Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • es25 kur. 88-97
  • Septemba

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Septemba
  • Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025
  • Vichwa vidogo
  • Jumatatu, Septemba 1
  • Jumanne, Septemba 2
  • Jumatano, Septemba 3
  • Alhamisi, Septemba 4
  • Ijumaa, Septemba 5
  • Jumamosi, Septemba 6
  • Jumapili, Septemba 7
  • Jumatatu, Septemba 8
  • Jumanne, Septemba 9
  • Jumatano, Septemba 10
  • Alhamisi, Septemba 11
  • Ijumaa, Septemba 12
  • Jumamosi, Septemba 13
  • Jumapili, Septemba 14
  • Jumatatu, Septemba 15
  • Jumanne, Septemba 16
  • Jumatano, Septemba 17
  • Alhamisi, Septemba 18
  • Ijumaa, Septemba 19
  • Jumamosi, Septemba 20
  • Jumapili, Septemba 21
  • Jumatatu, Septemba 22
  • Jumanne, Septemba 23
  • Jumatano, Septemba 24
  • Alhamisi, Septemba 25
  • Ijumaa, Septemba 26
  • Jumamosi, Septemba 27
  • Jumapili, Septemba 28
  • Jumatatu, Septemba 29
  • Jumanne, Septemba 30
Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025
es25 kur. 88-97

Septemba

Jumatatu, Septemba 1

Tutapata mapambazuko kutoka juu.—Luka 1:78.

Mungu amempa Yesu nguvu za kutatua matatizo yote ya wanadamu. Kupitia miujiza yake, Yesu alionyesha kwamba ana nguvu za kutatua matatizo yote ambayo hatuwezi kusuluhisha. Kwa mfano, ana uwezo wa kutuweka huru kutoka kwa chanzo cha matatizo ya wanadamu, yaani, dhambi tuliyorithi na matokeo yake, ugonjwa na kifo. (Mt. 9:​1-6; Rom. 5:​12, 18, 19) Miujiza aliyofanya inathibitisha kwamba anaweza kuponya “kila aina ya ugonjwa” na hata kuwafufua wafu. (Mt. 4:23; Yoh. 11:​43, 44) Pia, ana nguvu za kudhibiti dhoruba kali ya upepo na kuwashinda roho waovu. (Marko 4:​37-39; Luka 8:2) Tunafarijika kujua kwamba Yehova amempa Mwana wake nguvu hizo! Tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba baraka za wakati ujao chini ya Ufalme wa Mungu zitatimia. Miujiza ambayo Yesu alifanya alipokuwa mwanadamu duniani, inatufundisha mambo atakayofanya kwa kiwango kikubwa zaidi akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu ulio mbinguni. w23.04 3 ¶5-7

Jumanne, Septemba 2

Roho huchunguza ndani ya mambo yote, hata mambo mazito ya Mungu.—1 Kor. 2:10.

Ikiwa upo kwenye kutaniko kubwa na unahisi kwamba mara nyingi hupati nafasi ya kutoa maelezo, huenda ukashawishiwa kutoinua mkono tena. Lakini usiache kujitahidi kutoa maelezo. Tayarisha maelezo kadhaa kwa ajili ya kila mkutano. Kisha ikiwa hutachaguliwa kutoa maelezo mwanzoni mwa funzo, bado utakuwa na nafasi nyingine ya kutoa maelezo mkutano unapoendelea. Unapotayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi, fikiria jinsi kila fungu linavyohusiana na kichwa kikuu cha makala. Ukifanya hivyo, inaelekea kwamba utakuwa tayari kutoa maelezo wakati wowote wa funzo. Isitoshe, unaweza kujitayarisha kutoa maelezo katika mafungu ambayo yanazungumzia mafundisho mazito ya Biblia ambayo ni vigumu zaidi kuyaelezea. Kwa nini? Kwa sababu huenda si watu wengi watainua mkono katika sehemu hiyo. Namna gani ikiwa unatambua kwamba baada ya mikutano kadhaa bado hujapata nafasi ya kutoa maelezo? Kabla ya mkutano, mweleze yule anayeongoza swali ambalo ungependa kujibu. w23.04 21-22 ¶9-10

Jumatano, Septemba 3

Yosefu akaamka . . . na kufanya kama alivyoambiwa na malaika wa Yehova, akampeleka mke wake nyumbani.—Mt. 1:24.

Yosefu alikuwa tayari kufuata mwongozo wa Yehova, na hilo lilimfanya awe mume mzuri. Katika pindi tatu tofauti, alipata mwongozo kutoka kwa Yehova kuhusu familia yake. Kila mara, alitii bila kusita, hata ilipomaanisha kufanya mabadiliko makubwa. (Mt. 1:20; 2:​13-15, 19-21) Kwa kufuata mwongozo wa Yehova, Yosefu alimlinda Maria, akamtegemeza, na kumwandalia mahitaji yake. Wazia jinsi matendo ya Yosefu yalivyomfanya Maria ampende na kumheshimu hata zaidi! Waume, mnaweza kumwiga Yosefu kwa kutafuta ushauri katika Biblia kuhusu jinsi ya kutunza familia zenu. Unapofuata ushauri huo, hata ikimaanisha kufanya mabadiliko fulani, unaonyesha kwamba unampenda mke wako na unaimarisha ndoa yenu. Dada mmoja nchini Vanuatu ambaye amefunga ndoa kwa zaidi ya miaka 20 anasema hivi: “Mume wangu anapotafuta na kufuata mwongozo wa Yehova, ninamheshimu hata zaidi. Ninajihisi salama, na nina uhakika katika maamuzi anayofanya.” w23.05 21 ¶5

Alhamisi, Septemba 4

Huko kutakuwa na barabara kuu, naam, njia inayoitwa Njia ya Utakatifu.—Isa. 35:8.

