Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa—United States ya Amerika
KATIKA Maandiko, watu wa Mungu wanafananishwa na kondoo Yehova akiwa ndiye Mchungaji wao wa kimbinguni. (Zab. 28:8, 9; 80:1; Eze. 34:11-16) Zaidi ya kufurahia uangalizi wake wa huruma, wanafurahia msaada na uongozi wa Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, na vilevile msaada wa wachungaji wengine waliomo katika kundi la Kikristo. (Mt. 25:31-46; Luka 12:32; Yohana 10:14-16; 1 Pet. 5:1-4) Wanaume waliokuwa wamechaguliwa kuwa wazee kundi likiinua mikono kuanzia miaka ya 1870 mpaka 1932 walisimamia mafunzo ya Biblia ya kundi na kutoa hotuba. Wanaume waliochaguliwa kwa kuinua mikono washike vyeo vya mashemasi waliwasaidia hao. Kulingana na anavyosema C. W. Barber, wazee “walikuwa wakiongoza mambo ya kiroho, kuongoza mikutano, kutoa hotuba na kuangalia mambo ya jumla,” lakini mashemasi “walikuwa wakitumiwa kama wakaribishaji, wakiangalia vile watu watakavyoketi na kusaidia kwa njia za kimwili.”
“Ni nini kilichoamua ubora wa kiroho wa wenye kuchaguliwa kuangalia kundi?” auliza Henry A. Rheb. Kwa ufupi, ajibu hivi: “Kwanza, hakuna mtu mpya aliyechaguliwa, na bila shaka jambo hilo lililingana na Maandiko. Kabla ya mkutano wa shughuli, sifa za cheo hicho zilisomwa katika 1 Timotheo 3:1-13 na Tito 1:5-9.” “Orodha ya wenye kufikiriwa kuchaguliwa ilipokwisha kuwekwa,” asema Edith R. Brenisen, “tulionywa kwa bidii tufikirie kwa uangalifu na kwa kusali sifa na uwezo mbalimbali wa kila mmoja aliyefikiriwa kuchaguliwa kulingana na Biblia, tukiomba uongozi wa roho takatifu katika kufanya maamuzi yetu. . . . tulikutana tena katika wakati uliowekwa kuchagua wale waliokuwa wamefikiriwa.”
Wazee wengine walijiona wakubwa zaidi nao walitaka kutoa hotuba tu, asema Dada J. M. Norris. Aendelea kusema hivi: “Wengine walilaumu makala zilizokuwamo katika The Watchtower, wasitake kulikubali gazeti hilo kama njia ya Mungu ya kufunua kweli, sikuzote wakijaribu kushawishi wengine wafuate mawazo yao.”
Walakini, isiazimiwe kwamba wazee wote wa kuchaguliwa walikuwa na nia au roho mbaya. Wengi walitimiza madaraka yao kwa uaminifu kama wachungaji wa Kikristo wa watu wa Mungu. (1 Pet. 5:1-4)
“Wazee wa kuchaguliwa” walisimamia utendaji mbalimbali wa makundi kwa miaka mingi. Walakini, mwaka wa 1932 ulipofika, badiliko la muda lilitokea. Washiriki wa zamani wa jamaa ya Betheli ya Brooklyn wangali wakumbuka mkutano uliofanywa Jumatano jioni, Oktoba 5, 1932, katika Apollo Hall Brooklyn. Wakati huo washiriki karibu 300 wa kundi la New York walipitisha azimio la kuacha kuchagua wazee katika mji wa New York. (Tazama The Watchtower la Septemba 1, 1932, kurasa 265 na 266, na vilevile toleo la Oktoba 15, 1932, ukurasa wa 319.) Karibu makundi mengine yote yaliacha mara moja kuchagua wazee, wakapitisha maazimio kama hilo. Hivyo mwaka wa 1932 vikundi vya wanaume waliokomaa wa Kikristo wenye kuitwa “halmashauri ya utumishi” ndivyo vilivyokuwako badala ya “wazee wa kuchaguliwa,” nao wanaume hao walichaguliwa na kundi wasaidie msimamizi wa utumishi katika kila kundi aliyekuwa amewekwa na Watch Tower Society.
Kuanzishwa kwa mpango mpya mwaka wa 1932 kulileta magumu, na watu wengine walitoka katika tengenezo. Walakini, makundi mengi sana na washiriki wayo walilikubali badiliko la tengenezo kwa shukrani.
Mwaka wa 1938 kulikuwa na tukio jingine la maana sana katika tengenezo. Makala za Watchtower zenye kusema “Umoja Wafanya Kazi” (Mei 15) na “Tengenezo” (Juni 1 na 15) zilionyesha kwamba makundi moja moja siyo yaliyokuwa na mamlaka ya kuweka waangalizi na wasaidizi wao. Ilipendekezwa makundi ulimwenguni mwote yafikirie azimio lililotolewa katika The Watchtower, wakiomba “Sosaiti” itayarishe kundi kwa utumishi na ‘kuweka watumishi wake mbalimbali,’ yaani, wote watakaoshika vyeo vya madaraka katika kila kundi. (Tazama The Watchtower la 1938, kurasa 169, 182, 183.) Makundi mengi yalikubali azimio hilo, na machache yasiyofanya hivyo karibuni yalipoteza maoni yao ya kiroho na mapendeleo waliyokuwa nayo kuhusu utumishi wa Ufalme.—Kutoka 1975 Yearbook of Jehovah’s Witnesses.