-
Yehova Ni Mwenye Kukubali Sababu!Mnara wa Mlinzi—1994 | Agosti 1
-
-
Kukubali Sababu ni Ishara ya Hekima ya Kimungu
6. Ni zipi baadhi ya maana halisi na maana nyingine za neno la Kigiriki ambalo Yakobo alitumia akifafanua hekima ya kimungu?
6 Mwanafunzi Yakobo alitumia neno lenye kupendeza kufafanua hekima ya Mungu huyo anayejipatanisha na hali sana. Yeye aliandika: ‘Hekima ya kutoka juu ni yenye kukubali sababu.’ (Yakobo 3:17, NW) Ni vigumu kutafsiri neno la Kigiriki (e·pi·ei·kesʹ) alilotumia hapa. Watafsiri wametumia maneno kama “upole,” “-enye huruma,” “-enye kujizuia,” na “-enye kufikiria hali.” New World Translation yaitafsiri “-enye kukubali sababu,” kukiwa na kielezi-chini kinachoonyesha kwamba maana halisi ni “kukubali kupatana na hali.”a Neno hilo pia latoa maana ya kutosisitiza sana kila kijambo kidogo cha sheria, si kuwa mshurutishaji au mgumu. Msomi William Barclay aeleza hivi katika New Testament Words: “Jambo la msingi kuhusu epieikeia ni kwamba latokana na Mungu. Ikiwa Mungu angesisitiza haki zake bila kuondoleka, ikiwa Mungu angetumia viwango vigumu vya sheria pekee, tungekuwa wapi? Mungu ndiye kielelezo kikuu cha mtu ambaye ni epieikēs na anayeshughulika na wengine kwa epieikeia.”
7. Yehova alionyeshaje kukubali sababu katika bustani ya Edeni?
7 Fikiria wakati wanadamu walipoasi enzi kuu ya Yehova. Ingekuwa rahisi kama nini kwa Mungu kuua waasi hawa watatu wasio na shukrani—Adamu, Hawa, na Shetani! Angejiondolea maumivu mengi kama nini ya moyo! Na ni nani angebisha kwamba hakuwa na haki ya kutekeleza haki kikamili? Hata hivyo, Yehova hajafanya tengenezo lake lililo kama gari liwe katika kiwango fulani cha haki ambacho ni kigumu na kisichoweza kupatana na hali. Kwa hiyo gari hilo halikuendelea kusonga mbele na kuharibu familia ya wanadamu na matazamio yote ya wakati ujao wenye furaha kwa ajili ya wanadamu. Kinyume cha hilo, Yehova aliendesha gari lake kwa wepesi kama umeme. Mara tu baada ya uasi, Yehova Mungu alitaja kusudi la muda mrefu lililoandaa rehema na tumaini kwa wazao wote wa Adamu.—Mwanzo 3:15.
8. (a) Maoni ya Jumuiya ya Wakristo juu ya kukubali sababu yatofautianaje na maoni ya kweli ya Yehova ya kukubali sababu? (b) Kwa nini twaweza kusema kwamba kukubali sababu kwa Yehova hakumaanishi kwamba anaweza kuridhiana kanuni za kimungu?
8 Hata hivyo, jambo la kwamba Yehova akubali sababu halimaanishi kwamba angeweza kuvunja kanuni za kimungu. Makanisa ya leo ya Jumuiya ya Wakristo huenda yakafikiri kwamba yanakuwa yenye kukubali sababu yanapopuuza ukosefu wa adili ili tu yapendwe na makundi yayo yaliyopotea. (Linganisha 2 Timotheo 4:3.) Yehova havunji kamwe sheria zake, wala haridhiani kanuni zake. Badala ya hivyo, yeye huonyesha utayari wake wa kukubali kupatana na hali na kujipatanisha na hali, ili kanuni hizo zitumiwe kwa haki na kwa rehema. Nyakati zote yeye hufikiria kusawazisha haki na uwezo atekelezao pamoja na upendo na hekima yenye kukubali sababu. Ebu tufikirie njia tatu ambazo Yehova huonyesha kukubali sababu.
“Tayari Kusamehe”
9, 10. (a) Kuwa “tayari kusamehe” kwahusianaje na kukubali sababu? (b) Daudi alinufaikaje na utayari wa Yehova wa kusamehe, na kwa nini?
9 Daudi aliandika hivi: “Kwa maana Wewe, Bwana, U mwema, umekuwa tayari kusamehe; na mwingi wa fadhili, kwa watu wote wakuitao.” (Zaburi 86:5) Maandiko ya Kiebrania yalipotafsiriwa katika Kigiriki, neno la “tayari kusamehe” lilifasiriwa kuwa e·pi·ei·kesʹ, au “kukubali sababu.” Kwa kweli, kuwa tayari kusamehe na kuonyesha rehema labda ndiko njia kuu ya kuonyesha kukubali sababu.
10 Daudi mwenyewe alijua vizuri jinsi Yehova alivyo mwenye kukubali sababu kwa habari hiyo. Daudi alipofanya uzinzi na Bath-sheba na kupanga mumewe auawe, wote wawili yeye na Bath-sheba walistahili kuhukumiwa kifo. (Kumbukumbu la Torati 22:22; 2 Samweli 11:2-27) Kama ni mahakimu wa kibinadamu wasiobadilikana wangalishughulikia kesi hiyo, huenda hao wote wangalipoteza uhai wao. Lakini Yehova alionyesha kukubali sababu (e·pi·ei·kesʹ), ambayo, kama itajwavyo na Vine’s Expository Dictionary of Biblical Words, “yaonyesha ufikirio unaoona ‘mambo hakika ya kesi kwa huruma na kwa kukubali sababu.’” Mambo yaliyokuwa na uvutano kwa uamuzi wa Yehova wenye rehema yaelekea sana yalitia ndani toba ya unyoofu ya watenda-dhambi hao na rehema ambayo Daudi mwenyewe alikuwa ameonyesha kwa niaba ya wengine. (1 Samweli 24:4-6; 25:32-35; 26:7-11; Mathayo 5:7; Yakobo 2:13) Hata hivyo, kwa kupatana na maelezo ya Yehova juu yake mwenyewe katika Kutoka 34:4-7, kulikuwa ni kukubali sababu kwamba Yehova alimrekebisha Daudi. Alimtuma nabii Nathani kwa Daudi akiwa na ujumbe mzito, akimkazia Daudi kwamba alikuwa amepuuza neno la Yehova. Daudi alitubu na kwa hiyo hakufa kwa dhambi zake.—2 Samweli 12:1-14.
-
-
Yehova Ni Mwenye Kukubali Sababu!Mnara wa Mlinzi—1994 | Agosti 1
-
-
a Kule nyuma katika 1769, mtunga-kamusi John Parkhurst alifasili neno hilo kuwa “-enye kukubali kupatana na hali, -enye mwelekeo wa kukubali kupatana na hali, -tulivu, -pole, -enye saburi.” Wasomi wengine vilevile wamelifasili kuwa “-enye kukubali kupatana na hali.”
-