Wayahudi waliorudi kutoka Babiloni walipaswa kuwa “watu watakatifu” kwa Mungu wao. (Kum. 7:6) Hata hivyo, hilo halikumaanisha kwamba hawakuhitaji kufanya mabadiliko ili kumfurahisha Yehova. Wayahudi wengi waliozaliwa huko Babiloni walikuwa wameathiriwa na njia ya kufikiri na mazoea ya Wababiloni. Miaka mingi baada ya kikundi cha kwanza cha Wayahudi kurudi Israeli, Gavana Nehemia alishangaa alipotambua kwamba watoto ambao walikuwa wamezaliwa huko Israeli, hata hawakuwa wamejifunza lugha ya Kiyahudi. (Kum. 6:​6, 7; Neh. 13:​23, 24) Watoto hao wangewezaje kujifunza kumpenda na kumwabudu Yehova ikiwa hawangeweza kuelewa Kiebrania—lugha kuu ambayo ilitumiwa kuandika Neno la Mungu? (Ezra 10:​3, 44) Basi, Wayahudi hao walihitaji kufanya mabadiliko makubwa, lakini ingekuwa rahisi zaidi kwao kufanya mabadiliko hayo wakiwa huko Israeli, ambako ibada safi ilikuwa inarudishwa hatua kwa hatua.—Neh. 8:​8, 9. w23.05 15 ¶6-7

Ijumaa, Septemba 5

Yehova huwategemeza wote wanaoanguka na kuwainua juu wote walioinama chini.—Zab. 145:14.

Inasikitisha kwamba hata tuwe tumechochewa au tuna nidhamu kadiri gani, bado huenda tutakabili vipingamizi vinavyofanya iwe vigumu kufikia malengo yetu. Kwa mfano, “matukio yasiyotarajiwa” yanaweza kuchukua muda tunaohitaji ili tufanyie kazi lengo letu. (Mhu. 9:11) Huenda tukakabili hali ngumu ambayo itatuacha tukiwa tumevunjika moyo na kuishiwa nguvu. (Met. 24:10) Kwa kuwa hatujakamilika, huenda tukafanya makosa ambayo yatafanya iwe vigumu kutimiza lengo letu. (Rom. 7:23) Au huenda tukahisi tu kwamba tumechoka. (Mt. 26:43) Ni nini kinachoweza kutusaidia kushinda vipingamizi au hali ngumu? Kumbuka, kipingamizi hakimaanishi kwamba umeshindwa. Biblia inasema kwamba huenda tukakabili tena na tena matatizo au hali ngumu. Hata hivyo, pia inataja wazi kwamba tunaweza kusimama tena. Naam, ukisonga mbele licha ya vipingamizi, unamthibitishia Yehova kwamba unataka kumfurahisha. Bila shaka, Yehova anafurahi sana anapoona ukijitahidi kutimiza lengo lako! w23.05 30 ¶14-15

Jumamosi, Septemba 6

[Iweni] vielelezo kwa kundi.—1 Pet. 5:3.

Upainia unamsaidia mwanamume kijana kujifunza jinsi ya kufanya kazi vizuri pamoja na watu mbalimbali. Pia, unamsaidia kupanga bajeti vizuri na kushikamana nayo. (Flp. 4:​11-13) Njia nzuri ya kuanza utumishi wa wakati wote ni kufanya upainia msaidizi, jambo ambalo litakusaidia kuwa tayari kuanza upainia wa kawaida. Upainia unaweza kufungua mlango unaoongoza kwenye aina nyingine za utumishi wa wakati wote, kutia ndani kutumikia ukiwa mjenzi au Mwanabetheli. Wanaume Wakristo wanapaswa kuwa na lengo la kustahili kuwatumikia ndugu na dada zao wakiwa wazee wa kutaniko. Biblia inasema kwamba wanaume wanaojitahidi kufikia jukumu hilo ‘wanatamani kazi njema.’ (1 Tim. 3:1) Kwanza, ni lazima ndugu astahili kutumikia akiwa mtumishi wa huduma. Watumishi wa huduma wanawasaidia wazee kwa njia nyingi hususa. Wazee na watumishi wa huduma wanawatumikia kwa unyenyekevu ndugu na dada zao na kushiriki kwa bidii katika huduma. w23.12 28 ¶14-16

Jumapili, Septemba 7

Alipokuwa angali mvulana, alianza kumtafuta Mungu wa Daudi babu yake.—2 Nya. 34:3.

