Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g96 4/8 uku. 20
  • Migawo ya Utumishi wa Hekalu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Migawo ya Utumishi wa Hekalu
  • Amkeni!—1996
Amkeni!—1996
g96 4/8 uku. 20

Migawo ya Utumishi wa Hekalu

Migawo ya Utumishi wa Hekalu Kwa Ajili Ya Makuhani Katika Israeli Iliamuliwaje?

Kati ya ile migawanyo au vikundi 24, ya makuhani iliyoanzishwa na Mfalme Daudi, 16 ilifanyizwa kutokana na nyumba ya Eleazari na 8 kutokana na nyumba ya Ithamari. (1 Mambo ya Nyakati 24:1-19) Hata hivyo, angalau mwanzoni, ni makuhani kutoka kwa migawanyo minne tu waliorudi kutoka ule uhamisho wa Babiloni. (Ezra 2:36-39) Wengine hudokeza kwamba, ili kuuendeleza mpango wa kitengenezo wa awali, familia nne zilizokuwa zikirudi ziligawanywa hivi kwamba zikawa tena vikundi 24. Alfred Edersheim, katika kitabu The Temple (1874, ukurasa 63), adokeza kwamba hilo lilitimizwa kwa kila familia kupiga kura tano kwa ajili ya wale ambao hawakuwa wamerudi, kwa njia hiyo wakifanyiza kutokana na makundi yao vikundi vingine 20 vya ziada ambavyo walivipa yale majina ya awali. Baba ya Yohana Mbatizaji Zekaria alikuwa kuhani katika mgawanyo wa nane, ule wa Abija. Hata hivyo, ikiwa mtazamo ulioko juu ni kweli, huenda asiwe alikuwa mzao wa Abija—huenda alikuwa tu wa mgawanyo uliokuwa na jina lake. (1 Mambo ya Nyakati 24:10; Luka 1:5) Kukosekana kwa habari kamili hakuruhusu kufikia mikataa iliyo thabiti katika hoja hizi.

Katika utumishi wa hekalu makuhani walipangwa chini ya maofisa kadhaa. Kura zilipigwa ili kutoa migawo fulani. Kila mmoja wa ile migawanyo 24 ulitoa utumishi kwa juma moja, ukiwa kwenye kazi yao uliyogawiwa mara mbili kwa mwaka. Kwa uhakika ukuhani wote ulitoa utumishi kwenye sherehe mbalimbali wakati maelfu ya dhabihu yalipotolewa na watu, kama walivyofanya wakati wa kuwekwa wakfu kwa hekalu. (1 Mambo ya Nyakati 24:1-18, 31; 2 Mambo ya Nyakati 5:11; linganisha 2 Mambo ya Nyakati 29:31-35; 30:23-25; 35:10-19.) Kuhani aliweza kutoa utumishi nyakati nyinginezo maadamu hakujiingiza katika utumishi uliogawiwa makuhani waliokuwa kazini. Kulingana na desturi za kirabi, katika wakati wa maisha ya kidunia ya Yesu, makuhani walikuwa wengi, hivi kwamba ule utumishi wa juma moja uligawanywa hata zaidi kati ya familia mbalimbali zilizofanyiza mgawanyo fulani, kila familia ilikuwa ikitoa utumishi kwa siku moja au zaidi kulingana na idadi yao.

Huenda jambo lililoonwa kuwa lenye kuheshimika zaidi kati ya utumishi mbalimbali wa kila siku ni kule kufukiza uvumba katika madhabahu ya dhahabu. Hili lilifanywa baada ya dhabihu kutolewa. Wakati wa kufukiza uvumba, watu wangekuwa wamekusanyika nje ya patakatifu wakisali. Pokeo la kirabi husema kwamba kura zilipigwa kwa ajili ya utumishi huu lakini mmoja ambaye alikuwa ametumika mbeleni hakuruhusiwa kushiriki isipokuwa wote waliokuwako walikuwa wametoa utumishi wao mbeleni. (The Temple, kurasa 135, 137, 138) Ikiwa hivyo ndivyo ilivyokuwa, kwa kawaida kuhani angekuwa na pendeleo hilo mara moja tu maishani. Zekaria alikuwa akitoa utumishi huu wakati malaika Gabrieli alipomtokea na kutangaza kwamba Zekaria na mkewe Elisabeti wangepata mwana. Zekaria alipotoka nje ya patakatifu, umati uliokuwa umekusanyika hapo uliweza kufahamu kutokana na sura yake na kutoweza kwake kuongea kwamba Zekaria alikuwa ameona kitu fulani kipitacho nguvu za kibinadamu katika patakatifu; hivyo tukio hilo likajulikana na kila mtu.—Luka 1:8-23.

Yaonekana, kila siku ya Sabato, makuhani walikuwa na pendeleo la kuubadili mkate wa wonyesho. Ilikuwa pia katika Sabato wakati ambapo mgawanyo mmoja wa kikuhani wa juma hilo ulimaliza utumishi wao na kikundi kipya kuanza utumishi kwa juma lililofuata. Huu na utumishi mwingine wa lazima ulifanywa na makuhani bila kuvunja Sabato.—Mathayo 12:2-5; linganisha 1 Samweli 21:6; 2 Wafalme 11:5-7; 2 Mambo ya Nyakati 23:8.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki