Ile Paradiso Ambayo Yesu Alimwahidi Mtenda-Maovu
MASIMULIZI ya Luka huonyesha kwamba mtenda-maovu, aliyekuwa akiuawa kando ya Yesu Kristo, alisema maneno ya kumtetea Yesu na kuomba kwamba Yesu amkumbuke ‘atakapoingia katika ufalme wake.’ Jibu la Yesu lilikuwa: “Kweli mimi nakuambia wewe leo, utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Luka 23:39-43, New World Translation) Bila shaka, vituo vionyeshwavyo katika tafsiri ya maneno haya lazima vitegemee uelewevu wa mtafsiri wa maana ya maneno ya Yesu, kwa kuwa vituo havikutumiwa katika maandishi ya awali ya Kigiriki. Vituo vya mtindo wa kisasa havikutumika sana hadi karibu karne ya tisa W.K. Ingawa watafsiri wengi huweka koma kabla ya neno “leo” na hivyo kutoa maoni ya kwamba yule mtenda-maovu aliingia Paradiso siku hiyohiyo, katika sehemu nyingine za Maandiko hakuna jambo lolote linalounga mkono hilo. Yesu mwenyewe alikuwa mfu kwenye kaburi hata siku ya tatu na kisha akafufuliwa akiwa “matunda ya kwanza” ya ufufuo. (Matendo 10:40; 1 Wakorintho 15:20, NW; Wakolosai 1:18) Alipaa kwenda mbinguni siku 40 baadaye.—Yohana 20:17; Matendo 1:1-3, 9.
Hivyo, uthibitisho uliopo ni kwamba, matumizi ya Yesu ya neno “leo” hayakuwa yaonyeshe wakati wa mtenda-maovu kuwa katika Paradiso lakini, badala ya hilo, yalikuwa ya kuvuta uangalifu kwenye wakati ambapo ahadi hiyo ilitolewa na mtenda-maovu alipoonyesha kiasi fulani cha imani katika Yesu. Ilikuwa siku ambayo Yesu alikataliwa na kuhukumiwa na viongozi wa kidini wenye vyeo vya juu zaidi wa watu wake mwenyewe na baadaye akahukumiwa kifo na mamlaka ya Roma. Alikuwa amekuwa mtu wa kuchekwa na kudhihakiwa. Hivyo mkosaji aliyekuwa kando yake alikuwa ameonyesha sifa istahiliyo uangalifu na mtazamo wa moyoni ustahilio pongezi kwa kutokwenda pamoja na umati lakini, badala ya hilo, akamtetea Yesu na kuonyesha wazi imani yake katika Ufalme wake ujao. Zikitambua kwamba mkazo umewekwa pafaapo katika wakati wa kutolewa kwa ahadi badala ya wakati wa kutimizwa kwayo, tafsiri nyingine, kama zile za Kiingereza za Rotherham na Lamsa, zile za Kijerumani za Reinhardt na W. Michaelis, na vilevile ile Kyuretonia ya Kisiria ya karne ya tano W.K., zilitafsiri andiko hilo kwa njia inayofanana na jinsi New World Translation, iliyonukuliwa mwanzoni itafsirivyo.
Paradiso ambayo Yesu alizungumza juu yayo, ni wazi kwamba hiyo si Ufalme wa kimbingu wa Kristo. Mapema katika siku hiyo kuingia katika Ufalme huo wa kimbingu kulikuwa kumetolewa kukiwa taraja la wanafunzi waaminifu wa Yesu lakini kwa msingi wa ‘kudumu pamoja naye katika majaribu yake,’ jambo ambalo mtenda-maovu hakuwa amefanya kamwe, kufa kwake katika mti kando ya Yesu kukitokana na matendo yake ya kihalifu tu. (Luka 22:28-30; 23:40, 41) Ni wazi kwamba mtenda-maovu hakuwa ‘amezaliwa mara ya pili,’ kwa maji na roho, jambo ambalo Yesu alionyesha lilikuwa la lazima ili kuingia katika Ufalme wa mbinguni. (Yohana 3:3-6) Wala huyo mtenda-maovu hakuwa mmojawapo ‘washindi’ ambao Kristo Yesu aliyetukuzwa alisema wangekuwa pamoja naye katika kiti chake cha ufalme cha kimbingu na wanaoshiriki katika “ufufuo wa kwanza.”—Ufunuo 3:11, 12, 21; 12:10, 11; 14:1-4; 20:4-6.
Yamkini paradiso iliyojulikana vizuri na Myahudi mvunja-sheria ambaye Yesu alizungumza naye ilikuwa Paradiso ya kidunia iliyotajwa katika kitabu cha kwanza cha Maandiko ya Kiebrania, Paradiso ya Edeni. Hivyo, ahadi ya Yesu kwa kufaa ingeelekeza kwenye kurudishwa tena kwa hali ya kiparadiso ya kidunia. Hivyo ahadi yake kwa mtenda-maovu ingetokeza uhakikisho wa ufufuo wa wasio haki kama yeye wapate fursa ya kuishi katika Paradiso hiyo iliyorudishwa.—Linganisha Matendo 24:15; Ufunuo 20:12, 13; 21:1-5; Mathayo 6:10.