Mfalme Yosia alikuwa tineja alipoanza kumtafuta Yehova. Alitaka kujifunza kumhusu Yehova na kufanya mapenzi Yake. Hata hivyo, maisha hayakuwa rahisi kwa mfalme huyo kijana. Alihitaji kuchukua msimamo upande wa ibada safi wakati ambapo ibada ya uwongo ilikuwa imeenea. Na kwa kweli, alifanya hivyo! Kabla Yosia hajafikisha umri wa miaka 20, alianza kuondoa ibada ya uwongo katika taifa hilo. (2 Nya. 34:​1, 2) Hata ikiwa wewe ni kijana, unaweza kuamua kumwiga Yosia kwa kumtafuta Yehova na kujifunza kuthamini sifa Zake. Ukifanya hivyo, utachochewa kujiweka wakfu kwake. Kujiweka wakfu kutaathirije maisha yako ya kila siku? Luke, ambaye alibatizwa akiwa na umri wa miaka 14, anasema hivi: “Kuanzia sasa na kuendelea, nitatanguliza kumtumikia Yehova maishani mwangu na nitajitahidi kumfurahisha.” (Marko 12:30) Wewe pia utapata baraka ikiwa unatamani kufanya hivyo! w23.09 11 ¶12-13

Jumatatu, Septemba 8

Waheshimuni wale wanaofanya kazi kwa bidii miongoni mwenu na wanaowasimamia katika Bwana.—1 The. 5:12.

Mtume Paulo alipoandika barua hiyo, mwaka mmoja haukuwa umepita tangu kutaniko la Thesalonike lilipoanzishwa. Inaonekana kwamba wanaume waliowekwa rasmi hawakuwa na uzoefu na huenda walifanya makosa. Ingawa hivyo, walistahili kuheshimiwa. Dhiki kuu inapokaribia, huenda tukategemea hata zaidi mwongozo kutoka kwa wazee wa kutaniko kuliko ilivyo sasa. Huenda tukapoteza mawasiliano na makao makuu ya ulimwenguni pote au ofisi ya tawi; basi, ni jambo muhimu kujifunza sasa kuwapenda na kuwaheshimu wazee wa kutaniko. Hata jambo gani litokee, acheni tuendelee kutunza akili zetu, tusikazie fikira udhaifu wao, bali tukazie fikira kwamba Yehova anawaongoza wanaume hao waaminifu kupitia Kristo. Kama vile kofia ya chuma ilivyolinda kichwa cha mwanajeshi, tumaini letu la wokovu hulinda mawazo yetu. Tunatambua kwamba mambo yaliyo katika ulimwengu huu hayana thamani yoyote. (Flp. 3:8) Tumaini letu linatusaidia kuendelea kuwa watulivu na thabiti. w23.06 11-12 ¶11-12

Jumanne, Septemba 9

Mwanamke mpumbavu ana kelele. Yeye ni mjinga.—Met. 9:13.

Wale wanaosikia sauti ya “mwanamke mpumbavu” wanahitaji kufanya uamuzi huu: Je, watakubali mwaliko wake au wataukataa? Tuna sababu nzuri sana zinazotuchochea tuepuke uasherati. “Mwanamke mpumbavu” anafafanuliwa kuwa anasema hivi: “Maji yaliyoibwa ni matamu.” (Met. 9:17) “Maji yaliyoibwa” ni nini? Biblia inalinganisha uhusiano wa kingono ambao watu waliofunga ndoa hufurahia na maji yenye kuburudisha. (Met. 5:​15-18) Mume na mke waliofunga ndoa kisheria wanaweza kufurahia kufanya ngono. Hata hivyo, mambo ni tofauti kuhusu “maji yaliyoibwa.” Maji hayo yanarejelea uasherati. Watu hufanya uasherati kisiri kama mwizi anavyoiba kisiri. ‘Maji hayo yaliyoibwa’ huenda yakaonekana kuwa matamu hasa ikiwa wale wanaohusika wanafikiri kwamba hakuna mtu atakayejua jambo hilo. Kwa kweli wanajidanganya! Yehova anaona mambo yote. Ikiwa tutapoteza kibali cha Yehova, tutapatwa na uchungu mwingi sana na kwa kweli hilo si jambo ‘tamu’ au linalofurahisha.—1 Kor. 6:​9, 10. w23.06 22 ¶7-9

Jumatano, Septemba 10

Hata nikifanya hivyo bila kupenda, bado nimekabidhiwa usimamizi.—1 Kor. 9:17.

Utafanya nini ikiwa unahisi sala zako hazitoki moyoni, au hufurahii utumishi kama ilivyokuwa zamani? Usifikie mkataa kwamba umepoteza roho ya Yehova. Kwa kuwa wewe si mkamilifu, hisia zako zinaweza kubadilika mara kwa mara. Ikiwa bidii yako inaanza kupungua, tafakari mfano wa mtume Paulo. Ingawa alijitahidi kumwiga Yesu, alijua kwamba nyakati nyingine huenda hangekuwa na tamaa kubwa ya kufanya kile alichohitaji kufanya. Paulo aliazimia kutimiza huduma yake licha ya jinsi ambavyo huenda angehisi wakati huo. Vivyo hivyo, usifanye maamuzi kwa kutegemea tu jinsi unavyohisi. Azimia kufanya lililo sawa licha ya jinsi unavyohisi. Ikiwa utaendelea kufanya yaliyo sawa, baada ya muda huenda hisia zako zikabadilika.—1 Kor. 9:16. w24.03 11-12 ¶12-13

Alhamisi, Septemba 11

Thibitisheni upendo wenu kwao.—2 Kor. 8:24.

Tunawaonyesha upendo ndugu na dada zetu kwa kuwakaribisha wawe rafiki zetu. (2 Kor. 6:​11-13) Wengi wetu tunashirikiana na makutaniko yenye ndugu na dada kutoka katika malezi mbalimbali na wenye nyutu mbalimbali. Tunaweza kuimarisha upendo wetu kuelekea watu wote kwa kukazia fikira sifa zao nzuri. Tunapojifunza kuwaona wengine kama Yehova anavyowaona, tunathibitisha kwamba tunawapenda. Tutahitaji kuonyeshana upendo wakati wa dhiki kuu. Dhiki kuu itakapoanza tutapata wapi ulinzi? Fikiria jambo ambalo Yehova aliwaagiza watu wake wafanye Babiloni la kale liliposhambuliwa: “Nendeni, watu wangu, ingieni katika vyumba vyenu vya ndani, na mfunge milango nyuma yenu. Jificheni kwa muda mfupi mpaka ghadhabu itakapopita.” (Isa. 26:20) Inaonekana kwamba maneno hayo yanatuhusu pia sisi ambao tutakabiliana na dhiki kuu. w23.07 6-7 ¶14-16

Ijumaa, Septemba 12

Tamasha ya ulimwengu huu inabadilika.—1 Kor. 7:31.

Ujulikane kuwa mtu mwenye usawaziko. Jiulize hivi: ‘Je, watu wananiona kuwa mwenye usawaziko, mwenye kukubali sababu, na kuwavumilia wengine? Au je, wanaona kwamba ninashikilia maoni yangu, ni mkali, au mwenye kichwa kigumu? Je, ninawasikiliza wengine na kukubaliana na maoni yao inapofaa?’ Kadiri tunavyozidi kuwa wenye usawaziko, ndivyo tunavyoonyesha kwamba tunamwiga Yehova na Yesu. Usawaziko unahusisha kunyumbulika hali zetu zinapobadilika. Mabadiliko hayo yanaweza kutusababishia matatizo tusiyotarajia. Huenda ukapatwa na ugonjwa ghafla. Au mabadiliko ya ghafla ya hali ya kiuchumi au ya kisiasa yanapotokea mahali tunapoishi yanaweza kuvuruga kabisa maisha yetu. (Mhu. 9:11) Huenda hata tukakabili hali ngumu tunapopata badiliko la mgawo wa kitheokrasi. Tunaweza kufanikiwa kunyumbulika hali zinapobadilika ikiwa tutachukua hatua nne zifuatazo: (1) kubali kwamba mambo yamebadilika, (2) fikiria kuhusu wakati ujao, (3) kazia fikira mambo yanayojenga, na (4) uwasaidie wengine. w23.07 21-22 ¶7-8

Jumamosi, Septemba 13

Wewe ni mtu mwenye thamani sana.—Dan. 9:23.

Nabii Danieli alikuwa kijana Wababiloni walipomfanya kuwa mfungwa na kumpeleka nchi ya mbali huko Babiloni. Lakini ni wazi kwamba Danieli aliwafurahisha wale waliomchukua mateka. Waliona kile “kinachoonekana kwa macho”—kwamba Danieli ‘hakuwa na kasoro yoyote, alikuwa mzuri kwa umbo’ na alitoka kwenye familia mashuhuri. (1 Sam. 16:7) Kutokana na sababu hizo, Wababiloni walimzoeza ili atumikie kwenye makao ya mfalme. (Dan. 1:​3, 4, 6) Yehova alimpenda Danieli kwa sababu ya sifa alizoamua kusitawisha. Kwa kweli, huenda Danieli alikuwa mwishoni mwa miaka yake ya utineja au mwanzoni mwa miaka yake ya 20, Yehova alipomtaja kwa njia nzuri pamoja na Noa na Ayubu, wanaume ambao walikuwa wamemtumikia Mungu kwa uaminifu kwa miaka mingi. (Mwa. 5:32; 6:​9, 10; Ayu. 42:​16, 17; Eze. 14:14.) Na Yehova aliendelea kumpenda Danieli katika maisha yake yote marefu yenye mambo ya kustaajabisha.—Dan. 10:​11, 19. w23.08 2 ¶1-2

Jumapili, Septemba 14

Kufahamu kikamili upana na urefu na kimo na kina.—Efe. 3:18.

Unapotaka kununua nyumba, ungependa kuichunguza kwa kina nyumba hiyo wewe mwenyewe. Tunaweza kufanya jambo kama hilo tunaposoma na kujifunza Biblia. Ikiwa utaisoma haraka-haraka, huenda ukajifunza habari za msingi tu, yaani, “mambo ya msingi ya maneno matakatifu ya Mungu.” (Ebr. 5:12) Badala yake, kama ilivyokuwa kwa ile nyumba, unapaswa kuingia “ndani” na kuichunguza Biblia kwa makini ili uielewe kikamili zaidi. Njia bora ya kujifunza Biblia ni kuona jinsi sehemu mbalimbali za ujumbe wake zinavyohusiana. Jitahidi kuelewa ni kweli gani ambazo unaamini na kwa nini unaamini kweli hizo. Ili kuelewa kikamili Neno la Mungu, tunapaswa kujifunza kweli zenye kina za Biblia. Mtume Paulo aliwahimiza ndugu na dada zake Wakristo wajifunze Neno la Mungu kwa bidii ili “[wafahamu] kikamili upana na urefu na kimo na kina” cha ile kweli, kisha wangekuwa na “mizizi na kuimarishwa” katika imani yao. (Efe. 3:​14-19) Sisi tunahitaji kufanya hivyo pia. w23.10 18 ¶1-3

Jumatatu, Septemba 15

Akina ndugu, fuateni mfano wa manabii waliopatwa na uovu na kuonyesha subira na ambao walisema katika jina la Yehova.—Yak. 5:10.

Biblia ina mifano mingi ya watu walioonyesha subira. Kwa nini usijiwekee lengo la kufanya utafiti kuhusu mifano ambayo watu hao walituwekea? Kwa mfano, ingawa Daudi alitiwa mafuta alipokuwa na umri mdogo ili awe mfalme wa wakati ujao wa Israeli, alisubiri kwa miaka mingi kabla ya kuanza kutawala akiwa mfalme. Simeoni na Ana walimwabudu Yehova kwa uaminifu walipokuwa wakimsubiri Masihi aliyeahidiwa. (Luka 2:​25, 36-38) Unapochunguza masimulizi hayo, tafuta majibu ya maswali yafuatayo: Ni nini ambacho huenda kilimsaidia mtu huyo awe mwenye subira? Alinufaikaje kwa kuonyesha subira? Ninawezaje kumwiga? Huenda pia ukanufaika kwa kujifunza kutokana na wale ambao hawakuonyesha subira. (1 Sam. 13:​8-14) Unaweza kujiuliza hivi: ‘Ni nini kilichofanya wakose subira? Walipatwa na matokeo gani mabaya?’ w23.08 25 ¶15

Jumanne, Septemba 16

Tumeamini na tumejua kwamba wewe ndiye Mtakatifu wa Mungu.—Yoh. 6:69.

Mtume Petro alikuwa mshikamanifu; hakuruhusu jambo lolote limzuie kuendelea kumfuata Yesu. Kwa mfano, pindi fulani alionyesha ushikamanifu wake Yesu aliposema jambo ambalo wanafunzi wake hawakuelewa. (Yoh. 6:68) Bila kusubiri ufafanuzi, wengi waliacha kumfuata Yesu. Lakini Petro hakuacha. Alitambua kwamba Yesu tu ndiye aliyekuwa na “maneno ya uzima wa milele.” Yesu alijua kwamba Petro na wale mitume wengine wangemwacha. Ingawa hivyo, Yesu alikuwa na uhakika kwamba Petro angerudi na kuendelea kuwa mwaminifu. (Luka 22:​31, 32) Yesu alielewa kwamba “roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.” (Marko 14:38) Hivyo, hata baada ya Petro kukana kwamba hamjui Yesu, Yesu hakumwacha mtume huyo. Baada ya kufufuliwa Yesu alimtokea Petro—inaonekana Petro alikuwa peke yake. (Marko 16:7; Luka 24:34; 1 Kor. 15:5) Hilo lilimwimarisha mtume huyo ambaye alikuwa amehuzunika sana! w23.09 22 ¶9-10

Jumatano, Septemba 17

Wenye furaha ni wale ambao matendo yao ya kuasi sheria yamesamehewa na ambao dhambi zao zimefunikwa.—Rom. 4:7.

Mungu anasamehe au kufunika dhambi za wale wanaoweka imani kwake. Anawasamehe kabisa na hatahesabu dhambi zao kamwe. (Zab. 32:​1, 2) Yehova anawaona watu hao kuwa hawana hatia na waadilifu kwa msingi wa imani yao. Ingawa Abrahamu, Daudi, na waabudu wengine waaminifu wa Mungu walitangazwa kuwa waadilifu, bado walikuwa watenda dhambi wasio wakamilifu. Lakini kwa sababu ya imani yao, Mungu aliwaona kuwa wasio na hatia hasa alipowalinganisha na wale ambao hawakuwa na imani kwake. (Efe. 2:12) Kama mtume Paulo anavyoeleza waziwazi kwenye barua yake, ni lazima mtu awe na imani ili kuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu. Ndivyo ilivyokuwa kwa Abrahamu na Daudi, na ni hivyo kwetu pia. w23.12 3 ¶6-7

Alhamisi, Septemba 18

Sikuzote na tumtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo yetu ambalo hulitangaza jina lake hadharani.—Ebr. 13:15.

Leo, Wakristo wote wana pendeleo la kumtolea Yehova dhabihu kwa kutumia wakati, nguvu, na mali zao, ili kuendeleza kazi ya Ufalme wa Mungu. Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini pendeleo letu la kumwabudu Yehova kwa kumtolea dhabihu zetu zilizo bora kabisa. Mtume Paulo anataja mambo mbalimbali kuhusu ibada yetu ambayo hatupaswi kamwe kuyapuuza. (Ebr. 10:​22-25) Mambo hayo yanatia ndani kumkaribia Yehova katika sala, kutoa tangazo la hadharani la tumaini letu, kukutana pamoja tukiwa kutaniko, na kutiana moyo “zaidi kwa kadiri [tunavyoona] siku ile [ya Yehova] ikikaribia.” Karibu na mwisho wa simulizi la Ufunuo, malaika wa Yehova anasema maneno yafuatayo mara mbili ili kusisitiza: “Mwabudu Mungu!” (Ufu. 19:10; 22:9) Acheni tuendelee kukumbuka kweli hizi zenye kina za kiroho kuhusu hekalu kubwa la kiroho la Yehova na pendeleo letu lenye thamani la kumwabudu Mungu wetu Mkuu! w23.10 29 ¶17-18

Ijumaa, Septemba 19

Tuendelee kupendana.—1 Yoh. 4:7.

