NABII WA KIKE
Mwanamke anayetoa unabii au anayefanya kazi ya nabii. Kama inavyoonyeshwa chini ya vichwa NABII na UNABII, kutoa unabii kunamaanisha kuongozwa na roho ya Mungu kusema ujumbe unaotoka kwake, kufunua mapenzi ya Mungu. Kunaweza kuhusisha kutabiri matukio ya wakati ujao au la. Kama tu ambavyo kulikuwa na manabii wa kiume waliokuwa wa kweli na wa uwongo, vivyo hivyo baadhi ya manabii wa kike walitumiwa na Yehova na waliongozwa na roho yake ilhali wengine walikuwa wa uwongo, na hawakuwa na kibali Chake.
Miriamu alikuwa mwanamke wa kwanza katika Biblia kuwa nabii wa kike. Inaonekana kwamba Mungu aliwasilisha ujumbe au jumbe kupitia yeye, labda kupitia nyimbo zilizoongozwa na roho ya Mungu. (Kut 15:20, 21) Hivyo, yeye na Haruni walimwambia Musa hivi: “Je, [Yehova] hajazungumza kupitia sisi pia?” (Hes 12:2) Kupitia nabii Mika, Yehova mwenyewe alisema kwamba aliwatuma “Musa, Haruni, na Miriamu” mbele ya Waisraeli alipokuwa akiwatoa Misri. (Mik 6:4) Ingawa Miriamu alikuwa na pendeleo la kutumiwa kama kifaa cha Mungu cha mawasiliano, uhusiano wake na Mungu haukuwa wa karibu kama wa mdogo wake Musa. Alipokosa kutambua mipaka yake, aliadhibiwa vikali na Mungu.—Hes 12:1-15.
Katika kipindi cha Waamuzi, Debora alitumikia akiwa kama chanzo cha habari kutoka kwa Yehova, akifunua uamuzi wake kuhusu mambo fulani na kutoa maelekezo yake, kama katika kisa cha Baraka. (Amu 4:4-7, 14-16) Hivyo, katika kipindi ambacho taifa lilikuwa dhaifu kiroho na uasi imani, Debora alitumikia akiwa “kama mama katika Israeli.” (Amu 5:6-8) Hulda alikuwa nabii wa kike aliyetumikia kwa njia hiyohiyo katika siku za Mfalme Yosia, akiwafahamisha watu wa taifa hilo na mfalme wao hukumu za Mungu.—2Fa 22:14-20; 2Nya 34:22-28.
Isaya anasema kwamba mke wake alikuwa “nabii wa kike.” (Isa 8:3) Ingawa baadhi ya wachambuzi wanadokeza kwamba ilikuwa hivyo kwa sababu alikuwa mke wa nabii, Maandiko hayatoi uthibitisho wowote unaounga mkono wazo hilo. Inaelekea alipokea mgawo fulani wa kutoa unabii kutoka kwa Yehova, kama ilivyokuwa kwa manabii wengine wa kike waliokuwa kabla yake.
Nehemia anataja mambo mabaya kumhusu nabii wa kike aliyeitwa Noadia, ambaye pamoja na “manabii wengine” walijaribu kumwogopesha Nehemia ili wazuie ujenzi wa kuta za Yerusalemu. (Ne 6:14) Ingawa alipinga mapenzi ya Mungu, hilo halimaanishi kwamba kabla ya hapo hakuwa na msimamo mzuri mbele za Mungu.
Yehova alimwambia Ezekieli kuhusu wanawake Waisraeli ‘waliotunga unabii wao wenyewe.’ Jambo hilo linaonyesha kwamba manabii hao wa kike hawakupokea mgawo wao kutoka kwa Mungu, badala yake walikuwa manabii bandia, waliojifanya wenyewe kuwa manabii. (Eze 13:17-19) ‘Waliwawinda watu’ kwa mazoea yao ya kuwashawishi na kuwadanganya watu na kutumia propaganda, wakiwahukumu waadilifu na kuwaunga mkono waovu, lakini Yehova angewaokoa watu wake kutoka katika mikono yao.—Eze 13:20-23.
Yesu alipozaliwa, wakati ambapo Wayahudi walikuwa bado katika agano na Yehova, Ana aliyekuwa amezeeka alitumikia akiwa nabii wa kike. “Hakukosa kamwe hekaluni, akitoa utumishi mtakatifu usiku na mchana, akifunga na kutoa dua.” Kwa kuwaambia “kuhusu mtoto huyo wale wote waliokuwa wakisubiri ukombozi wa Yerusalemu,” alitenda kama nabii wa kike kwa maana ya kwamba ‘alisema’ kuhusu kufunuliwa kwa kusudi la Mungu.—Lu 2:36-38.
Kutoa unabii ni mojawapo ya zawadi za kimuujiza za roho takatifu ambazo washiriki wa kutaniko jipya la Kikristo walipewa. Wanawake fulani Wakristo, kama vile mabinti wanne wa Filipo ambao hawakuwa wameolewa, walitoa unabii wakiongozwa na roho takatifu ya Mungu. (Mdo 21:9; 1Ko 12:4, 10) Huo ulikuwa utimizo wa Yoeli 2:28, 29, iliyotabiri kwamba “wana wenu na mabinti wenu watatoa unabii.” (Yoe 2:28, 29; Mdo 2:14-18) Hata hivyo, zawadi kama hiyo haikumwondolea mwanamke wajibu wa kujitiisha chini ya ukichwa wa mume wake au chini ya wanaume wengine katika kutaniko la Kikristo; ili aonyeshe ujitiisho wake, alipaswa kufunika kichwa chake alipotoa unabii (1Ko 11:3-6) na hakupaswa kufundisha kutanikoni.—1Ti 2:11-15; 1Ko 14:31-35.
Mwanamke aliyekuwa kama Yezebeli katika kutaniko la Thiatira alidai kuwa na nguvu za kutoa unabii lakini aliiga mfano wa manabii wa kike wa uwongo wa siku za kale, naye alipokea hukumu kutoka kwa Kristo Yesu katika ujumbe wake kwa Yohana katika kitabu cha Ufunuo 2:20-23. Alijiendesha isivyofaa kwa kuwafundisha na kuwapotosha watu kutanikoni wajiingize katika mazoea mabaya.