Desemba
Jumatatu, Desemba 1
Wafu watafufuliwa.—Luka 20:37.
Je, Yehova ana nguvu za kuwafufua waliokufa? Bila shaka! Yeye ni “Mweza-Yote.” (Ufu. 1:8) Basi ana nguvu za kutosha kumshinda adui yeyote, kutia ndani kifo. (1 Kor. 15:26) Sababu nyingine inayotusaidia kujua kwamba Yehova ana uwezo wa kuwafufua waliokufa ni kwamba kumbukumbu yake haina mipaka. Anaita kila nyota kwa jina. (Isa. 40:26) Pia, anawakumbuka wale waliokufa. (Ayu. 14:13; Luka 20:38) Anaweza kukumbuka habari zote kuhusu wale atakaowafufua, kutia ndani mwonekano wao, utu wao, mambo waliyojionea maishani, na kumbukumbu zao. Ni wazi kwamba tunaweza kuamini ahadi ya Yehova kuhusu ufufuo wa wakati ujao kwa sababu tunajua anatamani na ana nguvu za kuitimiza. Fikiria sababu nyingine ya kuamini ahadi ya Mungu ya ufufuo: Tayari Yehova amefanya hivyo. Katika nyakati za Biblia, aliwawezesha wanaume wachache waaminifu, kutia ndani Yesu, wawafufue wafu. w23.04 9-10 ¶7-9
Jumanne, Desemba 2
Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yaliyokolezwa chumvi.—Kol. 4:6.
Ikiwa tutajieleza kwa busara na upole, huenda watu wakawa tayari zaidi kutusikiliza na kuendeleza mazungumzo. Bila shaka, ikiwa mtu fulani anataka kushinda mabishano au kudhihaki imani yetu, hatuhitaji kuendelea na mazungumzo hayo. (Met. 26:4) Lakini huenda watu wengi hawana mtazamo huo na watakuwa tayari kutusikiliza. Ni wazi kwamba tutanufaika sana tukijiwekea lengo la kuwa wapole. Mwombe Yehova akupe nguvu ili uendelee kuwa mpole unapojibu maswali ambayo yanaweza kusababisha mabishano au unapokosolewa kwa sababu zisizo za kweli. Kumbuka kwamba mtazamo wa upole unaweza kuzuia mazungumzo yenu yasiwe mabishano. Na unapojibu kwa upole na heshima, huenda ukawachochea baadhi ya wasikilizaji wabadili maoni yao kutuhusu na kuhusu kweli za Biblia. Sikuzote ‘uwe tayari kutetea’ imani yako ‘ukifanya hivyo kwa upole na heshima kubwa.’ (1 Pet. 3:15) Naam, kwa kweli sifa ya upole ina nguvu! w23.09 19 ¶18-19
Jumatano, Desemba 3
Jivikeni . . . subira.—Kol. 3:12.
Fikiria njia nne ambazo tunaweza kuonyesha subira. Kwanza, mtu mwenye subira si mwepesi wa hasira. Anajitahidi kuwa mtulivu na anajizuia asikasirike wengine wanapomuudhi au anapokuwa chini ya mkazo. (Kut. 34:6) Pili, mtu mwenye subira anaweza kungoja kwa utulivu. Anapolazimika kungoja jambo fulani kwa muda mrefu zaidi kuliko alivyotarajia, mtu mwenye subira anajitahidi kuwa mtulivu na hakasiriki. (Mt. 18:26, 27) Tatu, mtu mwenye subira hatendi haraka-haraka bila kufikiri. Mtu mwenye subira anapohitaji kufanya jambo muhimu, haanzi kulifanya papo hapo, wala halifanyi haraka-haraka. Badala yake, anatenga muda wa kutosha ili kujitayarisha vizuri. Kisha anafanya jambo hilo kwa muda unaohitajika. Nne, mtu mwenye subira anajitahidi kukabiliana na majaribu bila kulalamika. Anajitahidi kabisa kuendelea kuvumilia huku akidumisha mtazamo unaofaa. (Kol. 1:11) Tukiwa Wakristo, tunahitaji kuonyesha subira kwa njia hizo zote. w23.08 20-21 ¶3-6
Alhamisi, Desemba 4
Yehova ndiye mchunguzaji wa mioyo.—Met. 17:3.
Sababu muhimu inayotufanya tuulinde moyo wetu wa mfano ni kwamba Yehova huchunguza moyo wetu. Hilo linamaanisha kwamba haangalii tu jinsi tunavyoonekana kwa wengine, badala yake anachunguza utu wetu wa ndani. Atatupenda ikiwa tutajaza katika akili zetu hekima yake ambayo inatusaidia kuishi milele. (Yoh. 4:14) Tukifanya hivyo, hatutapatwa na madhara yanayosababishwa na upotovu wa maadili na uwongo unaotoka kwa Shetani na ulimwengu wake. (1 Yoh. 5:18, 19) Kadiri tunavyozidi kumkaribia Yehova, ndivyo tutakavyozidi kumpenda na kumheshimu hata zaidi. Kwa kuwa hatutaki kumhuzunisha Baba yetu, tutaepuka hata kuwazia kutenda dhambi. Marta, dada anayeishi nchini Kroatia, ambaye alishawishiwa kujihusisha na ukosefu wa maadili, aliandika hivi: “Ilikuwa vigumu kwangu kufikiria kwa njia nzuri na kushinda tamaa ya kufurahia dhambi kwa muda mfupi. Lakini kumwogopa Mungu kulinilinda.” Kumwogopa Mungu kulimlindaje? Marta anasema kwamba alitafakari kuhusu matokeo ambayo uamuzi wake mbaya ungemletea. Sisi pia tunaweza kufanya hivyo. w23.06 20-21 ¶3-4
Ijumaa, Desemba 5
“Mataifa yatalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova,” asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, “nitakapotakaswa miongoni mwenu mbele ya macho yao.”—Eze. 36:23.