Sote tunataka ‘kuendelea kupendana.’ Hata hivyo, ni muhimu kukumbuka kwamba Yesu alionya kuwa “upendo wa wengi [ungepoa].” (Mt. 24:12) Yesu hakumaanisha kwamba wanafunzi wake wengi wangeacha kupendana. Hata hivyo, tunapaswa kuwa makini ili tusiathiriwe na mtazamo wa ulimwengu wa kutopendana. Tukiwa na wazo hilo akilini, acheni tujiulize swali hili muhimu: Je, kuna njia yoyote ya kupima ikiwa upendo wetu kwa ndugu zetu una nguvu au ni dhaifu? Njia moja ya kupima ikiwa upendo wetu una nguvu au ni dhaifu ni kwa kuchunguza jinsi tunavyoshughulikia hali fulani maishani. (2 Kor. 8:8) Mojawapo ya hali hizo inatajwa na mtume Petro, alisema hivi: “Zaidi ya mambo yote, pendaneni sana, kwa sababu upendo hufunika dhambi nyingi.” (1 Pet. 4:8) Hivyo, udhaifu na kutokamilika kwa wengine kunaweza kujaribu upendo wetu. w23.11 10-11 ¶12-13

Jumamosi, Septemba 20

Mpendane.—Yoh. 13:34.

Hatuwezi kutii amri ya Yesu kuhusu kupendana ikiwa tunawaonyesha upendo baadhi ya watu kutanikoni na kuwabagua wengine. Ukweli ni kwamba huenda tukawa na uhusiano wa karibu zaidi na baadhi ya watu kama ilivyokuwa kwa Yesu. (Yoh. 13:23; 20:2) Lakini mtume Petro anatuonyesha kwamba tunapaswa kujitahidi kuonyesha “upendo wa kindugu”—uhusiano mchangamfu kama wa familia—kuwaelekea ndugu na dada zetu wote. (1 Pet. 2:17) Petro alituhimiza ‘tupendane sana kutoka moyoni.’ (1 Pet. 1:22) Katika muktadha huo, kupendana “sana” kunatia ndani kumpenda mtu hata kama ni vigumu kumwonyesha upendo. Namna gani ikiwa ndugu anatukasirisha au anatuumiza kwa njia fulani? Huenda tukashawishiwa kulipiza kisasi badala ya kuonyesha upendo. Ingawa hivyo, Petro alijifunza kutoka kwa Yesu kwamba Mungu hafurahishwi na watu wanaolipiza kisasi. (Yoh. 18:​10, 11) Petro aliandika hivi: “Msilipe ubaya kwa ubaya au matukano kwa matukano. Badala yake, lipeni kwa baraka.” (1 Pet. 3:9) Unapowaonyesha wengine upendo mwingi, utachochewa kuwatendea kwa fadhili na ufikirio. w23.09 28-29 ¶9-11

Jumapili, Septemba 21

Vilevile wanawake wanapaswa . . . wawe wenye kiasi katika mazoea, na waaminifu katika mambo yote.—1 Tim. 3:11

Tunastaajabishwa na jinsi mtoto anavyokua haraka na kuwa mtu mzima. Inaonekana ni kama watoto wanakua tu bila kufanya jitihada yoyote. Hata hivyo, jitihada inahitajika ili kuwa Mkristo mkomavu. (1 Kor. 13:11; Ebr. 6:1) Ili kufikia lengo hilo, tunahitaji kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Pia, tunahitaji roho takatifu ili tusitawishe sifa zinazompendeza Yehova, tuwe na ustadi unaofaa, na tujitayarishe kwa ajili ya majukumu ya wakati ujao. (Met. 1:5) Yehova alimuumba mwanamume na mwanamke. (Mwa. 1:27) Ni wazi kwamba wanaume na wanawake wanatofautiana kimwili, lakini wanatofautiana kwa njia nyingine pia. Kwa mfano, Yehova aliwapatia wanaume na wanawake majukumu hususa, hivyo wanahitaji sifa na ustadi ili waweze kutimiza majukumu yao.—Mwa. 2:18. w23.12 18 ¶1-2

Jumatatu, Septemba 22

Fanyeni wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana.—Mt. 28:19.

Je, Yesu alitaka wengine watumie jina la kibinafsi la Baba yake? Bila shaka. Huenda baadhi ya viongozi wa dini wa siku za Yesu waliamini kwamba jina la Mungu lilikuwa takatifu sana hivi kwamba halikupaswa kutamkwa, lakini Yesu hakuruhusu desturi hizo zisizo za kimaandiko zimzuie kuliheshimu jina la Baba yake. Fikiria wakati ambapo Yesu alimponya mwanamume mwenye roho waovu katika eneo la Wagerasene. Watu katika eneo hilo waliogopa na kumsihi Yesu aondoke, hivyo hakubaki katika eneo hilo. (Marko 5:​16, 17) Lakini bado Yesu alitaka jina la Yehova lijulikane huko. Hivyo, alimwambia mwanamume aliyemponya awaambie watu mambo ambayo Yehova alikuwa amefanya, si mambo ambayo Yesu alikuwa amefanya. (Marko 5:19) Leo pia, anataka tufanye vivyo hivyo, yaani, tuwajulishe watu ulimwenguni pote kuhusu jina la Baba yake! (Mt. 24:14; 28:20) Tunapofanya sehemu yetu, tunamfurahisha Mfalme wetu, Yesu. w24.02 10 ¶10

Jumanne, Septemba 23

Umestahimili kwa ajili ya jina langu.—Ufu. 2:3.

Tuna pendeleo kubwa sana kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova katika siku hizi za mwisho zilizo ngumu. Hali za ulimwengu zinavyozidi kuzorota, Yehova anatupatia familia ya ndugu na dada iliyo na umoja. (Zab. 133:1) Anatusaidia tuwe na maisha ya familia yenye furaha. (Efe. 5:33–6:1) Na anatupatia ufahamu na hekima tunayohitaji ili tuwe na amani ya kweli ya moyoni na akilini. Hata hivyo, ni lazima tujitahidi ili tuendelee kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Kwa nini? Kwa sababu nyakati nyingine tunaweza kukasirishwa na kutokamilika kwa wengine. Pia, tunaweza kuvunjika moyo kwa sababu ya makosa tunayofanya, hasa ikiwa tunarudia makosa yaleyale mara kwa mara. Tunahitaji kuendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu (1) mwabudu mwenzetu anapotukosea, (2) mwenzi wetu wa ndoa anapotuvunja moyo, na (3) tunapovunjika moyo kwa sababu ya makosa yetu. w24.03 14 ¶1-2

Jumatano, Septemba 24

Kwa kadiri ambavyo tumefanya maendeleo, na tuendelee kutembea kwa utaratibu katika mwendo huohuo.—Flp. 3:16.

Mara kwa mara, utasikia kuhusu mambo yaliyoonwa ya ndugu na dada ambao wamepanua utumishi wao mtakatifu. Labda walihudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme au walihamia maeneo yenye uhitaji mkubwa. Ikiwa hali zako zinakuruhusu, hilo ni lengo zuri sana la kujiwekea. Watu wa Yehova wanatafuta fursa mbalimbali za kupanua huduma yao. (Mdo. 16:9) Namna gani ikiwa hali zako za sasa hazikuruhusu kufanya hivyo? Usihisi kwamba wewe ni duni kuliko wale wanaofanya hivyo. (Mt. 10:22) Usisahau kwamba unamfurahisha sana Yehova unapofanya utumishi wake kwa bidii kulingana na uwezo na hali zako. Hiyo ni njia muhimu ya kuendelea kumfuata Yesu baada ya ubatizo.—Zab. 26:1. w24.03 10 ¶11

Alhamisi, Septemba 25

Alitusamehe kwa fadhili makosa yetu yote.—Kol. 2:13.

Baba yetu wa mbinguni anaahidi kwamba atatusamehe ikiwa tutatubu. (Zab. 86:5) Hivyo, ikiwa tumetubu dhambi zetu kikweli, tunaweza kuwa na uhakika kwamba jambo ambalo Yehova ametuahidi ni la kweli, naye ametusamehe. Kumbuka kwamba Yehova ana usawaziko na ni mwenye kunyumbulika. Kamwe hatarajii tufanye mengi zaidi ya yale tunayoweza kutimiza. Anathamini jambo lolote tunalofanya kwa ajili yake maadamu tumempa kilicho bora kulingana na uwezo wetu. Pia, tafakari kuhusu watu katika Biblia ambao walimtumikia Yehova kwa moyo wote. Mfikirie mtume Paulo. Kwa miaka mingi alifanya kazi kwa bidii, akisafiri umbali wa maelfu ya kilomita na kuanzisha makutaniko mengi. Hata hivyo, hali zake zilipobadilika na akashindwa kutimiza mengi zaidi katika kazi yake ya kuhubiri, je, alipoteza kibali cha Yehova? Hapana. Aliendelea kufanya yote aliyoweza, na Yehova alimbariki. (Mdo. 28:​30, 31) Vivyo hivyo, wakati mwingine mambo tunayomtolea Yehova yanaweza kutofautiana. Lakini jambo muhimu kwake ni nia yetu. w24.03 27 ¶7, 9

Ijumaa, Septemba 26

Asubuhi na mapema, [Yesu] akaenda mahali pasipo na watu, naye akaanza kusali.—Marko 1:35.

Kupitia sala alizotoa kwa Yehova, Yesu aliwawekea wanafunzi wake mfano. Katika huduma yake yote, Yesu alisali mara nyingi. Alihitaji kutenga muda wa kusali kwa sababu mara nyingi alikuwa na shughuli nyingi na alizungukwa na watu wengi. (Marko 6:​31, 45, 46) Aliamka asubuhi na mapema ili awe na muda wa kusali akiwa peke yake. Katika pindi moja, alisali usiku kucha kabla ya kufanya uamuzi muhimu. (Luka 6:​12, 13) Na Yesu alisali tena na tena usiku wa kabla ya kifo chake alipokuwa akikazia fikira kutimiza sehemu ngumu zaidi ya mgawo wake duniani. (Mt. 26:​39, 42, 44) Mfano wa Yesu unatufundisha kwamba hata tuwe na shughuli nyingi kadiri gani, tunahitaji kutenga muda wa kusali. Kama Yesu, tunahitaji kupanga muda wa kusali—tunaweza kuamka asubuhi na mapema ili kusali au tunaweza kusali usiku. Tunapofanya hivyo, tunamwonyesha Yehova kwamba tunathamini zawadi hii ya pekee. w23.05 3 ¶4-5

