Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Majuma Sabini
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
    • “Atakatiliwa mbali” katika nusu ya juma hilo. Gabrieli aliendelea kumwambia Danieli hivi: “Baada ya yale majuma 62 Masihi atakatiliwa mbali, bila kuwa na chochote kwa ajili yake.” (Da 9:26) Ilikuwa muda fulani baada ya mwisho wa ‘majuma 7 kuongezea 62,’ kwa kweli karibu miaka mitatu na nusu baadaye, ndipo Kristo alipokatiliwa mbali katika kifo juu ya mti wa mateso, akatoa kila kitu alichokuwa nacho, awe fidia kwa ajili ya jamii ya wanadamu. (Isa 53:8) Uthibitisho waonyesha kwamba nusu ya kwanza ya “juma” hilo ilitumiwa na Yesu katika huduma. Katika pindi moja, yawezekana ni katika vuli ya 32 W.K., alitoa mfano, kwa wazi akiongea juu ya taifa la Kiyahudi kana kwamba ni mtini (linganisha Mt 17:15-20; 21:18, 19, 43) ambao haukuzaa matunda yoyote kwa “miaka mitatu.” Mtunza-mizabibu akamwambia mwenye shamba la mizabibu: “Bwana, uache mwaka huu pia, mpaka niupalilie na kuweka mbolea; na ndipo ukizaa matunda wakati ujao, basi ni vema; lakini ikiwa sivyo, utaukata.” (Lu 13:6-9) Huenda hapa yeye alirejelea kipindi cha huduma yake mwenyewe katika taifa hilo lisiloitikia, huduma ambayo kufikia hatua hiyo ilikuwa imeendelea kwa karibu miaka mitatu nayo ingeendelea iingie katika mwaka wa nne.

  • Majuma Sabini
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
    • Maangamizi kwenye jiji hilo na mahali patakatifu. Iilikuwa baada ya “majuma” 70, lakini likiwa tokeo la moja kwa moja la Wayahudi kumkataa Kristo wakati wa lile “juma” la 70, matukio ya sehemu za mwisho za Danieli 9:26 na 27 yalitimizwa. Maandishi ya historia yanaonyesha kwamba Tito mwana wa Maliki Vepasiani wa Roma alikuwa ndiye kiongozi wa vikosi vya Roma vilivyokuja dhidi ya Yerusalemu. Kwa kweli majeshi hayo yaliingia ndani ya Yerusalemu na hekalu lenyewe, kama mafuriko, na kuliangamiza jiji hilo na hekalu lake. Kusimama huku kwa majeshi ya kipagani katika mahali patakatifu kuliyafanya yawe “chukizo.” (Mt 24:15) Jitihada zote zilizofanywa kabla ya mwisho wa Yerusalemu ili kunyamazisha hali hiyo zilishindwa kwa sababu amri ya Mungu ilikuwa ni hii: “Kilichoamuliwa ni ukiwa,” na “mpaka maangamizi, kitu kile kilichoamuliwa kitamwagika pia juu ya yule anayekaa ukiwa.”

      Maoni ya Kiyahudi. Maandishi-matini ya Masora, yenye mfumo wake wa nukta za irabu, yalitayarishwa katika sehemu ya mwisho ya nusu ya milenia ya kwanza W.K. Ni wazi kwa sababu ya kumkataa Yesu Kristo kuwa Masihi, Wamasora walitia alama ya mkazo kwenye maandishi-matini ya Kiebrania kwenye Daniel 9:25 wakiweka ʼath·nach′, au “kituo cha kikomo,” baada ya “majuma saba,” kwa jambo hilo wakagawanya hilo na yale “majuma 62”; katika njia hiyo yale majuma 62 ya unabii, yaani, miaka 434, yanaonekana kuhusu wakati wa kujenga upya Yerusalemu la kale. Tafsiri ya Isaac Leeser inasema hivi: “Basi ujue na kuelewa, kwamba tangu kutoka kwa neno la kurudisha na kujenga Yerusalemu hadi mtiwa-mafuta aliye mkuu kutakuwa majuma saba: [kituo cha kikomo hapa kinawakilishwa na nukta mbili] na wakati wa majuma sitini na mawili ndipo litakapojengwa tena likiwa na barabara na mahandaki (kulizunguka), naam katika mikazo ya nyakati hizo.” Tafsiri ya Chama cha Uchapishaji cha Kiyahudi cha Marekani yasema vivyo hivyo: “kutakuwa majuma saba; na kwa majuma makumi sita na mawili, litajengwa tena.” Katika tafsiri hizi mbili (katika Kiingereza) maneno “wakati” na “kwa,” yanaonekana katika tafsiri ya Kiingereza, bila shaka ili yaunge mkono fasiri ya watafsiri hao.

      Profesa E. B. Pusey, katika kielezi-chini kimoja katika mojawapo mihadhara yake iliyotolewa kwenye Chuo Kikuu cha Oxford, anatoa maelezo haya juu ya utiaji alama za mkazo za Wamasora: “Wayahudi walitia kituo kikuu cha mstari huo chini ya שׁבעה [saba], wakikusudia kutenganisha hizo namba mbili, 7 na 62. Lazima wawe walifanya hivyo kwa udanganyifu, למען המינים (kama Rashi [Rabi maarufu wa Kiyahudi wa karne ya 11 na ya 12 W.K.] anavyosema katika kukataa mafafanuzi halisi yaliyowafaa Wakristo) ‘kwa sababu ya wazushi,’ yaani, Wakristo. Kwa kishazi hicho cha mwisho, kugawanywa hivyo, ingeweza kumaanisha tu, ‘na wakati wa majuma makumi sita na mawili barabara na ukuta vitarudishwa na kujengwa,’ yaani, kwamba Yerusalemu lingechukua miaka 434 kujengwa upya, jambo ambalo lingekuwa ni upuuzi.”—Daniel the Prophet, 1885, ukur. 190.

      Kwa habari ya Danieli 9:26 (Le), ambalo lasema hivi, kwa sehemu, “Na baada ya yale majuma-sitini na mwili ndipo mtiwa-mafuta atakapokatiliwa mbali bila kuwa na mwandamizi mwenye kumfuata,” Wafafanuzi wa Kiyahudi hutumia hayo majuma 62 kufikia kipindi cha enzi za Wamakabayo, na usemi “mtiwa-mafuta” kumhusu Mfalme Agripa wa 2, aliyeishi wakati wa kuangamizwa kwa Yerusalemu, 70 W.K. Au wengine husema huyo alikuwa kuhani mkuu, Oniasi, aliyepinduliwa na Antioko Epifane katika 175 K.W.K Matumizi yao ya unabii huo kuhusu mojawapo kati ya wanaume hao yangekuwa yenye kuukosesha umuhimu au maana yoyote iliyo halisi, na tofauti hiyo katika kukadiria tarehe ingefanya yale majuma 62 yawe unabii usio na wakati ulio sahihi hata kidogo.—Ona Soncino Books of the Bible (ufafanuzi juu ya Da 9:25, 26), kilichofanyiwa uhariri na A. Cohen, London, 1951.

      Katika jitihada ya kutetea maoni yao, wasomi hao wa Kiyahudi husema kwamba yale “majuma saba” si 7 mara 7, au miaka 49, bali ni miaka 70; na huku wanahesabu yale majuma 62 kuwa 7 mara miaka 62. Wanadai hilo lilirejelea kile kipindi cha uhamisho wa Babiloni. Wanamfanya Koreshi au Zerubabeli au Kuhani Mkuu Yeshua awe “mtiwa-mafuta” katika mstari huu (Da 9:25), na huku yule “mtiwa-mafuta” katika Danieli 9:26 akiwa mtu mwingine.

      Inaweza kuangaliwa, kuhusiana na hilo, kwamba tafsiri ya Septuajinti, iliyofanywa na wasomi wa Kiyahudi katika karne tatu za kwanza K.W.K, yasema hivi, kwenye Danieli 9:25, “Tangu kutolewa kwa amri ya kujibu na kujengwa kwa Yerusalemu hadi Kristo aliye mkuu kutakuwa majuma saba, na majuma sitini na mawili: kisha ule wakati utarudi, na barabara itajengwa, na ukuta.” (LXX, Bagster) Kwa sehemu, Septuagint ya Thompson inasema hivi: “majuma saba, na majuma sitini na mawili. Hakika wao watarudi na barabara itajengwa na ukuta.”

      Tafsiri zilizo nyingi za Kiingereza hapa hazifuati alama za maandishi za Wamasora. Ama zina alama ya mkato baada ya usemi “majuma saba” au katika matumizi ya maneno zinaonyesha kwamba yale majuma 62 yanafuata yale 7 yakiwa sehemu ya yale 70, nazo hazionyeshi kwamba yale majuma 62 yanahusu kile kipindi cha kujenga upya Yerusalemu. (Linganisha Da 9:25 katika UV, AT, Dy, NW, Ro, Yg.) Taarifa ya mhariri ya James Strong katika Commentary on the Holy Scriptures cha Lange (Da 9:25, klz-chn, ukur. 198) yasema hivi: “Hoja pekee ya tafsiri hii, ambayo inatenganisha vile vipindi viwili vya majuma saba na majuma sitini na mawili, ikionyesha hayo ya kwanza kuwa ndio wakati wa kuwasili kwa Mkuu aliye Mtiwa-Mafuta, na hayo ya mwisho kuwa ndio upeo wa wakati wa kujenga upya, ni alama za maandishi za Wamasora, ambazo zinatia ile alama ya nukta katikati yake. . . . na tafsiri inayohusika inatia ndani muundo usiofaa wa sehemu ya pili, bila kihusishi. Kwa hiyo, ni afadhali zaidi, na ni sahili zaidi, kushikilia chapa ya Authorized Version, inayofuata tafsiri nyinginezo zote za kale.”—Kimetafsiriwa na kufanyiwa uhariri (Kiingereza) na P. Schaff, 1976.

      Maoni mengine mengi, mengine yakiwa ni ya Kimasihi na mengine yasiyokuwa ya Kimasihi, yametolewa kuhusu ni nini maana ya unabii huo. Mengine hujaribu kubadili utaratibu wa vipindi hivyo vya wakati wa unabii huo, huku mengine yakiyafanya yaende sambamba au kukanusha kwamba yana wakati halisi wa utimizo. Pia, kumekuwa na jitihada nyingi za kufanya matukio hayo yaliyotajwa yafae kipindi cha Wamakabayo au hata wakati wa kumalizia wa mwisho. Lakini wale wanaotokeza maoni hayo wanajiingiza katika utata mkubwa, na jitihada zao za kujinasua huwaingiza katika upumbavu au ukanushaji wa moja kwa moja kwamba unabii huo umeongozwa kwa roho au ni wa kweli. Kuhusu maoni hayo ya mwisho hasa, ambayo hutokeza matatizo mengi zaidi kuliko yale ambayo husuluhishwa nayo, msomi huyo aliyetangulia kutajwa, E. B. Pusey, anaeleza hivi: “Hayo ndiyo yaliyokuwa matatizo yasiyowezekana kusuluhishwa na ukosaji imani; ilibidi huo ujifanyie suluhisho, jambo ambalo, kufikia hapa, ndilo lililokuwa rahisi zaidi; kwa maana hapana lisilowezekana kuaminiwa na ukosefu wa imani, isipokuwa yale anayofunua Mungu.”—Ukur. 206.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki