Je, Wewe Ni Mzazi Mwenye Uchangamfu?
JE, WEWE wawapenda watoto wako? Je, wajivunia kuwa nao? Je, wahisi kwamba kila mmoja ni mtu maalumu, asiye na kifani, asiyeweza kubadilishwa kwa mwingine? Wazazi walio wengi huhisi hivyo. Lakini je, wewe huambia watoto wako kwamba ndivyo uhisivyo? Je, wewe huwasifu kihususa wafanyapo jambo fulani vema? Na je, wewe huonyesha uchangamfu kwa njia nyinginezo—kwa mchezo mwanana, mguso wenye uhakikishio, makumbatio yenye upendo?
“Lakini hiyo si asili yangu kamwe,” huenda wengine wakakataa. “Mimi sifungulii wazi hisia zangu kadiri hiyo.” Ni kweli, si kila mtu mwenye asili ya kuonyesha hisia. Hata hivyo, kuwaonyesha watoto wako uchangamfu huenda kukawa kwa maana kuliko ulivyopata kutambua.
Kikundi cha wanasayansi hivi majuzi kilifuatia uchunguzi mmoja uliofanywa 1951 kwa watoto 400 wa shule ya watoto wadogo sana. Miongoni mwa wale wanaume na wanawake 94 walioweza kuwafuatilia, waligundua vigezo fulani vya kufichua wazi. Kulingana na The New York Times, watoto wale waliokuwa na wazazi wachangamfu na wenye shauku walielekea kufaulu zaidi katika maisha yao ya utu mzima. Kwa msingi walikuwa na ndoa zenye mafanikio, walilea watoto, wakafurahia kazi yao, na kuendeleza urafiki wa karibu. Dakt. Carol Franz, aliyeongoza uchunguzi huo, aliambia gazeti hilo kwamba wao ‘walionyesha hali-njema ya kisaikolojia, bidii na kuridhika na wao wenyewe na maisha zao.’
Kwa kinyume, Franz alikuta kwamba “wale wenye wazazi baridi, wenye kuwakataa walitatizika zaidi katika maisha ya baadaye pande zote—kazini, katika rekebisho la kijamii, na katika hali-njema ya kisaikolojia.” Kwa kweli, uchunguzi huo ulidokeza kwamba kukosa uchangamfu kwa wazazi huenda hata kukadhuru watoto zaidi hatimaye kuliko kutalikiana kwa wazazi, uraibu wa alkoholi, au umaskini.
Hili halipasi kushangaza wanafunzi wa Biblia wenye moyo mweupe. Wao wajua vema jinsi Yesu alivyotendea watoto. Aliwathamini, akawavuta kwake mwenyewe, na kuacha shauku yake kwao ionekane. (Marko 10:13-16; Luka 9:46-48; 18:15-17) Bila shaka, yeye alikuwa akiiga tu Baba yake wa kimbingu katika jambo hili—Yeye awaye Baba kwa mvulana asiye na baba. (Zaburi 68:5) Yehova ndiye Mzazi mkamilifu; la kufurahisha kwa wale wampendao ni kwamba yeye aweza kujazia ukosefu wowote ulio katika wazazi wasiokamilika wa kibinadamu.—2 Wakorintho 6:18.