Novemba
Jumamosi, Novemba 1
Kutoka katika vinywa vya watoto wadogo na wanaonyonya, umetoa sifa.—Mt. 21:16.
Ikiwa wewe ni mzazi, wasaidie watoto wako watayarishe maelezo yanayolingana na umri wao. Nyakati nyingine, mambo mazito kama vile matatizo ya ndoa au masuala ya kiadili, huzungumziwa wakati wa funzo, lakini huenda kuna fungu moja au mawili ambayo mtoto anaweza kutoa maelezo. Pia, wasaidie watoto wako waelewe kwa nini huenda hawatachaguliwa kila mara wanapoinua mkono. Kufafanua jambo hilo kunaweza kuwasaidia wasivunjike moyo watu wengine wanapochaguliwa. (1 Tim. 6:18) Sisi sote tunaweza kutayarisha maelezo yenye kujenga ambayo yatamletea Yehova heshima na kuwatia moyo Wakristo wenzetu. (Met. 25:11) Ingawa wakati mwingine tunaweza kutoa maelezo mafupi ya mambo tuliyojionea, tunapaswa kuepuka kuzungumza sana kujihusu. (Met. 27:2; 2 Kor. 10:18) Badala yake, tunajitahidi kumkazia fikira Yehova, Neno lake, na watu wake kwa ujumla.—Ufu. 4:11. w23.04 24-25 ¶17-18
Jumapili, Novemba 2
Tusiendelee kulala usingizi kama wengine wanavyofanya, bali tukae macho na kutunza akili zetu.—1 The. 5:6.
Tunahitaji upendo ili tukae macho na kuendelea kutunza akili zetu. (Mt. 22:37-39) Kumpenda Mungu kunatusaidia kuendelea kuhubiri licha ya changamoto zozote ambazo huenda tukakabili. (2 Tim. 1:7, 8) Kwa kuwa tunawaonyesha upendo hata watu ambao hawamtumikii Yehova, tunaendelea kuhubiri, hata kutoa ushahidi kupitia simu na barua. Tunaendelea kutumaini kwamba siku moja jirani zetu watafanya mabadiliko na kuanza kutenda mambo yanayofaa. (Eze. 18:27, 28) Pia, tunawapenda ndugu na dada zetu. Tunaonyesha upendo huo kwa “kutiana moyo na kujengana.” (1 The. 5:11) Kama wanajeshi wanaotumikia vitani bega kwa bega, sisi pia tunatiana moyo. Hatuwezi kamwe kuwaumiza kimakusudi ndugu na dada zetu au kulipa ubaya kwa ubaya. (1 The. 5:13, 15) Pia, tunaonyesha upendo kwa kuwaheshimu ndugu wanaoongoza kutanikoni.—1 The. 5:12. w23.06 10 ¶6; 11 ¶10-11
Jumatatu, Novemba 3
[Yehova] akisema jambo, je, hatalitenda?—Hes. 23:19.
Njia moja tunayoweza kuimarisha imani yetu ni kwa kutafakari kuhusu fidia. Fidia inatuhakikishia kwamba ahadi za Mungu zitatimia. Tunapotafakari kwa makini kwa nini fidia ilitolewa na mambo yaliyohusika, tunaimarisha imani yetu kwamba ahadi ya Mungu kuhusu kuishi milele katika ulimwengu bora itatimizwa kwa uhakika. Kwa nini tunaweza kusema hivyo? Fidia ilihusisha nini? Yehova alimtuma Mwana wake mpendwa mzaliwa wa kwanza, mwandamani wake wa karibu zaidi, atoke mbinguni na kuzaliwa akiwa mwanadamu mkamilifu. Alipokuwa duniani, Yesu alivumilia hali ngumu mbalimbali. Kisha akateswa na kufa kifo chenye maumivu. Yehova alilipa bei kubwa sana! Mungu wetu mwenye upendo hangeruhusu kamwe Mwana wake ateseke na kufa ili tu kutuandalia maisha bora lakini ya muda mfupi. (Yoh. 3:16; 1 Pet. 1:18, 19) Kwa kuwa alilipa bei kubwa sana, Yehova atahakikisha kwamba tutaishi milele katika ulimwengu mpya. w23.04 27 ¶8-9
Jumanne, Novemba 4
Ewe Kifo, yako wapi maumivu yako makali?—Hos. 13:14.
Je, Yehova anatamani kuwafufua wafu? Bila shaka, anatamani kuwafufua. Aliwaongoza baadhi ya waandikaji wa Biblia kuandika kuhusu ahadi ya ufufuo wa wakati ujao. (Isa. 26:19; Ufu. 20:11-13) Na Yehova anapotoa ahadi sikuzote yeye huitimiza. (Yos. 23:14) Kwa kweli, Yehova anatamani kuwafufua waliokufa. Fikiria maneno ambayo Ayubu alisema. Alikuwa na uhakika kwamba hata akifa, Yehova angekuwa na hamu kubwa ya kumwona akiishi tena. (Ayu. 14:14, 15, maelezo ya chini) Bado Yehova anahisi hivyo kuelekea waabudu wake wote waliokufa. Anatamani kuwafufua, wakiwa na afya nzuri na furaha. Namna gani mabilioni ya watu ambao walikufa bila kupata nafasi ya kujifunza ukweli kumhusu Yehova? Mungu wetu mwenye upendo anataka kuwafufua pia. (Mdo. 24:15) Anataka wawe na nafasi ya kuwa rafiki zake na kuishi milele duniani.—Yoh. 3:16. w23.04 9 ¶5-6
Jumatano, Novemba 5
Kwa msaada wa Mungu tutapata nguvu.—Zab. 108:13.
