Sababu ya Broshua Hii
Broshua hii imechapishwa ili kukuza ufahamiano na ushirikiano kati ya Mashahidi wa Yehova na wakuu wa shule. Tamaa yetu ni kushirikiana na wote ambao kusudi lao ni kutaka mipango ya elimu iliyo ya msingi inayotolewa shuleni, ifanikiwe.
Wazazi walio Mashahidi wa Yehova wanataka kusaidia ili hali ya kujifunza iwe nzuri. Wanataka watoto wao wapate faida iliyo kubwa zaidi inayowezekana kutokana na masomo yao. Na wanataka walimu na wakuu wa shule wengine wajue kwamba watajitahidi kadiri wawezavyo wasaidie kutimiza mradi huo.
Kwa ujumla Mashahidi wa Yehova wanasifiwa po pote waishipo kwa sababu ya mwenendo bora wa adili. Wanajulikana kuwa wenye kutii mamlaka za kiserikali. Hata hivyo, huenda walimu fulani wakawa na maoni kwamba vijana-Mashahidi hawana utii kwa sababu hawashiriki kila mpango au utendaji wa shule. Lakini, sababu ya kukataa kushiriki si kwamba vijana hao ni waasi wala wenye kukosa urafiki. Vitendo vyao vinategemea masadikisho ya kidini na ya kiadili.
Kwa kutumia broshua hii tunataka tueleze ulio msingi wa Kimaandiko wa imani za Mashahidi wa Yehova zinazowafanya wasishiriki shughuli fulani za shule. Broshua hii imechapishwa hasa kwa matumizi ya kibinafsi ya Mashahidi wa Yehova na watoto wao. Twataka tueleze, kwa sababu ya imani zetu, kwa nini vijana-Mashahidi hawashiriki shughuli na mipango fulani ya shule inayofanywa mahali pengi ulimwenguni pote. Pia twataka kufahamisha waziwazi kwamba sisi hatuna nia ya kulazimisha wengine wafuate maoni yetu.