Neno Kwenu Wazazi
Upendo wa wazazi kwa watoto wao ni sifa ya ajabu. Kama karibu wazazi wote, bila shaka wewe unapendezwa sana kuwapa watoto wako mwanzo mzuri katika maisha.
Lakini sisi tuna hakika utafahamu kwamba kuna zaidi kwa hili kuliko kuwapatia watoto wako chakula na nguo na kuwatuma kwenye masomo tu wapate elimu. lli kushinda magumu ya maisha, ni lazima watoto wawe na uongozi wa adili, kanuni za kuishi nazo. Nao wanazitaka sana hizi tangu uchanga wao na kuendelea. Mambo yenye kuhuzunisha yaweza kutukia ikiwa watoto wanachelewa mno kupokea msaada.
Labda, kama wazazi wengi, kidogo wewe hujui utaanzia wapi na utafundisha watoto wako nini. Kwa kweli, kanuni bora zinazoweza kupatikana po pote zinapatikana katika Biblia. Agizo lenye msingi wa Biblia lina faida ya kweli. Kwa njia ya Biblia, watoto wanafahamu kwamba wanaloambiwa si wazo tu la baba na mama yao. Ni lile ambalo Muumba wao anasema; ni mapenzi yake. Hii inatia nguvu shauri la wazazi ambalo haliwezi kulinganishwa katika njia nyingine yo yote.
Katika kurasa za Biblia Mungu anawatia moyo wazazi wapendezwe wenyewe katika kukazia kanuni nzuri katika akili za watoto wao. Pengine itaonekana vyepesi zaidi kumwachia mwingine daraka hili. Lakini kufanya hivi maana yake ni kukosa jambo lenye kutajirisha sana. Maana yake ni kuacha nafasi ya kuufikia moyo wa mtoto wako katika njia ambayo wewe, na si mwingine angeweza kufikia.
Katika nyumba nyingi leo wazazi na watoto wanatengana polepole. Wakati watoto wanapokuwa watu wazima, mara nyingi wazazi wanaona vigumu zaidi kusema nao juu ya mambo yaliyo ya maana zaidi sana. Kitabu hiki, “Kumsikiliza Mwalimu Mkuu,” kimekusudiwa kuzuia hali hiyo katika nyumba yako. Kimekusudiwa ili wewe na watoto wako mweze kukisoma pamoja. Lakini, zaidi ya haya, kimekusudiwa kuamsha maongezi kati ya wazazi na watoto.
Hii ni kwa sababu inataka itikio upande wa watoto. Utaona maulizo mengi yaliyotungwa vizuri katika somo lililochapwa. Wakati unayafikia haya, utaona kistari (—), kukukumbusha wewe kusimama na kumtia moyo mtoto wako aseme mwenyewe. Watoto wanapenda kutiwa ndani. Pasipo kutiwa ndani upesi kupendezwa kwa mtoto kunapungua. Maana zaidi, maulizo haya yatakusaidia ujue yaliyo katika akili ya mtoto wako. Ndiyo, labda mtoto wako atakuwa na majibu ambayo si ya kweli. Lakini somo lililochapwa linalofuata ulizo limekusudiwa kumsaidia mtoto akuze mifano mizuri ya kufikiri.
Wakati mtoto anajua kusoma, mtie moyo akusomee kitabu, na mara nyingine kujisomea mwenyewe. Kadiri anavyokisoma zaidi, ndivyo shauri lake jema litakavyokaziwa zaidi katika akili na moyo wake. Lakini, ili kuvitia nguvu vifungo vya upendo na heshima kati yenu ninyi wazazi na mtoto wenu, kwa vyo vyote someni kitabu pamoja, na kufanya hivyo kwa kawaida.
Maandiko fulani ya Biblia yametajwa mwishoni mwa kila sura. Sababu gani msitumie wakati kuyasoma pamoja? Kwa njia hiyo wewe na watoto wako mwaweza kujifunza kuitumia Biblia vizuri. Eleza maandiko haya yanasema nini. Wasaidie wafahamu maana ya maneno yo yote magumu, kama inavyofanywa katika kitabu hiki. Kufanya hivi, utakuwa ukielekeza fikira za mtoto wako kwenye chanzo bora cha uongozi katika maisha, Biblia.
Kwa unyofu wa moyo twatumaini kitabu hiki kitakusaidia wewe na jamaa yako kufanyiza maisha zenu ill mpendeze kwa Muumba, kwa baraka yenu ya milele.
—WACHAPAJI