Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 4/15 kur. 190-191
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 4/15 kur. 190-191

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

● Je! mtume Paulo alikuwa mmoja wa wale mitume kumi na wawili?

Ushuhuda unafunua kwamba, ingawa Paulo alikuwa mtume wa Yesu Kristo, Biblia haimsemi kama mmoja wa ‘mitume kumi na wawili.’

Neno la Kigiriki a·poʹsto·los maana yake ni “anayetumwa.” Expository Dictionary of New Testament Words ya Vine, juu ya “Mitume,” inasema: “Paulo, ingawa alimwona Bwana Yesu, 1 Kor. 9:1; 15:8, ‘hakufuatana’ na mitume Kumi na Wawili ‘wakati wote’ wa huduma yake duniani, na hivyo hakufaa kuwa mmoja wao, kulingana na maelezo ya Petro ya sifa za maana, Matendo 1:22. Paulo aliamriwa moja kwa moja na Bwana Mwenyewe, nyuma ya Kupaa Kwake, kupeleka Injili kwa Mataifa.”

Yuda Iskariote alikuwa mmoja wa wale kumi na wawili wa kwanza aliyechaguliwa na Yesu kuwa mtume. (Mt. 10:2-5; Luka 6:13-16) Lakini akawa mwivi, na nyumaye akawa msaliti, akimsaliti Yesu na mwisho kujiua mwenyewe, akiwaacha mitume waaminifu kumi na mmoja.​—Yohana 12:4-6; 18:1-5.

Nyuma ya kifo cha Yesu, lakini mbele ya Pentekoste, 33 C.E., mtume Petro alieleza penye mkutano wa Kikristo lazima ya kujaza nafasi ya Yuda, kulingana na maneno ya unabii katika Zaburi 109:8. “Wakaweka [wanaume wote wa Kikristo wakiwepo] wawili, Yusufu aitwaye Barsaba, aliyekuwa na jina la pili Yusto, na Mathiya.” Wakristo waliokutanika wakashukuru, wakimwomba Yehova achague wa kushika nafasi. Ndipo “wakawapigia kura [wale wawili]; kura ikamwangukia Mathiya; naye akahesabiwa kuwa pamoja na mitume kumi na mmoja.”​—Matendo 1:15-26.

Kama vile wana kumi na wawili wa Yakobo walivyokuwa misingi ya taifa la Israeli wa asili mwanzoni, ndivyo ingekuwa kwa mfano kwamba misingi kumi na miwili ya Israeli wa kiroho (iliyojengwa juu ya Msingi Mkuu, Yesu Kristo) iwepo wakati wa kusimamishwa kwa kundi la Kikristo, wakati wa Pentekoste. Wakati wale wanafunzi karibu 120 walipokusanyika chumba cha juu siku ya Pentekoste, walikuwa wakitazamia kubatizwa kwa roho takatifu, kwa vile Yesu alikuwa amewaambia siku kumi mbele ya kupaa kwake kwamba haitakuwa ‘siku nyingi.’ (Matendo 1:5, 8) Hapo kundi la Kikristo lilianzishwa, na kama watu 3,000 walijengwa juu ya msingi siku ile ile. Sasa, hakuna msingi unaojengwa nyuma ya kuanzwa kwa ujenzi wa juu. Hivyo haielekei kwamba Mungu angeacha nafasi ya Yuda, akingojea kugeuka kwa Sauli (Paulo). Mungu papo hapo aliikubali sala ya wanafunzi waliokusanyika. Kwa hiyo kura ilionyesha uchaguzi wa Yehova kwa Mathiya.​—Mit. 16:33.

Je! nyumaye Mathiya alionyesha sifa za mtume? Maandiko yanaonyesha kuwa mitume walikuwa nao, kati ya vipawa vingine, uwezo wa kupisha vipawa vya miujiza vya roho. (Matendo 8:14-18; 10:44) Kwa kweli kama Mathiya hakuchaguliwa na Mungu, udhaifu wake wa kufanya hili ungekuwa wazi kwa wote. Lakini Biblia haisemi lo lote juu ya kasoro ya Mathiya katika jambo hili.

Muda fulani nyuma ya Pentekoste, 33 C.E., lakini mbele ya kuongoka kwa Paulo, “wale kumi na wawili” waliondoa ugumu wa mgawo wa chakula, kwa kuweka halmashauri ya watu saba wasimamizi. “Mitume” waliwapendekeza kwa kuweka mikono juu yao. Bila shaka Mathiya alikuwa mmoja wa ‘wale kumi na wawili,’ “mitume,” waliofanya hivyo.​—Matendo 6:1-6.

Labda ni karibu mwaka wa 34 au 35 C.E., Paulo alipoongoka kuingia katika Ukristo. Wakati huo Yesu aliyefufuliwa alimwambia Paulo kwamba angetumwa kutangaza jina la Yesu kwa mataifa yasiyo ya Kiyahudi. Kwa hiyo Paulo angekuwa ‘mtume [siyo wa kundi fulani, bali mtume au ‘aliyetumwa’ wa Bwana Yesu Kristo] kwa mataifa.’ (Matendo 9:15; 26:14-18; Gal. 1:15, 16; Rum. 1:5; 11:13; 1 Tim. 2:7) Mtume Yakobo hakuuawa na Herode mpaka mwaka wa 44 C.E., kwa hiyo inaelekea kwamba wote kumi na wawili walikuwa hai wakati Paulo alipopokea agizo. (Matendo 12:1, 2) Hata hivyo lazima ijulikane kwamba hakuna nafasi ya mtume ilijazwa kwa sababu ya kifo; ni nafasi ya Yuda tu iliyojazwa kwa sababu ya kutokuwa mwaminifu. Hakuna “warithi” wa mitume kumi na wawili. Hakuna shauri lo lote katika Biblia lisemalo kwamba Paulo alimwondoa Mathiya katika nafasi yake au kuchukua nafasi ya mwingine ye yote wa mitume.

Ingawa Paulo aliukubali utume wake, na alikuwa na nguvu zote na sifa za mtume wa Yesu Kristo kwa kuwekwa penye nafasi hii katika “mwili” wa Kikristo na Yehova, Paulo hakujihesabu kati ya wale kumi na wawili wakati wo wote. (Gal. 1:1; 2:8; 1 Kor. 9:1, 2; 12:27, 28) Kuliko hivyo, akiandika juu ya wale Kristo aliyefufuliwa alitokea, Paulo alijitaja kwa kujitofautisha mwenyewe na wale “mitume wote” na ‘wale kumi na wawili.’ (1 Kor. 15:5, 7, 8) Katika 1 Wakorintho 15:5 agizo la ‘kumi na wawili’ ni juu ya mitume kwa wakati mbele ya Mathiya kuchaguliwa, lakini kulingana na Matendo 1:21, 22 Mathiya anaweza kutiwa ndani, ambaye wakati huo alishirikiana na wale kumi na mmoja.

Katika maelezo ya Yerusalemu Mpya, mji wa mbinguni ambako Yehova na Yesu Kristo wanaonekana wakikaa, tunasoma: “Na ukuta wa mji ulikuwa na misingi kumi na miwili, na katika ile misingi majina kumi na mawili ya wale mitume kumi na wawili wa Mwana-Kondoo.” (Ufu. 21:2, 14) Ushuhuda uliotolewa sasa hivi unaongoza kwenye mwisho kwamba jina la Mathiya, siyo Paulo, lilikuwa juu ya mojawapo ya mawe kumi na mawili. Mathiya alikuwa mtume kutokea mwanzo (Pentekoste, 33 C.E.) wa taifa la kiroho la wale 144,000 wafanyao Yerusalemu Mpya, “bibi-arusi” wa Kristo. (2 Kor. 11:2; Ufu. 21:2) Ni kweli, Paulo aliandika nyaraka nyingi zilizoongozwa na roho ya Mungu. Lakini ya kwanza kati ya hizi aliandika miaka kumi na saba nyuma ya taifa la kiroho kuanzishwa, wakati ambao taifa lilikuwa limekua kuongezea na maelfu ya watu.

Kwa hiyo, ushuhuda unaonyesha kwamba Paulo hakuwa mmoja wa mitume kumi na wawili, misingi midogo ya Yerusalemu Mpya. Hata hivyo, alikuwa mtume wa pekee wa Kristo kwa mataifa, au wasio Wayahudi, na mgawo huu aliutimiza kwa bidii.​—2 Tim. 4:7, 8.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki