Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Je! mfano wa Biblia ambamo Yehova alimkataa Onani kwa sababu ya kuharibu bure shahawa yake unaonyesha kwamba matumizi ya dawa za kuzuia uzazi ni mabaya?—U.S.A.
Hapana, kwa maana uchunguzi wa maandishi juu ya Onani unafunua kwamba yeye hakuuawa kwa sababu ya kuzuia uzazi.
Nyuma ya kifo cha nduguye Eri, Onani alishauriwa na babaye Yuda afanye ndoa na mke wa nduguye Tamari. Hii ilikuwa kwa kusudi lenye maana la ‘kumwinulia nduguye aliyekufa uzao,’ Ama sivyo asingekuwa na haki yo yote ya kufanya ngono naye. Juu ya itikio la Onani kwa amri ya Yuda, twasoma: “Onani alijua ya kwamba huo uzao hautakuwa wake, ikawa, alipoingia kwa mke wa nduguye, akamwagia chini asimpe nduguye uzao. Neno hili alilolifanya likawa baya machoni pa [Yehova].” (Mwa. 38:8-10) Nyumaye ndoa ya mtu na mke wa nduguye ilitiwa katika agano la Torati kwa amri ya Yehova.—Kum. 25:5, 6.
Kwa kutenda tofauti na kusudi la ndoa ya mtu na mke wa nduguye, Onani alimvunjia babaye heshima. Kwa kutoitii amri ya babaye, kwa choyo alikataa kuuhifadhi ukoo wa Eri. Vile vile huu ulikuwa wonyesho wa chuki kwa Eri, kwa maana Onani hakusaidia katika faida za nduguye aliyekufa, bali alifanya tofauti yake. Onani alimwaibisha mjane wa nduguye bila ya huruma. Kwa choyo aliufunua utupu wake lakini akamnyima haki ya umama. Vile vile alionyesha kwamba ‘hakuona ubora wa mambo matakatifu,’ kwa maana ulikuwako uwezekano wa kwamba Masihi aliyeahidiwa angaliweza kupitia kwa uzao ambao yeye angaliweza kutokeza kwa Tamari. (Linganisha Waebrania 12:16, NW.) Mambo haya yote yanafunua kwamba Onani alikuwa mtu mwovu asiyeziheshimu faida za wengine faida zake mwenyewe zilipoelekea kuwa hatarini. Yehova alimwua Onani kwa maana sababu yake ya kutompa nduguye aliyekufa uzao haikuwa yenye nguvu.
Kisa cha Onani kuwa mtu asiyeliheshimu kusudi la ndoa ya mtu na mke wa nduguye kwa sababu ya choyo hakiwezi kutumiwa kwa kukataza uzuiaji wa uzazi. Inastahili kuangaliwa kwamba Biblia haizungumzi matumizi ya dawa za kuzuia uzazi katika ndoa mahali po pote. Wala haisemi kwamba Wakristo wanalazimishwa kuzaa watoto. Kwa hivyo, kwa habari ya kuzuia uzazi, wenzi waliooana wa Kikristo lazima wairuhusu dhamiri yao iliyozoezwa na Biblia iamue.
● Je! Wagalatia 4:15 inaonyesha namna iwapasavyo Wakristo kuona kupandikiza viungo vya mwili mmoja katika mwili mwingine?—U.S.A.
Wagalatia 4:15 inasema: “Kama ingaliwezekana, mngaling’oa macho yenu, mkanipa mimi.” Hapa mtume Paulo alikuwa akisema kwa njia ya mfano tu. Wagalatia walimheshimu na kumpenda sana Paulo hivyo kwamba wangalikuwa wenye nia ya kutoa cho chote chenye faida kwao wenyewe, ndiyo, hata kitu fulani kilicho bora na cha lazima kama macho yao yenye kuona, kusudi wamsaidie aone. Vivyo hivyo Yesu Kristo alilitaja jicho kama likifananisha kitu kilichopewa kuona aliposema: “Jicho lako la kuume likikukosesha, ling’oe ulitupe mbali nawe.” (Mt. 5:29) Matumizi ya kuona kusudi mtu atazame kitu fulani kinachomfanya mtu aanguke kwa kiroho yalipaswa yafishwe. Wala Yesu wala Paulo hakuwa akizungumza habari ya kupandikiza viungo vya mwili mmoja katika mwili mwingine.