Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jitahidi Kuboresha Paradiso ya Kiroho
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Julai 15
    • 1, 2. Maneno “kiti cha miguu” yanaweza kumaanisha nini katika Maandiko ya Kiebrania?

      YEHOVA MUNGU alitangaza hivi: “Mbingu ni kiti changu cha ufalme, na dunia ni kiti cha miguu yangu.” (Isa. 66:1) Pia alisema hivi kuhusu “kiti cha miguu” yake: “Nitapatukuza mahali pangu pa miguu.” (Isa. 60:13) Anafanya hivyo jinsi gani? Na jambo hilo linamaanisha nini kwetu sisi tunaoishi kwenye “kiti cha miguu” cha Mungu?

      2 Maneno “kiti cha miguu,” yanatumika pia kwa njia ya mfano katika Maandiko ya Kiebrania kufafanua hekalu lililotumiwa na Waisraeli. (1 Nya. 28:2; Zab. 132:7) Hekalu lilikuwa kituo cha ibada ya kweli duniani. Kwa sababu hiyo, lilikuwa lenye kupendeza sana machoni pa Yehova na lilipatukuza mahali pake pa miguu.

      3. Hekalu kubwa la kiroho la Mungu ni nini, na lilianza lini?

      3 Leo, kitovu cha ibada ya kweli si hekalu halisi. Badala yake, kuna hekalu la kiroho linalomtukuza Yehova kuliko jengo lolote lile. Hekalu hilo ni mpango unaowawezesha wanadamu kupatanishwa na Mungu kwa msingi wa ukuhani na dhabihu ya Yesu Kristo. Mpango huo ulianza mwaka wa 29 W.K. Yesu alipobatizwa na kutiwa mafuta kuwa Kuhani Mkuu katika hekalu kubwa la kiroho la Yehova.—Ebr. 9:11, 12.

      4, 5. (a) Zaburi ya 99 inafafanuaje tamaa kubwa ya waabudu wa kweli wa Yehova? (b) Tunapaswa kujiuliza swali gani?

      4 Tunamshukuru sana Yehova kwa mpango wa hekalu la kiroho. Tunamsifu kwa kuwajulisha watu jina lake na tunamtukuza kwa sababu ya zawadi bora sana ya fidia. Inasisimua sana kuona Wakristo wa kweli zaidi ya milioni nane wakimtukuza Yehova! Tofauti na baadhi ya wanadini wanaofikiri kimakosa kwamba watamsifu Mungu baada ya kuondoka duniani na kwenda mbinguni, Mashahidi wa Yehova wanatambua kwamba wanahitaji kumsifu Mungu sasa, wakiwa hapa hapa duniani.

      5 Tunafuata mfano wa watumishi waaminifu wa Yehova wanaotajwa kwenye Zaburi 99:1-3, 5-7. (Soma.) Kama zaburi hiyo inavyoonyesha, Musa, Haruni, na Samweli waliunga mkono kabisa mpango wa ibada ya kweli katika siku zao. Leo, watiwa-mafuta wanatumikia kwa uaminifu katika ua wa hekalu la kiroho duniani kabla ya kwenda mbinguni ili kutumikia wakiwa makuhani pamoja na Yesu. Mamilioni ya “kondoo wengine” wanawaunga mkono kwa ushikamanifu. (Yoh. 10:16) Ingawa wana matumaini tofauti, vikundi vyote viwili vinamwabudu Yehova kwa umoja katika kiti cha miguu cha Mungu. Hata hivyo, kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza hivi, ‘Je, ninaunga mkono kabisa mpango wa Yehova wa ibada safi?’

  • Jitahidi Kuboresha Paradiso ya Kiroho
    Mnara wa Mlinzi—2015 | Julai 15
    • 7 Kufikia mwaka wa 1919, wale waliokubaliwa na Yehova na kutumikia katika hekalu la kiroho walitambuliwa waziwazi. Walikuwa wamesafishwa kiroho ili wamtumikie Mungu kwa njia inayokubalika zaidi. (Isa. 4:2, 3; Mal. 3:1-4) Maono ambayo Paulo aliona karne nyingi zilizopita yalianza kutimia kwa kadiri fulani.

      8, 9. “Paradiso” ambayo Paulo aliiona katika maono inaweza kumaanisha nini?

      8 Maono ya Paulo yanapatikana kwenye 2 Wakorintho 12:1-4. (Soma.) Maono ambayo Paulo aliona yanaelezwa kuwa ni ufunuo. Yalihusu tukio la wakati ujao, si jambo lililokuwepo katika siku za Paulo. Paulo aliona “paradiso” gani ‘aliponyakuliwa mpaka kwenye mbingu ya tatu’? Paradiso ambayo Paulo aliizungumzia ingekuwa na utimizo halisi, wa kiroho, na wa kimbingu, na wote ungetimizwa katika kipindi kimoja wakati ujao. Paradiso hiyo inaweza kumaanisha Paradiso halisi tunayotarajia hapa duniani. (Luka 23:43) Pia, inaweza kumaanisha paradiso ya kiroho ambayo tutaifurahia kikamili katika ulimwengu mpya. Isitoshe, inaweza kumaanisha hali nzuri katika “paradiso ya Mungu” mbinguni.—Ufu. 2:7.

      9 Hata hivyo, kwa nini Paulo alisema kwamba alisikia “maneno yasiyoweza kutamkwa ambayo si halali mtu kuyasema”? Huo haukuwa wakati wa kueleza kwa kina mambo ya ajabu aliyokuwa ameona katika maono hayo. Lakini sasa tunaweza kueleza baraka ambazo watu wa Mungu wanazifurahia!

      10. Je, “paradiso ya kiroho” ni sawa na “hekalu la kiroho”? Eleza.

      10 Maneno “paradiso ya kiroho” yamekuwa msemo wa kawaida wa kitheokrasi. Msemo huo unafafanua mazingira au hali ya pekee ya kiroho inayotuwezesha kufurahia amani pamoja na Mungu na waumini wenzetu. Hilo halimaanishi kwamba “paradiso ya kiroho” ni sawa na “hekalu la kiroho.” Hekalu la kiroho ni mpango wa Mungu kwa ajili ya ibada ya kweli. Paradiso ya kiroho ni hali inayowatambulisha watu wenye kibali cha Mungu ambao wanatumikia katika hekalu lake la kiroho.—Mal. 3:18.

      11. Yehova ameturuhusu kufanya jambo gani la pekee?

      11 Inasisimua sana kujua kwamba tangu mwaka wa 1919, Yehova amewaruhusu wanadamu wasio wakamilifu washirikiane naye kusitawisha, kuimarisha, na kupanua paradiso ya kiroho duniani! Je, unashiriki katika kazi hiyo yenye kustaajabisha? Je, unajitahidi kufanya kazi na Yehova katika kutukuza ‘kiti chake cha miguu’?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki