazia Yehova akituambia maneno hayohayo. (Yoh. 15:​9, 15) Majaribu yanapotokea, hayamaanishi kwamba tumepoteza kibali cha Mungu. Badala yake, yanatupatia fursa ya kuthibitisha kina cha upendo wetu kwa Mungu na kwamba tunamtumaini.—Yak. 1:12. w24.03 28 ¶10-11

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki