Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Sayansi Yaweza Kutumainiwa? Mfululizo wa makala “Sayansi Yaweza Kutumainiwa Kadiri Gani?” (Machi 8, 1998) ulikuwa onyo la wakati ufaao. Ulinisaidia kuona kihalisi mavumbuzi ya kisayansi, mengi yake yakiwa na uwezo wa kusababisha madhara mabaya kwa binadamu na mazingira yake. Kwa wakati huohuo, mfululizo huo wa makala ulielekeza wasomaji kwa Biblia—kifaa kinachotumainika kabisa.
A. I. B., Brazili
Waapache Tunapendezwa sana na historia ya hao Wahindi na tumesoma vitabu vingi kuwahusu. Kwa hiyo tunawashukuru kwa makala “Ni Nini Kilichowapata Waapache?” (Machi 8, 1998) Ilizungumzia habari hii kwa njia iliyo wazi na yenye kusadikisha.
G. C. na R. S., Italia
Mfumo wa Tabaka Nina umri wa miaka 12, na ni jana tu nilipopewa mgawo wa shule kuhusu mfumo wa tabaka. Mimi ni nusu Mhindi. Leo nilipata makala “Wakristo na Mfumo wa Tabaka.” (Machi 8, 1998) Vitabu vyangu vya shule havikueleza habari hii kwa ukamili zaidi kama mlivyofanya.
S. S. N., Marekani
Kudhibiti Mkazo Nimesoma makala kuhusu uchovu na kuchanganyikiwa akili katika magazeti yanayopendwa sana. Lakini mara nyingi yananiacha mashakani iwapo nastahili kuendelea kujikaza! Nilifurahi kuona kwamba kati ya madokezo 15 yanayohusu kudhibiti mkazo, hakuna hata moja lililodokeza kukata tamaa. (“Unaweza Kudhibiti Mkazo!,” Machi 22, 1998) Badala ya hivyo, yalionyesha jinsi ya kupunguza mkazo huku ukiendelea na maisha yako.
J. B., Bolivia
Makala hizo zilitolewa kwa wakati ufaao, kwa kuwa nimekuwa nikisumbuka kwa sababu ya hangaiko. Mimi ni mhubiri wa wakati wote, na nilifikiri sipaswi kuwa na matatizo kama haya. Nilipokuwa nikizisoma makala hizo, machozi yalinitoka. Nikang’amua ya kuwa Yehova huwatunza watumishi wake kwa wororo na huelewa yale tunayovumilia.
D. M., Italia
Kilikuwa tu kile nilichohitaji kusoma, kwa kuwa nina ugonjwa wa ngozi unaonifanya niwe na mkazo. Nyakati nyingine mimi huhisi sifai chochote kwa Yehova, lakini makala yenu ilinionyesha kwamba sivyo ilivyo. Yeye ananihangaikia kwa kweli—ananihangaikia sana hivi kwamba ameniandalia habari zote ninazohitaji kuhusu mkazo.
S. S., Brazili
Ningependa kuwashukuru kwa moyo wangu wote kwa sababu ya lile sanduku “PTSD—Itikio la Kawaida kwa Tukio Lisilo la Kawaida.” Nilifadhaika utotoni, na ingawa ningali nina kumbukumbu ya mambo yaliyopita, makala hiyo ilinifariji sana.
R. N., Marekani
Makala hizo zilikuwa zenye kuelimisha sana. Kwa kuwa mikazo kutoka kwa Shetani inaongezeka, tunahitaji habari kama hizi ili kubaki katika imani. Zilinifanya nitambue kwamba mnapendezwa sana na matatizo yetu na mnatupatia kile tunachohitaji ili kuyavumilia.
V. T., Fiji