Wakati Ndoto za Amani Zilipozimwa
NI WATU wachache sana waliotazamia 1914 uwe mwaka ulio tofauti. Kwa kweli, wakati ujao ulionekana kuwa wenye uangavu usio wa kawaida kwa watu katika miaka iliyotangulia. Sayansi ilikuwa imefanya maendeleo dhidi ya ugonjwa. Na vita? Kama vile gazeti la Vatikani L’Osservatore Romano lilivyosema Februari 1991, kabla ya 1914 watu “waliamini kwamba vita vilikuwa vimeondoshwa kabisa hata kudidimia katika kumbukumbu la kihistoria” na kwamba mwanadamu alikuwa sasa anaishi katika “kizazi ambacho mataifa na serikali zilizoelimika zilikuwa zimepiga vita marufuku.”
Hata hivyo, 1914 na miaka iliyofuata ilikuwa na visa vya ukatili kwa ainabinadamu yenye kustarehe. Kwanza kulikuwa na vile viitwavyo Vita Vikuu vya 1914-18 ambavyo vilizima ndoto za amani. Hata L’Osservatore Romano iliviita “machinjo ya kwanza makubwa ya historia ya kisasa, yenye kutiwa alama, miongoni mwa vitu vingine, na mavumbuzi ya kiufundi ambayo wanasayansi mashuhuri wa vizazi vilivyopita waliamini kuwa vilitolewa kwa miradi ya amani.” Vita hivyo vilifanya sayansi idharauliwe kuwa njia ya kupata amani; badala yake, sayansi ilipatia vita uwezo wavyo usio na kifani wa uchinjaji wa ujumla.
Na machinjo ya vita yalipoisha, uchinjaji mwingine ukaanza. Homa ya Hispania ya 1918-19 iliua watu zaidi ya milioni 20—kiasi kikubwa zaidi ya idadi yenye kuogopesha ya waliokufa katika Vita Vikuu vyenyewe. Hatua kali zilichukuliwa; kueneza ugonjwa huo kulitangazwa kuwa uhalifu katika nchi fulani. Polisi hata walishika watu kwa sababu ya kupiga chafya hadharani! Lakini bila matokeo. Kama vile tufani, ugonjwa huo uliendelea ukifagia bila kuzuilika mpaka ukafifia wenyewe. Miji mizima-mizima ilifutwa fyu na ugonjwa huo. Maiti zilikuwa zimejaa vyumba vya kuwekea maiti vya mijini.
Wakati wa mabadiliko ulioanzia 1914 uliacha mwanadamu akihangaika. Matazamio bandia yake ya kushinda vita na magonjwa, ndoto zake za amani ya ulimwengu yenye kufanyizwa kwa hekima ya kibinadamu, zilivunjwavunjwa kwa kusikitisha. Na mambo yalipozidi kuharibika, na vile Vita Vikuu vya ulimwengu vya 1 kushushwa na mwandamizi wavyo, yaani, Vita vya Ulimwengu vya 2, huku magonjwa, umaskini, njaa, na uvunjaji sheria ukiendelea kuzidi kuongezeka na kuenea katika sehemu kubwa za ulimwengu, wanahistoria walianza kutambua 1914 kuwa mwaka uliotiwa alama katika historia ya kibinadamu.
Lakini tofauti na ulimwengu wote, wale Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa (kama vile Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo) walitazamia 1914 kuwa mwaka wenye maana sana. Na miaka iliyofuata tangu wakati huo, Mashahidi wa Yehova hawajashangazwa kuona ulimwengu ukizorota na kuwa katika hali isiyotumainika ulimo sasa. Unabii wa Biblia umewasaidia watazamie matukio hayo na hata kuona wakati mtukufu wa tumaini lililoko mbele. Hilo lawezekanaje? Wakati mwingine Mashahidi wa Yehova wakutembeleapo, labda utapenda kuwauliza kuhusu hilo. Au unaweza kuandikia watangazaji wa gazeti hili.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 32]
Imechorwa tena kutoka mchoro wa Franklin Booth