Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Kutumika Katika Eneo Lenye Uhitaji Mkubwa Zaidi Makala yenye kichwa “Laiti Wangejua!” (Januari 8, 2005) ilinifaa sana! Katika jamii ambayo vijana wanahimizwa wafuatie mali, ni rahisi kuacha kumtanguliza Yehova maishani. Mafanikio ambayo Davey alipata kwa kutumikia katika eneo lenye uhitaji mkubwa yamenichochea kushiriki katika mgawo kama huo wa kuhubiri mwishoni mwa mwaka huu.
C. G., Marekani
Ninakubaliana kabisa na maneno ya Davey kwamba “hakuna jambo bora kuliko kumtumikia Yehova kwa nafsi yote.” Inasikitisha sana kwamba si vijana wote wanaoelewa jambo hilo! Sisikitiki kwamba niliamua kutumia ujana wangu katika utumishi wa Yehova, na ninakusudia kudumisha bidii yangu hadi mwisho kama Davey alivyofanya!
A. P., Urusi
Iwe sisi ni vijana au wazee, bidii ya Davey hutuchochea tufikiri kuhusu jinsi tunavyotumia maisha yetu. Ningependa kuwapongeza wazazi wa Davey kwa kumlea mwana wao kwa upendo. Kwa kweli, wanaweza kujivunia mwana wao!
L. C., Italia
Nina umri wa miaka 17, nami ninajifunza kazi fulani. Bado mimi ni kijana na kielelezo cha Davey kimenitia moyo zaidi kumpa Yehova kilicho bora zaidi na kutumika nikiwa mweneza-injili wa wakati wote katika siku zijazo. Kama Davey, nina tamaa kubwa ya kwenda mahali penye uhitaji mkubwa zaidi wa watumishi wa Yehova. Ninajua kwamba hiyo ndiyo njia bora zaidi ya kutumia maisha yangu.
R. I., Finland
Ninakoishi ni kawaida kwa vijana kufanya kazi au kutumia wakati wao wakifanya mambo ya kibinafsi. Nina hakika kwamba kielelezo cha Davey kitawatia moyo vijana wengi zaidi wafikirie jinsi wanavyotumia maisha yao na umuhimu wa kutimiza wakfu wao kwa Yehova.
J. O., Sweden
Makala hiyo ilinisaidia nifikirie miradi yangu ya kiroho. Nilikuwa nimeipuuza kidogo. Lakini simulizi la Davey lilifanya nifikiri kuhusu yale ambayo huenda watu wakasema nikifa. Pia lilinionyesha kwamba ninapaswa kuchunguza utumishi wangu. Endeleeni kuandika makala kama hizo zenye kutia moyo.
S. K., Ujerumani
Kwa kuwa tunaishi katika jamii inayopenda mambo ya kimwili, tunahitaji nguvu za kupinga tamaa zenye ubinafsi. Sitasahau mfano mzuri wa Davey, nami nitafanya ninachotazamiwa kufanya ili niwepo katika ulimwengu mpya unaokuja na nimshukuru kwa kunifundisha somo muhimu kwamba “hakuna jambo bora kuliko kumtumikia Yehova kwa nafsi yote.”
O. G., Ufaransa
Nina umri wa miaka kumi. Ninajua jinsi Davey alivyohisi kwa kuwa mimi pamoja na wazazi wangu ni mapainia nchini Taiwan. Makala hiyo ilinitia moyo. Inafurahisha kujua kwamba kuna vijana wengine wanaotumika katika maeneo yenye uhitaji mkubwa. Ninakubaliana na Davey kwamba hakuna jambo linaloridhisha kama hilo!
J. R., Taiwan
Sili wa Harp Asanteni sana kwa makala yenye kichwa “Watoto wa Sili wa Visiwa vya Magdalen.” (Januari 8, 2005) Nilikuwa nimeshuka moyo kwa sababu ya tatizo la afya la muda mrefu. Lakini nilichangamka sana nilipowaona viumbe hao maridadi. Nilijawa na uthamini kwa kujifunza kuwahusu na nikatiwa kicho na uumbaji wa Yehova. Nilitamani kuwagusa! Ninamshukuru Yehova kwamba kuna jambo ninaloweza kutazamia katika nchi yake mpya yenye uadilifu.
Y. M., Japani