Yesu alijua kwamba kusudi la Yehova ni kulitakasa jina Lake, na kuliondolea shutuma zote. Hiyo ndiyo sababu Bwana wetu aliwafundisha wafuasi wake wasali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” (Mt. 6:9) Yesu alielewa kwamba hilo ndilo suala kuu zaidi linalokabili uumbaji wote. Hakuna kiumbe yeyote mbinguni au duniani ambaye amefanya mengi zaidi ya Yesu ili kulitakasa jina la Yehova. Hata hivyo, Yesu alipokamatwa, maadui wake walimshtaki kwa kosa gani? Kukufuru! Bila shaka, Yesu aliona kuwa kulitumia vibaya au kulichongea jina takatifu la Baba yake kuwa dhambi mbaya sana. Alihangaishwa sana kujua kwamba angeshtakiwa na kuhukumiwa kwa kosa hilo. Huenda hiyo ndiyo ilikuwa sababu kuu kwa nini Yesu “alikuwa na maumivu makali” saa chache kabla ya kukamatwa.—Luka 22:41-44. w24.02 11 ¶11
Jumamosi, Desemba 6
Nyumba hujengwa kwa hekima.—Met. 24:3.
Katika mbio zetu za uzima, tunapaswa kumpenda Yehova na Yesu kuliko tunavyowapenda watu wetu wa ukoo. (Mt. 10:37) Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba tunaweza kupuuza majukumu yetu katika familia kana kwamba yanatuzuia kufanya mambo yanayomfurahisha Mungu na Kristo. Kinyume chake, ili tumfurahishe Mungu na Kristo, tunahitaji kutimiza daraka letu katika familia. (1 Tim. 5:4, 8) Tunapofanya hivyo, tunakuwa wenye furaha zaidi. Kwa kweli, Yehova alikusudia familia ziwe na furaha mume na mke wanapotendeana kwa upendo na heshima, wazazi wanapowapenda na kuwazoeza watoto wao, na watoto wanapowatii wazazi wao. (Efe. 5:33; 6:1, 4) Hata uwe na jukumu gani katika familia, tegemea hekima inayopatikana katika Biblia badala ya kuongozwa tu na hisia zako, utamaduni, au mambo ambayo yanasemwa na wale wanaoitwa wataalamu. Tumia vizuri machapisho yanayotegemea Biblia. Machapisho hayo yana mapendekezo yanayofaa ya jinsi ya kutumia kanuni za Biblia. w23.08 28 ¶6-7
Jumapili, Desemba 7
Ukisome kwa sauti ya chini mchana na usiku ili ufuate kwa uangalifu mambo yote yaliyoandikwa humo; ndipo utakapofanikisha njia yako na kutenda kwa hekima.—Yos. 1:8.
Mwanamke Mkristo anahitaji kuwa na ustadi utakaomsaidia. Baadhi ya stadi ambazo msichana anajifunza akiwa mtoto, zitaendelea kumnufaisha katika maisha yake yote. Kwa mfano, jifunze kusoma na kuandika vizuri. Katika baadhi ya tamaduni, watu wanaona kwamba si muhimu kwa wanawake kujifunza kusoma na kuandika. Hata hivyo, huo ni ustadi muhimu sana kwa kila Mkristo. (1 Tim. 4:13) Hivyo, usiruhusu jambo lolote likuzuie kujifunza kusoma na kuandika vizuri. Utanufaikaje? Ustadi huo unaweza kukusaidia kupata kazi na kuidumisha. Utakusaidia kuwa mwanafunzi na mwalimu mzuri wa Neno la Mungu. Faida muhimu zaidi ni kwamba ustadi huo utakusaidia kumkaribia Yehova unaposoma Neno lake na kulitafakari.—1 Tim. 4:15. w23.12 20 ¶10-11
Jumatatu, Desemba 8
Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa kutoka kwenye jaribu watu wenye ujitoaji-kimungu.—2 Pet. 2:9.
Mwombe Yehova akusaidie kupinga majaribu. Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, sikuzote tunapambana dhidi ya majaribu ya kufanya mambo mabaya. Shetani anafanya yote anayoweza ili kufanya pambano hilo liwe ngumu hata zaidi. Njia moja anayojaribu kupotosha fikira zetu ni kupitia burudani zenye upotovu wa maadili. Burudani kama hizo hujaza akili yetu mawazo machafu—mawazo yanayomchafua yule mtu tuliye kwa ndani na yanayoweza kutuongoza kwenye dhambi nzito. (Marko 7:21-23; Yak. 1:14, 15) Tunahitaji msaada wa Yehova ili tushinde majaribu ya kufanya mambo mabaya. Yesu alitia ndani ombi hili katika sala ya kielelezo: “Usituingize katika majaribu, bali utukomboe kutoka kwa yule mwovu.” (Mt. 6:13) Yehova anataka kutusaidia, lakini ni lazima tumwombe msaada. Pia, lazima tutende kulingana na sala zetu. w23.05 6-7 ¶15-17
Jumanne, Desemba 9
Kamba ya nyuzi tatu haikatiki upesi.—Mhu. 4:12.