Jumamosi, Septemba 27

Upendo wa Mungu umemiminwa ndani ya mioyo yetu kupitia roho takatifu, ambayo tulipewa.—Rom. 5:5

Ona neno “umemiminwa” ambalo limetumiwa kwenye andiko la leo. Kitabu kimoja cha marejeo kinalinganisha neno “umemiminwa” na kijito cha maji, yaani, kinachotiririka maji mengi. Mfano huo unaonyesha jinsi Yehova anavyowapenda sana watiwa-mafuta! Watiwa-mafuta wanajua kwamba “wanapendwa na Mungu.” (Yuda 1) Mtume Yohana alieleza hisia zao alipoandika hivi: “Oneni upendo ambao Baba ametuonyesha, kwamba tunapaswa kuitwa watoto wa Mungu!” (1 Yoh. 3:1) Je, Yehova anawapenda tu watiwa-mafuta? La, Yehova amethibitisha upendo wake kwetu sisi sote. Ni nini kinachotuhakikishia zaidi kwamba Yehova anatupenda? Fidia—wonyesho mkubwa zaidi wa upendo katika ulimwengu wote!—Yoh. 3:16; Rom. 5:8. w24.01 28 ¶9-10

Jumapili, Septemba 28

Maadui wangu watakimbia siku nitakayoomba msaada. Nina hakika kuhusu jambo hili: Mungu yuko upande wangu.—Zab. 56:9.

Mstari huo unafunua njia iliyomsaidia Daudi kushinda woga wake. Ingawa uhai wake ulikuwa hatarini, alitafakari mambo ambayo Yehova angemfanyia wakati ujao. Daudi alijua kwamba Yehova angemwokoa kwa wakati unaofaa. Isitoshe, Yehova alikuwa ametangaza kwamba Daudi angekuwa mfalme anayefuata wa Israeli. (1 Sam. 16:​1, 13) Daudi alikuwa na uhakika kwamba jambo lolote ambalo Yehova aliahidi lingetimia. Yehova ameahidi atakufanyia nini? Hatutarajii kwamba atukinge kutokana na matatizo yote. Lakini kumbuka kwamba majaribu yoyote ambayo huenda ukakabili katika mfumo huu wa mambo, Yehova atayaondoa katika dunia mpya inayokuja. (Isa. 25:​7-9) Bila shaka Muumba wetu ana nguvu za kufufua wafu, kutuponya, na kuondoa wapinzani wote.—1 Yoh. 4:4. w24.01 6 ¶12-13

Jumatatu, Septemba 29

Mwenye furaha ni mtu ambaye amesamehewa kosa lake, ambaye dhambi yake imefunikwa.—Zab. 32:1.

Fikiria kuhusu wakfu na ubatizo wako. Ulichukua hatua hizo kwa sababu ulitaka kusimama upande wa Yehova. Kumbuka mambo ambayo yalikusaidia kusadiki kwamba umepata kweli. Ulipata ujuzi sahihi kumhusu Yehova na ukaanza kumheshimu na kumpenda akiwa Baba yako wa mbinguni. Ulisitawisha imani na ukachochewa kutubu. Moyo wako ulikuchochea kuacha mazoea yasiyofaa na kuishi kulingana na mapenzi ya Mungu. Ulifarijika ulipotambua kwamba Mungu amekusamehe. (Zab. 32:2) Ulihudhuria mikutano ya Kikristo na ukaanza kuwaambia wengine kuhusu mambo mazuri uliyokuwa unajifunza. Sasa ukiwa Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa, unatembea kwenye barabara ya uzima ukiwa umeazimia kuendelea kutembea katika barabara hiyo. (Mt. 7:​13, 14) Na usimame imara na thabiti katika ujitoaji wako kwa Yehova na sikuzote uendelee kutii amri zake. w23.07 17 ¶14; 19 ¶19

Jumanne, Septemba 30

Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na majaribu hayo ataifanya pia njia ya kutokea ili mweze kuyavumilia.—1 Kor. 10:13.

Ukitafakari sala uliyotoa ulipojiweka wakfu kwa Yehova, utapata nguvu za kushinda kishawishi chochote. Kwa mfano, je, utamchezea kimapenzi mwenzi wa ndoa wa mtu mwingine? Bila shaka hapana! Tayari ulishamwahidi Yehova kwamba hutafanya jambo kama hilo. Ikiwa hutaruhusu tamaa mbaya zisitawi, hutahitaji kupambana baadaye ili kuzing’oa. ‘Utajiepusha’ na “kijia cha waovu.” (Met. 4:​14, 15) Ukikumbuka azimio la Yesu la kumpendeza Baba yake, utakataa haraka na kwa uthabiti jambo lolote ambalo unajua halitampendeza Mungu ambaye umejiweka wakfu kwake. (Mt. 4:10; Yoh. 8:29). Ukweli ni kwamba majaribu na vishawishi vinakupa nafasi ya kuonyesha kwamba umeazimia ‘kuendelea kumfuata’ Yesu. Unapofanya hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakusaidia. w24.03 9-10 ¶8-10

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki