Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa
—United States ya Amerika
HUKO nyuma katika miaka ya 1920, watumishi wa Yehova walikuwa wenye kazi nyingi ya kumtangaza Mfalme na Ufalme, wakawa na matokeo mazuri. Zaidi ya hilo, ingawa watu wa Mungu hawakulijua jambo hili, wakati huo walikuwa wakitimiza kwa njia ya kusisimua unabii mbalimbali wa Ufunuo. Wakati malaika wapiga-tarumbeta saba walipokuwa wakipiga mbiu zao, Wakristo wa kweli walishiriki katika matukio ya kutazamisha duniani nao wanaendelea kuyashiriki hata sasa.—Ufu. 8:1—9:21; 11:15-19.
Tangu malaika wa kwanza alipopiga tarumbeta (baragumu) yake, Jumuiya ya Wakristo imepigwa kwa mawe ya barafu ya mfano yenye kuharibu, ikaonyeshwa sana kuwa mbaya kwa kweli ya Biblia. (Ufu. 8:7) Hilo lilianza wakati wa kusanyiko la Wanafunzi wa Biblia la Cedar Point Septemba mwaka wa 1922. Huko watu wa Mungu walikubali kwa shauku azimio lililoitwa “Mwito wa Kushindana.” Kwa ujasiri lilifunua wazi kutoaminika kwa mapadre juu ya Mungu kwa kushiriki vitani kisha kukana ufalme Wake wa Kimasihi kwa kushikilia kwamba Ushirika wa Mataifa ulikuwa ndio wonyesho wa kisiasa wa ufalme huo. Oktoba mwaka huo wa 1922 nakala 45,000,000 za azimio hilo na habari zenye kuunga mkono zilianzwa kuenezwa duniani pote. Tangu wakati huo na kuendelea, Jumuiya ya Wakristo (mapadre wake wa Kikatoliki na wa Kiprotestanti na wanakanisa wake) imefunuliwa wazi kuwa ya uongo katika dai la kuwa wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo.
Chini ya uongozi wa malaika mpiga-tarumbeta pili, Wanafunzi wa Biblia walifanya kusanyiko la jimbo katika Los Angeles, California, Agosti 18-26, 1923. Huko walikubali kwa shangwe azimio lenye kujulikana sana lililoitwa “Onyo.” Lilifunua wazi kushindwa kwa mapadre wa Jumuiya ya Wakristo kusaidia kutangaza ujumbe wa Ufalme nalo likaomba watu wenye mfano wa kondoo waugeukie ufalme wa Mungu, si Ushirika wa Mataifa wenye kuungwa mkono na mapadre hao, kama “njia ya pekee ya kuondolea mabaya yenye kutendwa na mataifa na watu mmoja mmoja.” Kushindwa kwa mapadre kufanya hivyo kumetokeza sana watu wenye kutaka mapinduzi, wenye kufananishwa na “bahari” isiyotulia. Lakini wataka mapinduzi hao hawawezi kuwapa wanadamu uzima, kama vile damu iliyomwagwa kutoka mwili wa kibinadamu isivyoweza kupa uzima. Desemba 1923 trakti yenye kuitwa “Tangazo—Onyo kwa Wakristo Wote” ilianzwa kuchapwa, nayo ilikuwa na azimio la kusanyiko. Zaidi ya mamilioni ya nakala yaliyochapwa ng’ambo, nakala 13,478,400 zilichapwa United States. Uenezaji mkubwa sana wa trakti Tangazo ulikuwa mwanzo tu. Hata leo hii, wafuasi watiwa mafuta wa Yesu wametoa matangazo mengi ya kutetea ufalme wa Mungu.—Ufu. 8:8, 9.
Wakati malaika wa tatu alipopiga tarumbeta (baragumu) yake, theluthi au sehemu moja ya tatu ya maji iligeuzwa ikawa pakanga (yakawa machungu). (Ufu. 8:10, 11) Kulingana na hilo, katika kusanyiko la Wanafunzi wa Biblia la Julai 20-27, 1924, katika Columbus, Ohio, watu wa Mungu walikubali kwa shauku azimio lililoitwa “Shtaka.” Liliyafunua wazi mafundisho ya uongo yenye kumsuta Mungu yanayoonyesha vile wao na wenzi wao wa kisiasa walivyokuwa wakielekeza watu kwenye mauti. Kwa kweli, mapadre walikuwa wakifanya watu wanywe kitu kichungu kama pakanga nao wangekufa kiroho na mwishowe waharibiwe. Azimio la kusanyiko lilitiwa katika trakti iliyoitwa “Mapadre Washtakiwa,” na nakala 13,545,000 zilichapwa United States. Mamilioni zaidi katika lugha za kigeni yalichapwa ng’ambo. Baadaye, nakala 50,000,000 zilikuwa zimekwisha enezwa. Shtaka hilo lilichapwa pia katika The Watch Tower. Tena, huo ulikuwa mwanzo tu. Kwa kutumia radio, vitabu, vijitabu, magazeti na ushuhuda wa mdomo watumishi wa Yehova wameendelea kuonyesha wazi kwamba mafundisho ya mapadre wa Jumuiya ya Wakristo si maji ya uzima, bali yaelekeza kwenye mauti.
Ndipo ulipokuja mwaka wa 1925 kisha malaika wa nne mpiga tarumbeta akajitayarisha kuchukua hatua. Akapiga tarumbeta (baragumu) yake na theluthi moja au sehemu moja ya tatu ya jua, mwezi na nyota ikapigwa na kutiwa giza. (Ufu. 8:12) Katika kusanyiko la jimbo katika Indianapolis, Indiana, Agosti 24-31, 1925, watumishi wa Mungu waliunga mkono kwa moyo azimio lililoitwa “Ujumbe wa Tumaini.” Lilitoa maneno ya upendo, lakini likaonyesha pia kwamba watu walikuwa wameanguka gizani katika Jumuiya ya Wakristo, ambayo inajidai kuwa ndiyo nuru ya kiroho ya ulimwengu. Zaidi ya kuchapwa kwa azimio hilo katika The Watch Tower na The Golden Age, mwishowe mamilioni mengi ya nakala zilichapwa katika trakti zikaenezwa katika lugha mbalimbali. Hivyo watu walifahamishwa kwamba Jumuiya ya Wakristo haikuwa ikifurahia nuru ya kweli ya kimbinguni wala kibali ya kimungu.
Shambulio la nzige wa mfano lilitangazwa wakati malaika wa tano alipopiga tarumbeta (baragumu) yake katika masika ya mwaka wa 1926. (Ufu. 9:1-11) Mei 25-31 ya mwaka huo Wanafunzi wa Biblia walifanya kusanyiko la mataifa yote London, Uingereza. Huko walikubali kwa moyo wote azimio lililoitwa “Ushuhuda kwa Watawala wa Ulimwengu.” Azimio hilo na hotuba ya watu wote yenye kuliunga mkono “Sababu Mamlaka za Ulimwengu Zinatikisika—Dawa,” iliyotolewa Jumapili, Mei 30, na Ndugu Rutherford kwa wasikilizaji wengi sana katika Royal Albert Hall, lilionyesha wazi kwamba Ushirika wa Mataifa ulianzwa na Shetani kisha likaonyesha mapadre walikuwa wameshindwa kuunga mkono ufalme wa Mungu wa Kimasihi. Habari kama hizo zilitokea katika kitabu kilichotolewa karibuni huko Deliverance (Ukombozi) na katika kijitabu The Standard for the People (Kanuni kwa Ajili ya Watu.) Jumatatu asubuhi, The Daily News la London lilitumia ukurasa mzima kuandika azimio hilo na muhtasari ya hotuba ya watu wote ya Jumapili, pamoja na tangazo la hotuba ya usiku wa Jumatatu ya Rutherford. Nafasi hiyo iliyotumiwa kuandika habari katika gazeti hilo ilikuwa imenunuliwa kwa pesa nyingi, na nakala milioni moja au zaidi za chapa hiyo zilienezwa kwa hadhara ya watu.
Baadaye, karibu nakala za trakti 50,000,000 zenye azimio “Ushuhuda” zilikuwa zimeenezwa duniani mwote katika lugha nyingi. Kuonyesha wazi hivyo kwamba hila za kibinadamu zilikuwa zimetungwa kupinga ufalme wa Mungu kwa kutumia dini, kulikuwa kama kichomi cha mkia wa nge, na bado hilo linaendelea kuonyeshwa wazi.
Wakati malaika wa sita alipopiga tarumbeta (baragumu) yake, malaika wanne wa mfano walifunguliwa kisha farasi 200,000,000 wa mfano wakaondoka “waue theluthi ya wanadamu.” “Farasi” hao wanafananisha njia ya kutangazia ujumbe wa kuogofya wa hukumu, hasa kwa vitabu na magazeti. Hatua hiyo ilianza kwa tukio linalojulikana sana la mwaka wa 1927—kusanyiko la mataifa yote la Wanafunzi wa Biblia katika Toronto, Ontario, Canada. (Ufu. 9:13-19) Huko katika Coliseum (Jumba Kubwa) Jumapili, Julai 24, karibu watu 15,000 walimsikia J. F. Rutherford akisoma azimio lenye kutolewa “Kwa Watu wa Jumuiya ya Wakristo,” ambayo ina karibu theluthi moja ya wanadamu. Liliwasihi watu wenye mioyo minyofu waiache Jumuiya ya Wakristo wasije wakaharibiwa pamoja nayo. Watu walisihiwa wajitoe kwa moyo wote na uaminifu wote kwa Yehova Mungu na Mfalme na ufalme wake.
Lo! wafuasi wa Jumuiya ya Wakristo walitaabikaje chini ya moto wa maneno fulani yaliyokuwamo katika azimio hilo lenye kuchochea! Azimio hilo na hotuba ya watu wote iliyoambatana nalo lilichapwa katika kijitabu Freedom for the Peoples. Baada ya muda fulani mamilioni ya nakala yalienezwa kwa watu wa kawaida na watawala. Hivyo mamilioni ya farasi wa mfano yalianza kuishambulia Jumuiya ya Wakristo, yakifanya hivyo kwa uongozi wa mabaki watiwa mafuta, wale “malaika wanne.” Miaka yote iliyofuata, mamia ya mamilioni ya nakala za vitabu hivyo vya Kikristo zimechapwa na maelfu ya watu wameitikia vizuri, wakaacha Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo.—Ufu. 9:13-19; 18:2, 4, 5.
Matukio ya kutazamisha yalitukia wakati malaika wa saba alipopiga tarumbeta (baragumu) yake. “Pakawa na sauti kuu katika mbingu, zikisema, Ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atamiliki hata milele na milele.” Ingawa ufalme wa ulimwengu wa wanadamu ni haki ya Mungu, tangu mwaka wa 607 K.W.K. yeye aliruhusu ufalme wa mzao mtiwa mafuta wa Mfalme Daudi ukome au ukatizwe kwa “nyakati saba,” au miaka 2,520. Kipindi hicho kilimalizika karibu na Oktoba 4/5, mwaka wa 1914 W. K. Watu walipaswa kujua kwamba karibuni Yehova ‘angewaharibu hao waiharibuo nchi’ kupitia kwa ufalme wa Kimasihi uliosimamishwa mwaka huo, na kwamba watu wenye kulicha jina lake wangekuwa wafanya kazi wenzake katika kuifanya dunia iwe paradiso.—Ufu. 11:15-18.
Ni wakati gani mambo hayo yangetangazwa ulimwenguni pote kama kwa mlio wa tarumbeta ya “malaika wa saba”? Tangazo hilo la kuzunguka dunia yote lilianza kutolewa mwaka wa 1928, wakati Wanafunzi wa Biblia walipokuwa na kusanyiko katika Detroit, Michigan, Julai 30—Agosti 6. Hasa inayostahili kuangaliwa ni Jumapili, Agosti 5, kwa maana wakati huo wajumbe walilisikia azimio lenye kuchochea lililoitwa “Tangazo la Kupinga Shetani na Kuunga Mkono Yehova,” na vilevile hotuba ya watu wote ya J. F. Rutherford yenye kuliunga mkono, “Mtawala wa Watu.” Kati ya mambo mengi yaliyotangazwa, azimio hilo Iilitangaza kwamba kwa sababu Shetani hatakubali kuacha kutawala vibaya mataifa na watu, Yehova pamoja na afisa wake mtekelezaji Yesu Kristo atachukua hatua juu ya Ibilisi na majeshi yake ya uovu, kisha Shetani atazuiwa kabisa na tengenezo lake litapinduliwa kabisa. Tena, lilionyesha kwamba Mungu atamtumia Kristo kuimarisha haki duniani, akomboe wanadamu katika uovu na kuleta baraka za milele kwa mataifa yote ya dunia. “Kwa hiyo,” likamalizia azimio, “wakati unaofaa umekuja kwa wote wapendao haki kusimama upande wa Yehova na kumtii na kumtumikia yeye kwa moyo safi, ili wapokee baraka zisizo na kikomo ambazo Mungu Mwenyezi amewawekea akibani.”
Ripoti za hilo “Tangazo la Kupinga Shetani na Kuunga Mkono Yehova” na hotuba ya watu wote yenye kuliunga mkono zilichapwa katika The Golden Age na The Watch Tower. Zaidi ya hilo, mamilioni ya nakala za azimio hilo na hotuba pia yalienezwa katika lugha kadha katika kijitabu The Peoples Friend. Hivyo ujumbe wenye kuunga mkono ufalme wa Mungu kupitia kwa Yesu Kristo na wenye kudharau utawala wa ulimwengu wa Shetani na mawakili wake ulienezwa zaidi ya miaka 40 iliyopita. Lakini umetangazwa kwa nguvu zaidi duniani pote kwa vitabu, magazeti na hotuba za watu wote tangu wakati huo, wakati watumishi wa Yehova wanapoendelea kupelekea watu wa dunia ujumbe wa ufalme wa Mungu.
—Kutoka 1975 Yearbook of Jehovah’s Witnesses.