Ikiwa wenzi wa ndoa wanathamini urafiki wao pamoja na Baba yao wa mbinguni, wanakuwa tayari kufuata ushauri wake, na hilo linawasaidia kuepuka na kushinda matatizo ambayo yanaweza kufanya upendo kati yao upoe. Watu wanaopenda mambo ya kiroho pia hujitahidi kumwiga Yehova na kusitawisha sifa ambazo anaonyesha, kama vile fadhili, subira, na kusamehe. (Efe. 4:32–5:1) Wenzi wa ndoa wanaoonyesha sifa kama hizo hufanya iwe rahisi kwa upendo wao kusitawi. Dada anayeitwa Lena, ambaye amefunga ndoa kwa zaidi ya miaka 25, anasema hivi: “Ni rahisi kumpenda na kumheshimu mtu anayependa mambo ya kiroho.” Fikiria mfano ufuatao ulio katika Biblia. Wakati Yehova alipokuwa akiwachagua wenzi wa ndoa ambao wangekuwa wazazi wa Masihi wa wakati ujao, aliwachagua Yosefu na Maria kati ya wazao wengi wa Daudi. Kwa nini? Wote wawili walikuwa na urafiki wa kibinafsi pamoja na Yehova, na Yehova alijua kwamba wangemtanguliza katika ndoa yao. w23.05 21 ¶3-4
Jumatano, Desemba 10
Watiini wale wanaoongoza kati yenu.—Ebr. 13:17.
Ingawa Kiongozi wetu Yesu ni mkamilifu, wale ambao anawatumia kuongoza hapa duniani si wakamilifu. Huenda ikawa vigumu kuwatii, hasa wanapotuambia tufanye jambo ambalo hatutaki kulifanya. Pindi fulani mtume Petro alisitasita kutii mwongozo aliopewa. Malaika alipomwagiza ale wanyama ambao walionwa kuwa wasio safi kulingana na Sheria ya Musa, Petro alikataa—si mara moja, bali mara tatu! (Mdo. 10:9-16) Kwa nini? Kwa maoni yake, mwongozo huo mpya haukupatana na akili. Kwa upande mwingine, mtume Paulo aliwatii wazee Wakristo huko Yerusalemu walipomwagiza aende pamoja na wanaume wanne hekaluni na kujitakasa kisherehe ili kuonyesha kwamba alikuwa akitii Sheria. Paulo alijua kwamba Wakristo hawakuwa tena chini ya Sheria ya Musa. Naye hakuwa amefanya kosa lolote. Ingawa hivyo, Paulo “akaenda pamoja na wanaume hao siku iliyofuata, akajitakasa kisherehe pamoja nao.” (Mdo. 21:23, 24, 26) Utii wa Paulo ulichangia umoja.—Rom. 14:19, 21. w23.10 10 ¶15-16
Alhamisi, Desemba 11
Urafiki wa karibu pamoja na Yehova ni wa wale wanaomwogopa.—Zab. 25:14.
Huenda usifikiri kwamba woga ni sifa muhimu ili kuwa na urafiki mzuri. Hata hivyo, wale wanaotaka kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Yehova ni lazima ‘wamwogope.’ Hata iwe tumemtumikia Yehova kwa muda mrefu kadiri gani, sisi sote tunahitaji kusitawisha woga unaofaa kumwelekea. Lakini kumwogopa Mungu kunamaanisha nini? Mtu aliye na woga unaofaa kumwelekea Mungu anampenda na anaepuka kufanya jambo lolote ambalo linaweza kuharibu uhusiano wake pamoja na Mungu. Yesu ‘alimwogopa Mungu’ kwa njia hiyo. (Ebr. 5:7) Hakumwona Yehova kuwa mwenye kutisha. (Isa. 11:2, 3) Badala yake, alikuwa na upendo mwingi sana kumwelekea na alitaka kumtii. (Yoh. 14:21, 31) Kama Yesu, tunamheshimu na kumstahi sana Yehova kwa sababu Yeye ni mwenye upendo, hekima, haki, na nguvu. Pia, tunajua kwamba Yehova anatupenda na anapendezwa kuona jinsi tunavyoitikia mwongozo wake. Yehova anahuzunika tunapokosa kutii, lakini tunapomtii moyo wake unashangilia.—Zab. 78:41; Met. 27:11. w23.06 14 ¶1-2; 15 ¶5
Ijumaa, Desemba 12
Mara tu alipokuwa na nguvu, moyo wake ukawa na kiburi ambacho kilisababisha aangamie, naye alikosa kutenda kwa uaminifu kumwelekea Yehova.—2 Nya. 26:16.
Mfalme Uzia alipokuwa na nguvu, alisahau kwamba Yehova ndiye aliyekuwa Chanzo cha nguvu zake na ufanisi wake. Tunajifunza somo gani? Tunapaswa kukumbuka kwamba baraka na mapendeleo yetu yanatoka kwa Yehova. Badala ya kujigamba kuhusu mambo ambayo tunatimiza, tunapaswa kumshukuru Yehova kwa mambo ambayo tunafanya. (1 Kor. 4:7) Tunapaswa kutambua kwa unyenyekevu kwamba sisi sio wakamilifu na tunahitaji nidhamu. Ndugu fulani mwenye umri wa miaka 60 hivi, aliandika hivi: “Nimejifunza kutokasirika au kuvunjika moyo wengine wanapotambua makosa yangu. Ninapopokea nidhamu kwa sababu ya makosa ya kipumbavu ambayo wakati mwingine ninafanya, mimi hujitahidi kufanya marekebisho na kuendelea kumtumikia Yehova.” Ukweli ni kwamba ikiwa tutamwogopa Yehova na kuendelea kuwa wanyenyekevu, tutakuwa na maisha yenye kufurahisha sana.—Met. 22:4. w23.09 10 ¶10-11
Jumamosi, Desemba 13
Mnahitaji uvumilivu, ili baada ya kufanya mapenzi ya Mungu, mpokee utimizo wa ile ahadi.—Ebr. 10:36.
Wakristo wa karne ya kwanza walihitaji kuvumilia. Licha ya kushughulika na matatizo ambayo huwapata watu wote, pia walikabili majaribu mengine ya ziada. Wengi wao waliteswa, si tu na viongozi wa kidini Wayahudi na maofisa wa serikali Waroma, bali pia na watu wa familia zao wenyewe. (Mt. 10:21) Na wakati mwingine katika kutaniko walihitaji kukabiliana na uvutano wa waasi-imani na mafundisho yao yaliyosababisha mgawanyiko. (Mdo. 20:29, 30) Ingawa hivyo, Wakristo hao walivumilia. (Ufu. 2:3) Walifanya hivyo jinsi gani? Walitafakari mifano ya watu wanaotajwa katika Maandiko ambao walivumilia, kama vile Ayubu. (Yak. 5:10, 11) Walisali ili wapate nguvu. (Mdo. 4:29-31) Na walikazia fikira matokeo mazuri ambayo wangepata kwa kuvumilia. (Mdo. 5:41) Sisi pia tunaweza kuvumilia ikiwa tutajifunza kwa ukawaida mifano ya watu waliovumilia iliyo katika Neno la Mungu na pia katika machapisho yetu, na kutafakari kuwahusu. w23.07 3 ¶5-6
Jumapili, Desemba 14
Basi, endeleeni kuutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.—Mt. 6:33.
Yehova na Yesu hawatatuacha. Baada ya mtume Petro kumkana Yesu alihitaji kufanya uamuzi muhimu. Je, angekata tamaa, au angejitahidi kuendelea kuwa mwanafunzi mwaminifu wa Kristo? Yesu alikuwa ametoa dua kwa Yehova kwamba imani ya Petro isidhoofike. Yesu alimwambia Petro kuhusu sala hiyo na akamhakikishia Petro kwamba baadaye angewaimarisha ndugu zake. (Luka 22:31, 32) Bila shaka, Petro alitiwa moyo sana alipokumbuka maneno ya Yesu! Tunapohitaji kufanya uamuzi muhimu maishani, huenda Yehova akawatumia wachungaji wanaotujali kututia moyo ili tuendelee kuwa waaminifu. (Efe. 4:8, 11) Kama vile Yehova alivyowaandalia mahitaji ya kimwili Petro na mitume wengine, atatuandalia mahitaji yetu ya kimwili ikiwa tutatanguliza huduma maishani. w23.09 24-25 ¶14-15
Jumatatu, Desemba 15
Anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamkopesha Yehova, naye Atamlipa kwa anayotenda.—Met. 19:17.
Yehova hutambua hata matendo madogo ya fadhili tunayowatendea wengine. Anaona matendo hayo kuwa dhabihu yenye thamani na kama deni ambalo atalipa. Ikiwa zamani ulitumikia ukiwa mtumishi wa huduma au mzee, Yehova anakumbuka kazi uliyofanya wakati uliopita na upendo uliokuchochea kufanya hivyo. (1 Kor. 15:58) Pia, anaona upendo unaoendelea kuonyesha. Yehova angependa sisi sote tuimarishe upendo wetu kwake na kwa wengine. Tunaweza kuimarisha upendo wetu kwa Yehova kwa kusoma Neno lake na kulitafakari, na kwa kuzungumza naye kwa ukawaida katika sala. Tunaweza kuimarisha upendo wetu kwa ndugu na dada zetu kwa kuwasaidia kwa njia hususa. Upendo wetu unapozidi kukua, tutazidi kumkaribia Yehova na ndugu na dada zetu. Na tutafurahia urafiki huo milele! w23.07 10 ¶11; 11 ¶13; 13 ¶18
Jumanne, Desemba 16
Kila mtu ataubeba mzigo wake mwenyewe.—Gal. 6:5.
