‘Wanaona Mema Kwa Sababu ya Kazi Yao’
PUSAN, Korea, ni mji wenye kusongamana watu. Kwa muda unaopungua miaka 30, idadi ya watu imeongezeka sana kutoka robo milioni ikawa milioni na nusu, na bado watu wanaongezeka! Mji Pusan ulianza kujulikana sana wakati wa Vita ya Korea, wakati ambao ulipata kuwa mji mkuu wa nchi hiyo kwa muda, na mahali pa kukimbiliwa na maelfu ya watu waliotoroka kabla Wakomunisti hawajaanza shambulio lao.
Kati ya watoro hao walikuwako watu walioziamini ahadi za Ufalme wa Mungu zilizomo katika Biblia, wakafanya kama Wakristo wa kwanza walivyofanya baada ya ‘kutawanywa,’ yaani, wakaendelea ‘kuzitangaza habari njema za lile neno.’ Kwa hiyo, kundi la Mashahidi wa Yehova lilianzwa Pusan. Huo ulikuwa mwaka 1950. Lakini kufika mwaka 1976 kundi hilo la kwanza lilikuwa limepanuka likawa makundi 54 katika eneo la Pusan.—Matendo 8:4, tafsiri ya Kiingereza ya New World.
Mpanuko huo, pamoja na ukuzi wa idadi ya watu, umeleta matatizo. Katika mji huo wenye kusongamana watu ikawa inaelekea kutowezekana Mashahidi wa Yehova wakodi mahali pa makusanyiko yao ya mzunguko ya kila nusu-mwaka. Wangefanya nini? Katika nchi nyingi za Magharibi Mashahidi walikuwa wakijenga majumba ya makusanyiko hayo. Ikiwa hilo lingeweza kufanywa Amerika na Ulaya, sababu gani lisiwezekane Asia? Hivyo ndivyo Mashahidi Wakorea walivyoanza kufanya.
Katika nchi hiyo yenye matatizo mengi ya pesa, wangetoa wapi pesa za kazi kubwa hiyo? Shahidi mmoja aliuza biashara yake akachanga pesa nyingi alizopata zitumiwe kwa ujenzi. Basi ujenzi ulipata nguvu, nayo michango iliyohitajiwa ikaletwa kwa wingi, hata jumba likawa linakaribia kumalizwa kulipiwa wakati lilipokwisha. Bila shaka roho ya Yehova ilichochea watu wake waunge mkono kwa moyo wote kazi hii ambayo ingeleta baraka za kiroho za ajabu.
Kazi ilipasa ifanywe upesi, baada ya wakati wa baridi kumalizika na kabla ya makusanyiko ya mzunguko ya wakati wa masika. Lilimalizwa baada ya miezi miwili tu! Kazi nyingi ya ujenzi ilifanywa na wenye kujitolea, nao Mashahidi walifanya kazi upesi sana hata jirani wakashangaa kama kweli walikuwa wakifuata maagizo ya kutokuwa nje usiku, wakati wa saa nne ambazo watu walikatazwa kuwa nje ya nyumba zao kwa sababu ya hatari. Lakini walikuwa wakiyafuata. Basi kazi yao ilitokeza jumba imara, lenye kung’aa na kuonekana vizuri, wanamoweza kukaa watu karibu 1,200.
Naam, linakaliwa kulingana na desturi ya Korea, na wenye kuketi wanakalia sakafu nzuri ya mbao. Siku ya kuweka wakf jumba la kusanyiko, yaani Aprili 5, wenye kuketi walisongamana kidogo nafasi ikapatikana ya kukaa watu 1,300. Walipokuwa wakiingia, kila mmoja alipewa mfuko wa viatu wa plastiki na kalamu ya wino yenye maandishi yaliyohusiana na kuwekwa wakf kwa jumba, kwa sababu watu wa nchi za Mashariki wana desturi ya kutayarisha vitu vya namna hiyo kwa ajili ya nyakati za pekee. Wote walipendezwa na jukwaa lenye kung’aa, vikuza-sauti vizuri sana, kidimbwi cha ubatizo katika orofa ya pili na bustani yenye mimea michanga mbele ya jengo, iliyopandwa mtindo wa nchi za Mashariki.
Hotuba ya wakf ilitolewa na Milton Hamilton, mmojawapo wamisionari wenye bidii waliosaidia kuanza kazi ya Yehova katika Pusan mara baada ya Vita ya Korea. Wamisionari karibu 25 walikuwa wamefanya kazi Pusan miaka mingi, nao wote wanafurahi pamoja na Mashahidi wenyeji ‘wanapoona mema kwa sababu ya kazi yao’! Mashahidi wa Yehova wa Pusan wanafurahi kuwa na Jumba la Makusanyiko hilo la kwanza huko Mashariki, nao wanamimina machozi ya furaha kuonyesha shukrani zao.—Mhu. 2:24.
[Picha katika ukurasa wa 522]
Jumba la Makusanyiko la Pusan, Korea