Unawezaje kuimarisha tumaini lako? Kwa mfano, ikiwa una tumaini la kuishi milele duniani, soma ufafanuzi wa Biblia kuhusu Paradiso na utafakari kuhusu mambo hayo. (Isa. 25:8; 32:16-18) Fikiria jinsi maisha yatavyokuwa katika ulimwengu mpya. Jiwazie ukiwa huko. Ikiwa tutaendelea kufikiria kuhusu tumaini la ulimwengu mpya, matatizo yetu yatakuwa ya ‘muda mfupi na mepesi.’ (2 Kor. 4:17) Tumaini ambalo Yehova amekupatia linaweza kukutia nguvu. Tayari amekuandalia mambo unayohitaji ili upate nguvu kutoka kwake. Basi, unapohitaji msaada ili kutimiza mgawo fulani, kuvumilia jaribu, au kudumisha shangwe yako, sali kwa Yehova kwa bidii na utafute mwongozo wake kupitia funzo la kibinafsi. Waruhusu ndugu na dada zako Wakristo wakutie moyo. Dumisha tumaini lako likiwa jangavu na wazi akilini. Kisha utaimarishwa “kwa nguvu zote kwa uwezo [wa Mungu] wenye utukufu ili uvumilie kikamili kwa subira na shangwe.”—Kol. 1:11. w23.10 17 ¶19-20
Alhamisi, Novemba 6
Toeni shukrani kuhusu kila jambo.—1 The. 5:18.
Tuna sababu nyingi za kumshukuru Yehova katika sala. Tunaweza kumshukuru kwa ajili ya kitu chochote kizuri tulicho nacho; kwa sababu kila zawadi njema hutoka kwake. (Yak. 1:17) Kwa mfano, tunaweza kumshukuru kwa dunia yetu maridadi na vitu vyenye kustaajabisha alivyoumba. Pia, tunaweza kumshukuru kwa uhai wetu, familia yetu, rafiki zetu, na tumaini letu. Na tungependa kumshukuru Yehova kwa kuturuhusu tufurahie urafiki wenye thamani pamoja naye. Huenda tukahitaji kufanya jitihada za pekee ili kufikiria sababu ambazo zinatufanya sisi binafsi tumshukuru Yehova. Tunaishi katika ulimwengu usio na shukrani. Mara nyingi watu hukazia fikira vitu wanavyotaka, badala ya kukazia fikira mambo wanayoweza kufanya ili kuonyesha shukrani kwa ajili ya vitu walivyo navyo. Ikiwa tutaathiriwa na mtazamo huo, sala zetu zinaweza kuwa orodha ya mambo tunayotaka. Ili jambo hilo lisitokee, tunapaswa kuendelea kusitawisha na kuonyesha shukrani kwa ajili ya mambo yote ambayo Yehova anatufanyia.—Luka 6:45. w23.05 4 ¶8-9
Ijumaa, Novemba 7
[Endeleeni] kuomba kwa imani, bila kuwa na shaka hata kidogo.—Yak. 1:6.
Akiwa Baba yetu mwenye upendo, Yehova hapendi kuona tukiteseka. (Isa. 63:9) Hata hivyo, hazuii majaribu yetu yote, ambayo yanaweza kulinganishwa na mito au miali ya moto. (Isa. 43:2) Lakini anaahidi atatusaidia ‘tunapopita katika’ majaribu hayo. Na hataruhusu majaribu yetu yatusababishie madhara ya kudumu. Pia, Yehova anatupatia roho yake takatifu yenye nguvu ili itusaidie kuvumilia. (Luka 11:13; Flp. 4:13) Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote atatupatia mambo tunayohitaji ili tuvumilie na kuendelea kuwa waaminifu kwake. Yehova anatarajia tumtumaini. (Ebr. 11:6) Wakati mwingine, tunaweza kulemewa na majaribu yetu. Huenda hata tukawa na shaka ikiwa Yehova atatusaidia. Lakini Biblia inatuhakikishia kwamba kwa nguvu za Mungu tunaweza “kuupanda ukuta.” (Zab. 18:29) Hivyo, badala ya kuwa na shaka, tunapaswa kusali tukiwa na imani kamili, tukiamini kwamba Yehova atajibu sala zetu.—Yak. 1:6, 7. w23.11 22 ¶8-9
Jumamosi, Novemba 8
Miale [ya upendo] ni moto mkali, mwali wa Yah. Maji yenye nguvu hayawezi kuuzima upendo, wala mito haiwezi kuufagilia mbali.—Wim. 8:6, 7.
Huo ni ufafanuzi maridadi sana wa upendo wa kweli! Maneno hayo yanawahakikishia hivi wenzi wa ndoa: Mnaweza kuwa na upendo wa kweli kati yenu. Wenzi wa ndoa wanahitaji kujitahidi ili kuwa na upendo unaodumu. Kwa mfano, moto wa kuni unaweza kuendelea kuwaka daima—ikiwa tu utaendelea kuongezwa kuni. Bila kuongeza kuni, mwishowe moto huo utazima. Vivyo hivyo, upendo kati ya mume na mke unaweza kuendelea kuwa wenye nguvu daima—ikiwa tu wataimarisha uhusiano wao. Nyakati fulani, huenda wakahisi upendo kati yao unapoa, hasa ikiwa wanakabili matatizo ya kifedha, matatizo ya kiafya, au mkazo wa kulea watoto. Hivyo, ili “mwali wa Yah” uendelee kuwaka, mume na mke wanapaswa kuwa na uhusiano wenye nguvu pamoja na Yehova. w23.05 20-21 ¶1-3
Jumapili, Novemba 9
Usiogope.—Dan. 10:19.
Tunahitaji kufanya nini ili tusitawishe ujasiri? Huenda wazazi wetu wakatuhimiza tuwe jasiri, lakini hatuwezi kurithi sifa hiyo kutoka kwao kana kwamba ni mali ya familia yetu. Kupata ujasiri ni kama kujifunza ustadi mpya. Njia moja ya kuboresha ustadi huo ni kwa kutazama kwa makini matendo ya mwalimu, kisha kuiga mfano wake. Vivyo hivyo, tunajifunza kuwa jasiri kwa kutazama kwa makini jinsi wengine wanavyoonyesha sifa hiyo, kisha kuiga mfano wao. Kama Danieli, tunahitaji kulifahamu vizuri Neno la Mungu. Tunapaswa kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kwa kuzungumza naye kwa uhuru na mara nyingi. Na tunahitaji kumtumaini Yehova, na kusadiki kwamba sikuzote atatusaidia. Kisha imani yetu itakapojaribiwa, tutakuwa na ujasiri. Mara nyingi watu wanaoonyesha ujasiri huheshimiwa na wengine. Pia, huenda wakawasaidia watu wenye mioyo minyoofu wamjue Yehova. Bila shaka, tuna sababu nzuri za kusitawisha ujasiri. w23.08 2 ¶2; 4 ¶8-9
Jumatatu, Novemba 10
Hakikisheni mambo yote.—1 The. 5:21.
Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “hakikisheni” lilitumiwa kuhusiana na kupima uhalisi wa madini yenye thamani. Hivyo, tunahitaji kupima mambo tunayosikia au tunayosoma ili kuthibitisha ukweli wake. Jambo hilo litakuwa muhimu hata zaidi kwetu dhiki kuu inapokaribia. Badala ya kukubali kila jambo ambalo watu wanasema, tunatumia uwezo wetu wa kufikiri ili kulinganisha mambo tunayosoma au yale tunayosikia na mambo ambayo Biblia na tengenezo la Yehova linasema. Tukifanya hivyo, hatutadanganywa na propaganda yoyote ya roho waovu au njia nyingine ya ujanja. (Met. 14:15; 1 Tim. 4:1) Wakiwa kikundi, watumishi wa Mungu wataokoka dhiki kuu. Hata hivyo, tukiwa mtu mmoja-mmoja hatujui mambo tutakayokabili wakati ujao. (Yak. 4:14) Ingawa hivyo, iwe tutaokoka dhiki kuu tukiwa hai au tutakufa kabla ya wakati huo, Yehova atatuthawabisha kwa kutupa uzima wa milele ikiwa tutaendelea kuwa waaminifu. Acheni sisi sote tuendelee kukazia fikira tumaini letu zuri na kuendelea kuwa tayari kwa ajili ya siku ya Yehova! w23.06 13 ¶15-16
Jumanne, Novemba 11
[Amewafunulia] watumishi wake . . . siri yake.—Amo. 3:7.
Hatujui jinsi baadhi ya unabii wa Biblia utakavyotimizwa. (Dan. 12:8, 9) Lakini kwa kuwa hatujui kikamili jinsi unabii fulani utakavyotimizwa, hilo halimaanishi kwamba hautatimizwa. Bila shaka, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatufunulia mambo tunayohitaji kujua kwa wakati unaofaa, kama alivyofanya zamani. Tangazo la “amani na usalama” litatolewa. (1 The. 5:3) Kisha serikali za kisiasa za ulimwengu zitashambulia dini za uwongo na kuziangamiza. (Ufu. 17:16, 17) Kisha zitashambulia watu wa Mungu. (Eze. 38:18, 19) Matukio hayo yataongoza moja kwa moja kwenye vita vya mwisho vya Har–Magedoni. (Ufu. 16:14, 16) Tunaweza kuwa na hakika kwamba matukio hayo yatatokea hivi karibuni. Kabla wakati huo haujafika, acheni tuendelee kuonyesha uthamini wetu kwa Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo kwa kukazia uangalifu unabii wa Biblia na kuwasaidia wengine wafanye hivyo pia. w23.08 13 ¶19-20
Jumatano, Novemba 12
Na tuendelee kupendana, kwa sababu upendo unatoka kwa Mungu.—1 Yoh. 4:7.
Mtume Paulo alipokuwa akizungumzia imani, tumaini, na upendo, alimalizia kwa kusema kwamba ‘sifa kubwa zaidi kati ya hizo ni upendo.’ (1 Kor. 13:13) Kwa nini mtume Paulo alisema hivyo? Wakati ujao, hatutahitaji kuwa na imani katika ahadi za Mungu kuhusu ulimwengu wake mpya au kutumaini kwamba ahadi zake zitatimia kwa sababu tayari zitakuwa zimetimizwa. Lakini sikuzote tutahitaji kumpenda Yehova na kuwapenda watu. Kwa kweli, upendo wetu kwao utaendelea kukua milele. Pia, upendo unatutambulisha kuwa Wakristo wa kweli. Yesu aliwaambia hivi mitume wake: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.” (Yoh. 13:35) Isitoshe, tukiwa na upendo miongoni mwetu tutadumisha umoja. Paulo aliuita upendo “kifungo kikamilifu cha muungano.” (Kol. 3:14) Mtume Yohana aliwaandikia waabudu wenzake hivi: “Yeyote anayempenda Mungu lazima pia ampende ndugu yake.” (1 Yoh. 4:21) Tunapopendana, tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu. w23.11 8 ¶1, 3
Alhamisi, Novemba 13
Tuondoe kila uzito.—Ebr. 12:1.
Biblia inalinganisha maisha yetu tukiwa Wakristo na mbio. Wakimbiaji ambao wanafaulu kumaliza mbio hizi wanapewa zawadi ya uzima wa milele. (2 Tim. 4:7, 8) Tunahitaji kufanya kila jitihada ili tuendelee kukimbia, hasa kwa sababu tumekaribia sana kufika mwisho wa mbio hizo. Mtume Paulo, alitaja mambo ambayo yanaweza kutusaidia kushinda mbio hizo. Alituagiza “tuondoe kila uzito na . . . tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.” Je, Paulo alimaanisha kuwa hakuna majukumu ambayo Mkristo anapaswa kubeba? Hapana, hakumaanisha hivyo. Badala yake, alimaanisha kwamba tunapaswa kuondoa kila uzito usio wa lazima. Uzito huo usio wa lazima unaweza kufanya tupunguze mwendo na kusababisha tuchoke. Ili tuvumilie, tunapaswa kutambua haraka na kuondoa mzigo wowote usio wa lazima ambao unaweza kufanya tupunguze mwendo wetu. Hata hivyo, hatungependa kupuuza majukumu ambayo tunapaswa kubeba. Ikiwa tutayapuuza, hatutastahili kushiriki katika mbio za uzima.—2 Tim. 2:5. w23.08 26 ¶1-2
Ijumaa, Novemba 14
Kujipamba kwenu kusiwe kwa nje.—1 Pet. 3:3.
Usawaziko unatusaidia kuheshimu maoni ya wengine. Kwa mfano, kuna akina dada ambao wanapenda kujipamba usoni, na kuna wengine ambao hawapendi. Baadhi ya Wakristo hufurahia kunywa kileo kwa kiasi, lakini wengine huamua kwamba hawatakunywa. Wakristo wote wanatamani kuwa na afya nzuri, lakini wanachagua aina mbalimbali ya matibabu. Ikiwa tunafikiri kwamba sikuzote sisi tuko sahihi, huenda tukajaribu kuwashawishi wengine wafuate maoni yetu, jambo ambalo linaweza kuwakwaza wengine na kusababisha migawanyiko. (1 Kor. 8:9; 10:23, 24) Kwa mfano, badala ya kutupatia sheria kali kuhusu jinsi tunavyopaswa kuvaa, Yehova anatupatia kanuni. Tunapaswa kuvaa kwa njia ambayo inamfaa mtumishi wa Mungu, inayoonyesha usawaziko, kiasi, na “utimamu wa akili.” (1 Tim. 2:9, 10) Kwa hiyo, hatujielekezei fikira wenyewe kupitia jinsi tunavyovaa. Kanuni za Biblia pia zitawasaidia wazee wa kutaniko waepuke kuweka sheria zao wenyewe kuhusu mavazi na mitindo ya nywele. w23.07 23-24 ¶13-14
Jumamosi, Novemba 15
Nisikilizeni kwa makini, mle kilicho chema, nanyi mtafurahia sana vitu vyenye lishe kwelikweli.—Isa. 55:2.
Yehova anatuonyesha jinsi tunavyoweza kuwa na wakati ujao wenye furaha. Wale wanaokubali mwaliko unaotolewa kwa sauti kubwa na “mwanamke mpumbavu,” wanakazia fikira kujifurahisha kupitia ukosefu wa maadili kisiri. Matendo yao yatawaongoza katika “vina vya Kaburi.” (Met. 9:13, 17, 18) Matokeo ni tofauti kabisa kwa wale wanaokubali mwaliko wa “hekima ya kweli”! (Met. 9:1) Tunajifunza kupenda mambo ambayo Yehova anapenda na kuchukia mambo ambayo anachukia. (Zab. 97:10) Na tunafurahi kuwaalika wengine ili waje na kunufaika kutokana na “hekima ya kweli.” Ni kana kwamba tunaita “kwa sauti [hivi] kutoka vileleni juu ya jiji: ‘Yeyote ambaye ni mjinga na aje humu.’” Sisi na wale wanaokubali mwaliko huo hatunufaiki tu sasa. Tutaendelea kunufaika na kuishi milele ‘tunapotembea moja kwa moja katika njia ya uelewaji.’—Met. 9:3, 4, 6. w23.06 24 ¶17-18
Jumapili, Novemba 16
Mtu asiyekasirika upesi ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu, na mtu anayedhibiti hasira yake ni bora kuliko mtu anayelishinda jiji.—Met. 16:32.
Unahisije mfanyakazi mwenzako au mwanafunzi mwenzako anapokuuliza kuhusu imani yako? Je, unapatwa na wasiwasi? Wengi wetu huhisi hivyo. Lakini swali hilo linaweza kutusaidia kutambua mambo ambayo mtu huyo anafikiri au kuamini na kutupatia nafasi ya kuhubiri habari njema. Hata hivyo, nyakati nyingine mtu anaweza kuuliza swali kwa njia inayoweza kutokeza mabishano. Hilo halipaswi kutushangaza. Kwa sababu, baadhi ya watu wameambiwa habari za uwongo kuhusu mambo tunayoamini. (Mdo. 28:22) Isitoshe, tunaishi katika “siku za mwisho,” kipindi ambacho wengi ‘hawataki makubaliano yoyote’ na hata ni “wakali.” (2 Tim. 3:1, 3) Huenda ukajiuliza hivi, ‘Ninawezaje kujibu kwa neema na kwa njia isiyo ya ukali mtu anapopinga imani yangu inayotegemea Biblia?’ Ni nini kitakachokusaidia? Upole utakusaidia. Mtu mwenye sifa ya upole hakasiriki upesi na ana uwezo wa kujizuia anapochokozwa au ikiwa hajui jinsi ya kujibu. w23.09 14 ¶1-2
Jumatatu, Novemba 17
Utawaweka kuwa wakuu katika dunia yote.—Zab. 45:16.
Nyakati nyingine, tunapata ushauri unaotulinda kutokana na mambo kama vile kupenda mali na mambo mengine ambayo yanaweza kutufanya tuvunje sheria za Mungu. Katika hali hizo pia, tunanufaika tunapofuata mwongozo ambao Yehova huandaa. (Isa. 48:17, 18; 1 Tim. 6:9, 10) Bila shaka, Yehova ataendelea kutumia wawakilishi wake hapa duniani ili kutupatia mwongozo wakati wa dhiki kuu na tutakapokuwa kwenye ule Utawala wa Miaka Elfu Moja. Je, tutaendelea kufuata mwongozo huo? Itakuwa rahisi zaidi kufanya hivyo ikiwa tunafuata mwongozo ambao Yehova anatupatia sasa. Hivyo, acheni sikuzote tuendelee kufuata mwongozo wa Yehova, kutia ndani mwongozo ambao unatolewa na wanaume ambao wamewekwa rasmi ili kutulinda. (Isa. 32:1, 2; Ebr. 13:17) Na tunapofanya hivyo, tuna kila sababu ya kumtumaini Yule anayetuongoza, Yehova, ambaye atatuondoa mbali na hatari za kiroho na kutuongoza ili tufike mwisho wa safari yetu, yaani, kwenye uzima wa milele katika ulimwengu mpya. w24.02 25 ¶17-18
Jumanne, Novemba 18
Mmeokolewa kupitia fadhili zisizostahiliwa.—Efe. 2:5.
Mtume Paulo alikuwa na maisha yenye kuridhisha katika utumishi wa Yehova, lakini alikabiliana na changamoto nyingi. Mara kwa mara Paulo alisafiri kwa mwendo mrefu, na siku hizo haikuwa rahisi kusafiri. Katika safari zake, wakati mwingine Paulo alikabili “hatari za kutokana na mito” na “hatari za kutokana na wezi.” Pindi nyingine hata alipigwa na wapinzani wake. (2 Kor. 11:23-27) Na wakati mwingine Wakristo wenzake hawakuthamini jitihada za Paulo za unyoofu za kuwasaidia. (2 Kor. 10:10; Flp. 4:15) Ni nini kilichomsaidia Paulo aendelee kumtumikia Yehova? Paulo alijifunza mengi kuhusu utu wa Yehova kutokana na Maandiko na kupitia mambo yaliyompata. Paulo alisadiki kwamba Yehova Mungu anampenda. (Rom. 8:38, 39; Efe. 2:4, 5) Naye akampenda Yehova sana. Paulo alionyesha upendo wake kwa Yehova “kwa kuhudumu na kuendelea kuwahudumia watakatifu.”—Ebr. 6:10. w23.07 9 ¶5-6
Jumatano, Novemba 19
[Jitiishe] kwa mamlaka zilizo kubwa.—Rom. 13:1.
Watu wengi wanakubali kwamba tunahitaji serikali za wanadamu na kwamba tunapaswa kutii angalau baadhi ya sheria zilizowekwa na “mamlaka [hizo] zilizo kubwa.” Lakini huenda watu haohao wakasita kutii sheria fulani wanayoona kwamba si ya haki au wanayohisi inawabana sana. Neno la Mungu linasema kwamba serikali za wanadamu zinasababisha mateso, zinaongozwa na Shetani, na hivi karibuni zitaangamizwa. (Zab. 110:5, 6; Mhu. 8:9; Luka 4:5, 6) Pia, linasema kwamba “yeyote anayepinga mamlaka amechukua msimamo dhidi ya mpango wa Mungu.” Tunajitiisha kwa kadiri fulani chini ya mamlaka zilizo kubwa kwa sababu ni mpango wa Yehova wa muda mfupi wa kudumisha utaratibu. Kwa hiyo, tunapaswa ‘kuwapa wote haki zao,’ kutia ndani kulipa kodi, kuwapa heshima, na kuwa watiifu. (Rom. 13:1-7) Huenda tukaona sheria fulani kuwa yenye kubana, isiyo ya haki, au inatugharimu sana. Lakini tunamtii Yehova ambaye anatuambia tuzitii mamlaka hizo mradi tu hazituamuru kuvunja amri zake.—Mdo. 5:29. w23.10 8 ¶9-10
Alhamisi, Novemba 20
Roho ya Yehova ikamtia nguvu.—Amu. 15:14.
Samsoni alipozaliwa, Wafilisti walikuwa wakitawala taifa la Israeli na kuwanyanyasa. (Amu. 13:1) Utawala wao wa kikatili uliwasababishia Waisraeli mateso mengi. Yehova alimchagua Samsoni “[kuwaokoa] Waisraeli kutoka mikononi mwa Wafilisti.” (Amu. 13:5) Ili kutimiza jukumu hilo gumu, Samsoni alihitaji kumtegemea Yehova. Pindi moja, wanajeshi Wafilisti walikuja kumkamata Samsoni huko Lehi, inawezekana kwamba ni huko Yuda. Wanaume wa Yuda waliogopa, basi wakaamua kumkabidhi Samsoni kwa maadui wao. Waisraeli wenzake, walimfunga Samsoni kwa kamba mbili mpya na kumpeleka kwa Wafilisti. (Amu. 15:9-13) Hata hivyo, ‘roho ya Yehova ilimtia nguvu’ Samsoni na akajifungua kutoka katika zile kamba. Kisha “akaona utaya mbichi wa punda dume,” akauchukua, na kuutumia kuwaua wanaume 1,000 Wafilisti!—Amu. 15:14-16. w23.09 2 ¶3-4
Ijumaa, Novemba 21
Hii ni kulingana na kusudi la milele alilofanyiza kuhusiana na Kristo, Yesu Bwana wetu.—Efe. 3:11.
Yehova amefunua hatua kwa hatua ‘kusudi lake la milele’ katika Biblia. Kwa njia moja au nyingine, sikuzote anafanikiwa kwa sababu “amefanya kila kitu kitimize kusudi lake.” (Met. 16:4) Na matokeo ya mambo ambayo Yehova anatimiza yatadumu milele. Kusudi la Yehova ni nini, na amefanya mabadiliko gani ili kulitimiza? Mungu aliwaambia wanadamu wa kwanza kusudi lake kwa ajili yao. Aliwaambia, “Zaeni, muwe wengi, muijaze dunia na kuitiisha, na mtawale . . . kila kiumbe aliye hai” duniani. (Mwa. 1:28) Adamu na Hawa walipoasi na kufanya dhambi iingie katika familia ya wanadamu, hilo halikumzuia Yehova kutimiza kusudi lake. Alifanya mabadiliko katika njia ambayo kusudi lake lingetimizwa. Mara moja, aliamua kwamba atasimamisha Ufalme mbinguni ambao ungetimiza kusudi lake la mwanzoni kwa ajili ya wanadamu na dunia.—Mt. 25:34. w23.10 20 ¶6-7
Jumamosi, Novemba 22
Ikiwa Yehova hangekuwa msaidizi wangu, ningekuwa nimeangamia upesi.—Zab. 94:17.
Yehova anaweza kutusaidia kuendelea kuwa waaminifu. Huenda isiwe rahisi sikuzote hasa ikiwa tunapambana na udhaifu unaoendelea kwa muda mrefu. Nyakati nyingine, huenda udhaifu wetu ukaonekana kuwa mkubwa zaidi kuliko ule ambao mtume Petro alikabili. Lakini Yehova anaweza kutupatia nguvu ili tusife moyo. (Zab. 94:18, 19) Kwa mfano, ndugu fulani alijihusisha na ngono za watu wa jinsia moja kwa miaka mingi kabla ya kujifunza kweli. Aliamua kuacha maisha hayo yaliyopotoka kimaadili. Hata hivyo, wakati mwingine alipambana na tamaa zisizofaa. Ni nini kilichomsaidia kuendelea kuwa mwaminifu? Anaeleza hivi: “Yehova ndiye anayetuimarisha.” Anaongezea hivi: “Kwa msaada wa roho ya Yehova . . . , nimejifunza kwamba ninaweza [kuendelea] kutembea kwenye njia ya kweli . . . Yehova ameendelea kunitumia na licha ya udhaifu wangu mbalimbali anaendelea kuniimarisha.” w23.09 23 ¶12
Jumapili, Novemba 23
Unyenyekevu na kumwogopa Yehova huleta utajiri na utukufu na uzima.—Met. 22:4.
Ndugu vijana, hamwezi kuwa wanaume Wakristo wakomavu bila jitihada zozote. Mnahitaji kuchagua mifano mizuri ya kuiga, kusitawisha uwezo wa kufikiri, kutegemeka, kujifunza stadi zitakazowasaidia maishani, na kujitayarisha kwa ajili ya majukumu ya wakati ujao. Wakati mwingine huenda ukahisi umelemewa unapotafakari mambo unayohitaji kufanyia kazi. Lakini unaweza kufanikiwa. Kumbuka kwamba Yehova anatamani kukusaidia. (Isa. 41:10, 13) Bila shaka, akina ndugu na dada kutanikoni watakusaidia pia. Utakapofikia hatua ya kuwa mwanamume Mkristo mkomavu, maisha yako yatakuwa yenye kufurahisha na yenye kuridhisha. Tunawapenda, enyi ndugu vijana! Yehova na awabariki mnapojitahidi kuwa wanaume Wakristo wakomavu. w23.12 29 ¶19-20
Jumatatu, Novemba 24
[Achilia] kosa.—Met. 19:11.
Wazia uko kwenye tafrija pamoja na ndugu na dada wengine. Mnafurahia kuwa pamoja, na mnapiga picha. Kisha mnapiga picha mbili zaidi ili ikiwa picha ya kwanza haijatokea vizuri mweze kuchagua nyingine. Sasa una picha tatu. Lakini kwenye picha moja unaona ndugu amenuna. Hivyo, unafuta picha hiyo kwa sababu katika zile picha mbili nyingine, kila mmoja ametabasamu, kutia ndani ndugu huyo. Kwa kawaida, sisi huwa na kumbukumbu nzuri za pindi tulizofurahia pamoja na ndugu na dada zetu. Lakini huenda katika pindi hizo, ndugu au dada yetu anaweza kusema au kutenda jambo fulani lisilo la fadhili. Tunapaswa kufanya nini? Tunapaswa kufuta kumbukumbu hiyo mbaya, kama tunavyofuta picha isiyofaa. (Efe. 4:32) Tunaweza kufuta kumbukumbu hiyo, kwa sababu tuna kumbukumbu nyingi nzuri za pindi ambazo tulifurahia pamoja naye. Hizo ndizo kumbukumbu tunazotaka kutunza na kuzithamini. w23.11 12-13 ¶16-17
Jumanne, Novemba 25
Wanawake wanapaswa kujipamba kwa mavazi yanayofaa, . . . kwa njia inayowafaa wanawake wanaokiri kwamba wanamtumikia Mungu.—1 Tim. 2:9, 10.
Maneno ya Kigiriki yaliyotumiwa hapa yanadokeza kwamba mavazi ya mwanamke Mkristo yangepaswa kuwa ya heshima na yangeonyesha kwamba anajali hisia au maoni ya wengine. Tunajivunia dada zetu Wakristo wakomavu ambao wanavalia kwa kiasi! Utambuzi ni sifa nyingine ambayo akina dada wote Wakristo wakomavu huonyesha. Utambuzi ni nini? Ni uwezo wa kufanya maamuzi mazuri, yaani, uwezo wa kutofautisha lililo sawa na lisilo sawa na kisha kutenda kwa hekima. Fikiria mfano wa Abigaili. Mume wake alifanya uamuzi mbaya ambao ungekuwa na matokeo mabaya kwa watu wote wa nyumba yake. Abigaili alichukua hatua haraka. Uamuzi wake mzuri uliokoa uhai. (1 Sam. 25:14-23, 32-35) Pia, sifa ya utambuzi inatusaidia kujua wakati wa kuzungumza na wakati wa kukaa kimya. Na inatusaidia kupendezwa kibinafsi na wengine kwa njia isiyopita kiasi.—1 The. 4:11. w23.12 20 ¶8-9
Jumatano, Novemba 26
Tushangilie, kwa kutegemea tumaini la utukufu wa Mungu.—Rom. 5:2.
Mtume Paulo aliliandikia kutaniko la Roma maneno hayo. Ndugu na dada kwenye kutaniko hilo walikuwa wamejifunza kumhusu Yehova na Yesu, walikuwa wamesitawisha imani, na kuwa Wakristo. Hivyo, Mungu “[aliwatangaza] kuwa waadilifu kutokana na imani,” na kuwatia mafuta kwa roho takatifu. (Rom. 5:1) Naam, walipata tumaini lenye uhakika na zuri ajabu. Baadaye, Paulo aliwaandikia Wakristo watiwa-mafuta jijini Efeso kuhusu tumaini ambalo Mungu alikuwa amewapatia. Tumaini hilo linatia ndani kupokea ‘urithi wa watakatifu.’ (Efe. 1:18) Pia, Paulo aliwaeleza Wakolosai mahali ambapo tumaini lao lingetimizwa. Aliliita “tumaini [walilowekewa] akiba mbinguni.” (Kol. 1:4, 5) Hivyo, tumaini la Wakristo watiwa-mafuta ni kwamba watafufuliwa ili wapate uzima wa milele mbinguni, ambapo watatawala pamoja na Kristo.—1 The. 4:13-17; Ufu. 20:6. w23.12 9 ¶4-5
Alhamisi, Novemba 27
Amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.—Flp. 4:7.
Neno la awali lililotafsiriwa “linda” lilitumiwa jeshini na lilikuwa likirejelea kikosi cha wanajeshi kilichopewa kazi ya kulinda jiji ili lisishambuliwe. Wakaaji wa jiji lililolindwa walilala bila wasiwasi, wakijua kwamba wanajeshi walikuwa wakilinda malango ya jiji. Katika maana hiyohiyo, amani ya Mungu inapoilinda mioyo na akili zetu, tunahisi utulivu tukijua kwamba tuko salama. (Zab. 4:8) Kama ilivyokuwa kwa Hana, hata kama hali yetu haibadiliki papo hapo, bado tunaweza kuwa na kiasi fulani cha amani. (1 Sam. 1:16-18) Na tunapokuwa na utulivu, mara nyingi inakuwa rahisi zaidi kufikiri kwa njia nzuri na kufanya maamuzi ya hekima. Tunaweza kufanya nini? Kama wakaaji wa jiji walivyowaomba walinzi wawalinde, tunaweza kumwomba Yehova atulinde tunapopata matatizo. Jinsi gani? Sali hadi uhisi umepata amani ya Mungu. (Luka 11:9; 1 The. 5:17) Ikiwa unakabili hali ngumu, dumu katika sala, nawe utajionea amani ya Mungu ikilinda akili na moyo wako.—Rom. 12:12. w24.01 21 ¶5-6
Ijumaa, Novemba 28
Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.—Mt. 6:9.
Ili kulitakasa jina la Baba yake, Yesu alivumilia mateso, matukano, na uchongezi wa kila aina. Alijua kwamba alikuwa amemtii Baba yake katika mambo yote; hakuwa na sababu yoyote ya kuaibika. (Ebr. 12:2) Pia, alijua kwamba Shetani alikuwa akimshambulia moja kwa moja katika kipindi hicho kigumu. (Luka 22:2-4; 23:33, 34) Bila shaka Shetani alitamani sana kuvunja utimilifu wa Yesu; hata hivyo, Shetani alishindwa kabisa! Yesu alithibitisha kabisa kwamba Shetani ni mwongo mbaya sana na kwamba Yehova ana watumishi washikamanifu, ambao wanadumisha utimilifu wao hata chini ya majaribu makali zaidi! Je, unataka kumfurahisha Mfalme wako anayetawala? Endelea kulisifu jina la Yehova, na kuwasaidia wengine waujue vizuri kabisa utu wa Mungu. Kwa kufanya hivyo, utakuwa unafuata hatua za Yesu. (1 Pet. 2:21) Kama Yesu, utamfanya Yehova ashangilie na kuthibitisha kwamba adui Yake, Shetani, ni mwongo mwovu sana! w24.02 11-12 ¶11-13
Jumamosi, Novemba 29
Nitamlipa Yehova nini kwa mema yote aliyonitendea?—Zab. 116:12.
Katika miaka mitano iliyopita, watu zaidi ya milioni moja wamebatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova. Unapojiweka wakfu kwa Yehova unachagua kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo na jambo kuu zaidi maishani mwako linakuwa kufanya mapenzi ya Mungu. Wakfu wa Kikristo unahusisha nini? Yesu alisema: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe.” (Mt. 16:24) Msemo wa Kigiriki unaotafsiriwa “lazima ajikane mwenyewe” unaweza pia kurejelewa kuwa “kutoishi tena kwa ajili yetu wenyewe.” Ukiwa mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu, utahitaji kukataa kitu chochote kisichopatana na mapenzi yake. (2 Kor. 5:14, 15) Hilo linatia ndani kukataa “matendo ya mwili,” kama vile uasherati. (Gal. 5:19-21; 1 Kor. 6:18) Je, kutii maagizo hayo kunafanya maisha yako yawe magumu? Hapana, hutahisi hivyo ikiwa unampenda Yehova na unasadiki kwamba sheria zake ni kwa ajili ya manufaa yako.—Zab. 119:97; Isa. 48:17, 18. w24.03 2 ¶1; 3 ¶4
Jumapili, Novemba 30
Nimekukubali.—Luka 3:22.
Yehova huwapatia wale walio na kibali chake roho yake takatifu. (Mt. 12:18) Tunaweza kujiuliza hivi, ‘Je, nimefaulu kuonyesha sifa fulani ya tunda la roho ya Mungu maishani mwangu?’ Je, umetambua kwamba wewe ni mwenye subira zaidi unaposhughulika na wengine kuliko ulivyokuwa kabla hujamjua Yehova? Ukweli ni kwamba kadiri unavyojifunza kuonyesha zaidi sifa za tunda la roho ya Mungu, ndivyo utakavyokuwa na uhakika zaidi kwamba una kibali cha Yehova! Yehova anatumia thamani ya dhabihu ya fidia kwa wale walio na kibali chake. (1 Tim. 2:5, 6) Lakini namna gani ikiwa mioyo yetu haikubali kwamba tuna kibali cha Yehova, hata ingawa tuna imani katika fidia na tumebatizwa? Kumbuka kwamba hatuwezi kutumaini hisia zetu sikuzote, lakini tunaweza kumtumaini Yehova. Anawaona wale walio na imani katika fidia kuwa waadilifu machoni pake na anaahidi kuwabariki.—Zab. 5:12; Rom. 3:26. w24.03 30 ¶15; 31 ¶17