Kila Mkristo anapaswa kuamua jinsi atakavyotunza afya yake. Biblia ina sheria chache hususa, kama vile amri ya kuepuka damu na kuepuka kuwasiliana na roho ambazo zinaongoza uamuzi wa Mkristo kuhusu matibabu. (Mdo. 15:20; Gal. 5:19, 20) Mambo mengine ni maamuzi ya kibinafsi. Ingawa huenda tukasadiki kwamba aina fulani ya matibabu ndiyo inayofaa, tunahitaji kuheshimu haki ya ndugu na dada zetu ya kujifanyia maamuzi kuhusu matibabu. Kuhusu hilo, tunapaswa kukumbuka mambo yafuatayo: (1) Ufalme wa Mungu ndio tu utakaoleta uponyaji wa kudumu. (Isa. 33:24) (2) Kila Mkristo anapaswa ‘kusadiki kikamili’ jambo linalomfaa. (Rom. 14:5) (3) Hatuwahukumu wengine au kufanya wakwazike. (Rom. 14:13) (4) Wakristo wanaona umoja wa kutaniko kuwa jambo muhimu zaidi kuliko uhuru wao wa kujifanyia maamuzi ya kibinafsi.—Rom. 14:15, 19, 20. w23.07 24 ¶15
Jumatano, Desemba 17
Atakuwa mtakatifu kwa Yehova siku zote atakazokuwa Mnadhiri.—Hes. 6:8.
Je, unathamini uhusiano wako na Yehova? Bila shaka! Tangu nyakati za kale, watu wengi wamehisi kama unavyohisi. (Zab. 104:33, 34) Wengi wamejidhabihu ili kumwabudu Yehova. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Wanadhiri katika taifa la Israeli la kale, au waliowekwa wakfu. Msemo huo unafafanua vizuri Waisraeli wenye bidii ambao walijidhabihu kibinafsi ili kumtumikia Yehova kwa njia ya pekee. Sheria ya Musa ilimruhusu mwanamume au mwanamke aweke nadhiri ya pekee kwa Yehova kwa kuchagua kuishi akiwa Mnadhiri kwa kipindi fulani cha wakati. (Hes. 6:1, 2) Nadhiri hiyo, au ahadi nzito, ilihusisha kufuata miongozo ambayo Waisraeli wengine hawakuhitaji kufuata. Basi, kwa nini Mwisraeli angechagua kuweka nadhiri ya kuwa Mnadhiri? Inaelekea Mwisraeli huyo alichochewa na upendo wake wenye nguvu kwa Yehova, naye alithamini kutoka moyoni baraka Zake nyingi.—Kum. 6:5; 16:17. w24.02 14 ¶1-2
Alhamisi, Desemba 18
Yehova . . . [unawatendea] kwa upendo mshikamanifu wale wanaokupenda na kushika amri zako.—Dan. 9:4.
Katika Biblia, neno la Kiebrania linalomaanisha “ushikamanifu” au “upendo mshikamanifu,” linatokeza wazo la uhusiano mchangamfu wenye upendo ambao mara nyingi unafafanua upendo ambao Mungu huwaonyesha watumishi wake. Neno hilohilo pia linatumiwa kufafanua upendo ambao watumishi wa Mungu huonyeshana. (2 Sam. 9:6, 7) Ushikamanifu wetu unaweza kuimarika kadiri muda unavyopita. Fikiria jinsi hilo lilivyothibitika kuwa kweli kwa Danieli. Ushikamanifu wa Danieli kwa Yehova ulijaribiwa katika maisha yake yote. Lakini alijaribiwa kwa njia kubwa zaidi alipokuwa na zaidi ya umri wa miaka 90. Maofisa wa makao ya mfalme hawakumpenda Danieli na hawakumheshimu Mungu ambaye Danieli alimwabudu. Basi, walipanga njama ili Danieli auawe. Walimwomba mfalme atoe agizo ambalo lingeonyesha ikiwa Danieli alikuwa mshikamanifu kwa Mungu wake au kwa mfalme. Ili Danieli athibitishe kwamba alikuwa mshikamanifu kwa mfalme, alihitaji kuacha kusali kwa Yehova kwa siku 30. Danieli hakulegeza msimamo wake.—Dan. 6:12-15, 20-22. w23.08 5 ¶10-12
Ijumaa, Desemba 19
Endeleeni kupendana.—1 Yoh. 4:7.
Yehova anataka tuendelee kuwaonyesha upendo ndugu na dada zetu. Ikiwa ndugu au dada yetu anatutendea kwa njia isiyo ya Kikristo, tunaweza kutumaini kwamba hakukusudia kutuumiza na anajitahidi kufanya kile ambacho Yehova anakiona kuwa sawa. (Met. 12:18) Mungu anawapenda watumishi wake waaminifu licha ya hali yao ya kutokamilika. Tunapokosea, anaendelea kuwa rafiki yetu; na haendelei kuwa na hasira. (Zab. 103:9) Ni muhimu sana kumwiga Baba yetu anayesamehe! (Efe. 4:32–5:1) Pia, kumbuka kwamba kadiri mwisho unavyokaribia, ndivyo tunavyohitaji kuendelea kuwa karibu na ndugu na dada zetu. Tunaweza kutarajia mateso yatazidi kuongezeka. Huenda hata tukafungwa kwa sababu ya imani yetu. Ikiwa hilo litatokea, tutawahitaji ndugu na dada zetu kuliko wakati mwingine wowote.—Met. 17:17. w24.03 15-16 ¶6-7
Jumamosi, Desemba 20
Hatua za mtu huongozwa na Yehova.—Met. 20:24.
Maandiko yana masimulizi ya vijana ambao walimkaribia Yehova, wakapata kibali chake, na kuwa na maisha yenye kuridhisha. Daudi alikuwa mmoja wao. Alipokuwa na umri mdogo, aliamua kumwabudu Mungu na baadaye akawa mfalme mshikamanifu. (1 Fal. 3:6; 9:4, 5; 14:8) Unaweza kutiwa moyo na kuchochewa kwa kujifunza kuhusu maisha ya Daudi na jinsi alivyomtumikia Yehova kwa uaminifu. Au unaweza kuwa na mradi wa kujifunza kumhusu Marko au Timotheo. Utaona kwamba walianza kumtumikia Yehova walipokuwa na umri mdogo nao wakaendelea kumtumikia kwa uaminifu. Maisha yako ya wakati ujao yanategemea jinsi unavyotumia maisha yako sasa. Ikiwa utamtegemea Yehova badala ya uelewaji wako mwenyewe, atakusaidia kufanya maamuzi yenye hekima. Unaweza kuwa na maisha yenye furaha na yenye kuthawabisha. Kumbuka, Yehova anathamini mambo ambayo unafanya kwa ajili yake. Bila shaka, njia bora ya kutumia maisha yako ni kumtumikia Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo. w23.09 13 ¶18-19
Jumapili, Desemba 21
Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.—Kol. 3:13.
Mtume Paulo alijua kwamba ndugu na dada zake Wakristo hawakuwa wakamilifu. Kwa mfano, muda mfupi tu baada ya kuanza kushirikiana na kutaniko la Kikristo, baadhi ya ndugu na dada katika kutaniko la Yerusalemu hawakuamini kwamba Paulo amekuwa mwanafunzi. (Mdo. 9:26) Baadaye, baadhi yao walikuwa wakizungumza vibaya kumhusu ili kumharibia sifa yake nzuri. (2 Kor. 10:10) Paulo alimwona ndugu anayetegemeka akifanya uamuzi mbaya ambao huenda ungewakwaza wengine. (Gal. 2:11, 12) Na Marko, ndugu aliyeshirikiana kwa ukaribu na Paulo, alimvunja moyo sana. (Mdo. 15:37, 38) Paulo angeweza kuruhusu hali hizo zifanye aache kushirikiana na watu hao waliomkosea. Hata hivyo, aliendelea kuwathamini ndugu na dada zake na kuendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Ni nini kilichomsaidia Paulo aendelee kuwa mwaminifu? Paulo aliwapenda ndugu na dada zake. Upendo wa Paulo kwa wengine ulimsaidia kukazia fikira sifa zao nzuri, si hali yao ya kutokamilika. Upendo ulimsaidia Paulo kufanya kile kinachotajwa kwenye andiko la leo. w24.03 15 ¶4-5
Jumatatu, Desemba 22
Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote.—2 Tim. 2:24.
Biblia ina masimulizi mengi yanayoonyesha thamani ya sifa ya upole. Kwa mfano mfikirie Isaka. Alipokuwa akiishi katika eneo la Wafilisti la Gerari, jirani zake wenye wivu walifukia visima ambavyo watumishi wa baba yake walikuwa wamechimba. Badala ya kupigania visima hivyo, Isaka alihamishia familia yake sehemu nyingine na akachimba visima vingine. (Mwa. 26:12-18) Lakini Wafilisti walidai kwamba maji ya visima hivyo yalikuwa yao. Licha ya hali hizo, Isaka alidumisha amani. (Mwa. 26:19-25) Ni nini ambacho kilimsaidia aendelee kuwa mpole hata ilipoonekana kwamba wengine wameazimia kumchokoza? Bila shaka, alichunguza mfano wa wazazi wake na akajifunza mengi kutokana na jinsi Abrahamu alivyodumisha amani na jinsi ambavyo Sara alikuwa na “roho ya utulivu na ya upole.”—1 Pet. 3:4-6; Mwa. 21:22-34. w23.09 15 ¶4
Jumanne, Desemba 23
Nimekusudia, nami pia nitalitekeleza.—Isa. 46:11.
Kwa upendo, Yehova alimtuma Mwana wake mzaliwa wa kwanza aje duniani ili kuwafundisha watu kuhusu Ufalme na kutoa uhai wake uwe fidia kwa ajili ya kutukomboa kutoka katika dhambi na kifo. Kisha Yesu akafufuliwa na kurudi mbinguni ili atawale akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Kichwa kikuu cha Biblia ni kwamba jina la Yehova litatetewa anapoendelea kutimiza kusudi lake kwa ajili ya dunia kupitia Ufalme wake unaoongozwa na Kristo. Kusudi la Yehova haliwezi kubadilishwa. Ametoa uhakikisho kwamba atafanikiwa kulitimiza. (Isa. 46:10, maelezo ya chini; Ebr. 6:17, 18) Hatimaye, dunia itabadilishwa na kuwa paradiso ambamo wazao wakamilifu na waadilifu wa Adamu na Hawa ‘watafurahia maisha milele.’ (Zab. 22:26) Lakini Yehova atatimiza mambo mengi zaidi, kusudi lake ni hatimaye kuunganisha viumbe wake wote wenye akili walio mbinguni na duniani. Kisha wote walio hai watajitiisha chini yake kwa ushikamanifu akiwa Mwenye Enzi Kuu wao. (Efe. 1:8-11) Je, hustaajabishwi na jinsi Yehova anavyotimiza kusudi lake kwa njia yenye kupendeza? w23.10 20 ¶7-8
Jumatano, Desemba 24
“Jipeni moyo, . . . kwa maana niko pamoja nanyi,” asema Yehova wa majeshi.—Hag. 2:4.
Muda mfupi baada ya Wayahudi walioondoka Babiloni kufika Yerusalemu, walianza kuathiriwa na hali mbaya ya kiuchumi, kisiasa, pamoja na upinzani. Kwa hiyo, baadhi yao walishindwa kukazia fikira kazi ya kujenga upya hekalu la Yehova. Hivyo, Yehova aliwatuma manabii wawili, Hagai na Zekaria, ili kuchochea upya bidii ya watu wake, kazi ambayo ilikuwa na matokeo mazuri. (Hag. 1:1; Zek. 1:1) Hata hivyo, karibu miaka 50 baadaye, Wayahudi hao walipunguza bidii yao tena. Ezra, mwandishi wa Sheria mwenye ustadi, alitoka Babiloni kwenda Yerusalemu ili kuwatia moyo watu wa Mungu watangulize ibada ya kweli. (Ezra 7:1, 6) Kama unabii wa Hagai na Zekaria ulivyowasaidia watu wa Mungu kuendelea kumtumaini Yehova wakati wa upinzani, ndivyo unavyoweza kutusaidia kuendelea kuwa na uhakika katika msaada wa Yehova licha ya changamoto zisizotarajiwa.—Met. 22:19. w23.11 14-15 ¶2-3
Alhamisi, Desemba 25
Jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.—Kol. 3:14.
Tunawezaje kuwaonyesha upendo waabudu wenzetu? Njia moja ya kufanya hivyo ni kwa kuwafariji. Tutaweza ‘kuendelea kufarijiana’ ikiwa tutachochewa na huruma. (1 The. 4:18) Tunawezaje kuimarisha upendo miongoni mwetu? Kwa kujitahidi kadiri tuwezavyo kusamehe makosa ya wengine. Kwa nini ni muhimu hasa leo kuonyesha upendo miongoni mwetu? Ona sababu ambayo Petro aliitoa, aliposema hivi: “Mwisho wa mambo yote umekaribia. Kwa hiyo, . . . pendaneni sana.” (1 Pet. 4:7, 8) Kadiri mwisho wa mfumo huu unavyokaribia, tunaweza kutarajia nini? Yesu alitabiri hivi alipozungumza kuhusu wafuasi wake: “Mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.” (Mt. 24:9) Ili kuvumilia chuki hiyo, tunahitaji kuendelea kudumisha umoja. Tukifanya hivyo, jitihada za Shetani za kutugawanya hazitafanikiwa, kwa sababu tutakuwa tumeunganishwa pamoja kwa upendo.—Flp. 2:1, 2. w23.11 13 ¶18-19
Ijumaa, Desemba 26
Sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu.—1 Kor. 3:9.
Kweli za Neno la Mungu zina nguvu nyingi. Tunapowafundisha watu kuhusu Yehova na kuwasaidia waujue kabisa utu wa Yehova, tunajionea jambo zuri sana. Hatua kwa hatua watu hawadanganywi tena na uwongo wa Shetani, wanaanza kumwona Baba yetu mpendwa kama sisi tunavyomwona. Wanastaajabishwa sana na nguvu zake zisizo na kifani. (Isa. 40:26) Wanajifunza kumtumaini kwa sababu ya haki yake kamilifu. (Kum. 32:4) Wanaelimishwa na hekima yake nyingi. (Isa. 55:9; Rom. 11:33) Na wanafarijika kujua kwamba sifa yake kuu ni upendo. (1 Yoh. 4:8) Kadiri wanavyomkaribia Yehova zaidi, tumaini lao la kuishi milele wakiwa watoto wake linakuwa la hakika zaidi. Ni pendeleo lililoje kuwasaidia watu wamkaribie Baba yao! Tunapofanya hivyo, Yehova anatuona kuwa “wafanyakazi wenzi.”—1 Kor. 3:5. w24.02 12 ¶15
Jumamosi, Desemba 27
Ni afadhali usiweke nadhiri kuliko kuweka nadhiri na kukosa kuitimiza.—Mhu. 5:5.
Ikiwa wewe ni mwanafunzi wa Biblia au unalelewa na wazazi ambao ni Mashahidi wa Yehova, je, unafikiria kubatizwa? Hilo ni lengo nzuri sana! Lakini kabla ya kubatizwa, utahitaji kujiweka wakfu kwa Yehova. Unajiweka wakfu kwa Yehova jinsi gani? Unamwahidi katika sala kwamba utamwabudu yeye peke yake na kwamba utatanguliza mapenzi yake katika maisha yako. Kwa kweli, unamwahidi Yehova kwamba utaendelea kumpenda “kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Unajiweka wakfu ukiwa faraghani, na ni kati yako na Yehova. Tofauti na hilo, ubatizo hufanywa hadharani; unawaonyesha wengine kwamba tayari umejiweka wakfu kwa Yehova. Wakfu wako ni nadhiri takatifu. Lengo lako linapaswa kuwa kutimiza ahadi hiyo na Yehova anatarajia ufanye hivyo.—Mhu. 5:4. w24.03 2 ¶2; 3 ¶5
Jumapili, Desemba 28
Kila mtu kati yenu anapaswa kumpenda mke wake kama anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.—Efe. 5:33.
Ndoa zote zinakabili changamoto fulani. Biblia inaeleza wazi kwamba watu waliofunga ndoa “watakuwa na dhiki katika mwili wao.” (1 Kor. 7:28) Kwa nini? Kwa sababu ndoa inawaunganisha watu wawili wasio wakamilifu, kila mmoja ana sifa tofauti na mwenzake na ana mambo anayopenda na asiyopenda. Wenzi wa ndoa wanaweza kutoka kwenye utamaduni na malezi tofauti. Baada ya muda, huenda wakaonyesha tabia ambazo hazikutambuliwa kabla ya kufunga ndoa. Mambo hayo yanaweza kusababisha matatizo. Badala ya kutambua jinsi kila mmoja alivyochangia tatizo na hivyo kujitahidi kulisuluhisha, huenda mwenzi mmoja akamlaumu mwenzake. Huenda hata wakahisi suluhisho ni kutengana au kutalikiana. Je, watakuwa na furaha wakitengana au kutalikiana? Hapana. Yehova anawaagiza watu waliofunga ndoa waheshimu mpango wa ndoa hata ikiwa wanaishi na mtu ambaye ni vigumu kuishi naye. w24.03 16 ¶8; 17 ¶11
Jumatatu, Desemba 29
Tumaini halikatishi tamaa.—Rom. 5:5.
Baada ya kujiweka wakfu na kubatizwa, tumaini lako la kuishi milele katika dunia paradiso liliendelea kukua kadiri ulivyoendelea kujifunza mengi na kukomaa kiroho. (Ebr. 5:13–6:1) Inaelekea umejionea mambo yanayotajwa kwenye Waroma 5:2-4. Ulikabili dhiki mbalimbali, lakini ulivumilia na kuhisi kibali cha Mungu. Ukiwa na uhakika kwamba una kibali cha Mungu, sasa una sababu kubwa hata zaidi ya kutarajia kupokea mambo aliyoahidi. Tumaini lako limekuwa imara zaidi kuliko mwanzoni. Limekuwa halisi zaidi kwako, linakugusa kibinafsi. Linakuchochea zaidi, linakuongoza katika kila sehemu ya maisha yako na kubadili jinsi unavyowatendea watu wa familia yako, jinsi unavyofanya maamuzi, na hata jinsi unavyotumia wakati wako. Mtume Paulo anataja jambo lingine muhimu sana kuhusu tumaini tunalokuwa nalo baada ya kupata kibali cha Mungu. Anakuhakikishia kwamba tumaini lako litatimizwa.—Rom. 15:13. w23.12 12-13 ¶16-19
Jumanne, Desemba 30
[Yehova] ndiye tegemeo imara la nyakati zako.—Isa. 33:6.
Tunapopatwa na hali ngumu, huenda tukahisi, tukafikiri, au kutenda kwa njia tofauti na ile tuliyozoea. Huenda tukahisi kama meli inayosukumwa huku na huku na mawimbi katika bahari yenye dhoruba. Yehova anatusaidiaje hisia kama hizo zinapotulemea? Anatuhakikishia kwamba atatuimarisha. Meli inapokabiliwa na dhoruba, inaweza kuyumbayumba kwa njia ya hatari. Ili zisiyumbeyumbe, meli nyingi zimewekewa vifaa vya pekee vinavyoisaidia meli itulie na iwe imara. Vifaa hivyo vya pekee vinaisaidia meli isiyumbe sana na kufanya safari iwe salama na yenye kustarehesha. Hata hivyo, mifumo hiyo ya kuimarisha meli hufanya kazi vizuri zaidi ikiwa meli inasonga mbele. Vivyo hivyo, Yehova atatuimarisha tunaposonga mbele kwa uaminifu wakati wa majaribu. w24.01 22 ¶7-8
Jumatano, Desemba 31
Katika Mungu ninaweka tumaini langu; siogopi.—Zab. 56:4.
Unapoogopa, jiulize hivi, ‘Ni mambo gani ambayo tayari Yehova amenifanyia?’ Tafakari kuhusu vitu alivyoumba. Kwa mfano, ‘tunapoangalia kwa makini’ jinsi Yehova anavyowatunza ndege na maua—ambayo hakuyaumba kwa mfano wake na wala hayana uwezo wa kumwabudu—tunaweza kuimarisha uhakika wetu kwamba atatutunza sisi pia. (Mt. 6:25-32) Fikiria pia mambo ambayo Yehova amewafanyia waabudu wake. Unaweza kujifunza kuhusu mwabudu wake anayetajwa katika Biblia ambaye alionyesha imani ya pekee, au unaweza kusoma kuhusu simulizi la maisha la mtumishi wa Yehova katika siku zetu. Zaidi ya hayo, tafakari kuhusu jinsi ambavyo Yehova tayari amekutunza. Alikuvutaje katika kweli? (Yoh. 6:44) Amejibuje sala zako? (1 Yoh. 5:14) Unanufaikaje kila siku kutokana na dhabihu ya Mwana wake mpendwa?—Efe. 1:7; Ebr. 4:14-16. w24.01 4 ¶6; 7 ¶17