Kupigana Chini ya “Gogu, wa Nchi ya Magogu”
(Makala ya funzo la kitabu)
1. (a) Ni adui gani wa muda mrefu wa waabudu wa kweli ambaye hatakuwako wakati vita ya mwisho itakapotukia? (b) Ingawaje, ni nani anayezisukuma “pembe kumi” kwenda kupigana?
KUNA mshambuliaji mmoja wa zamani ambaye hatakuwako katika vita hii ya mwisho juu ya mabaki waliotiwa mafuta wa Israeli wa kiroho na wenzi wao wenye uaminifu thabiti walio sehemu ya “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wa Mchungaji Mwema. Huyo ni Babeli Mkuu, ile milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Zamani ilitumia “mkono wa Serikali” kama chombo chake cha kufanyia vita ya kiroho katika njia yenye jeuri juu ya “watakatifu” wa Yehova wanaofuata nyayo za Yesu Kristo. Mtume Yohana aliandika matendo yake yenye hatia katika Maandiko Matakatifu, alipoandika hivi: “Nikamwona yule mwanamke amelewa kwa damu ya watakatifu, na kwa damu ya mashahidi wa Yesu.” (Ufu. 17:6) Lakini sasa, kwa sababu ya kuharibiwa kwake na zile “pembe kumi,” hampandi tena yule “mnyama” mwekundu sana ili amwongoze katika njia yo yote. Hata hivyo, kuna uwezo usioonekana unaozisukuma zile “pembe kumi” zikapigane na Mwana-Kondoo kama anavyowakilishwa na wanafunzi wake waaminifu wasaliao duniani. Uwezo huo usioonekana na usio wa kibinadamu ni Shetani Ibilisi.—Ufu. 13:1, 2.
2. (a) Shetani Ibilisi atakuwa bado ana cheo gani wakati huo? (b) Maandiko yaonyeshaje kwamba Ibilisi kweli ndiye mwenye kusababisha vita vinavyofanywa juu ya waabudu wa Yehova duniani?
2 Kuharibiwa kwa Babeli Mkuu wa kidini hakukumshusha Shetani Ibilisi katika cheo cha kuwa kama Yesu alivyomwita, “mtawala wa ulimwengu huu,” au asiwe kama mtume Paulo alivyomwita, “mungu wa taratibu hii ya mambo.” (Yohana 12:31; 14:30; 16:11; 2 Kor. 4:4, NW; Ufu. 13:3, 4) Baada ya kuharibiwa kwa Babeli Mkuu, aliyekuwa ameendeleza ibada ya Ibilisi, hasira kuu yake juu ya waabudu wa Kikristo wa Yehova duniani inakuwa kali zaidi kuliko zamani. Anaongeza sana vita ambavyo amefanya wakati wote tangu kufukuzwa kwake kutoka mbinguni, vita vinavyoripotiwa kwa unabii katika maneno haya: “Joka akamkasirikia yule mwanamke [tengenezo la Mungu la kimbinguni lililouzaa ufalme wa Kimasihi], akaenda zake afanye vita juu ya wazao wake waliosalia, wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu.”—Ufu. 12:17.
3. Ufunuo 16:12-16 waonyeshaje kwamba Ibilisi na taratibu yake ya kisiasa ndio wenye kusaidia kufanywa kwa vita juu ya Mungu katika Har–Magedoni?
3 Basi sasa wafika wakati wa kutokea “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” mahali pa matukio ya ulimwengu paitwapo Har–Magedoni. Kuingiza kwa Shetani mataifa ya kilimwengu katika vita hiyo ya mwisho kwaonyeshwa, katika Ufunuo 16:12-16, ambamo mtume Yohana anaandika hivi: “Nikaona roho tatu za uchafu zilizofanana na vyura, zikitoka katika kinywa cha yule joka [Shetani Ibilisi], na katika kinywa cha yule mnyama, na katika kinywa cha yule nabii wa uongo [wale walioshauri na kuendeleza kufanywa kwa ‘sanamu’ ya kisiasa ya yule mnyama]. Hizo ndizo roho za mashetani, zifanyazo ishara, zitokazo na kuwaendea wafalme wa ulimwengu wote, kuwakusanya kwa vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi. . . . Wakawakusanya hata mahali paitwapo kwa Kiebrania, Har–Magedoni.” Hivyo taratibu ya kisiasa ya ulimwenguni pote na Mamlaka ya Ulimwengu ya Waingereza na Waamerika hufanya kazi pamoja na yule Joka katika kusaidia kufanya vita na Mungu katika Har–Magedoni.
4. (a) Sehemu ambayo Ibilisi anatimiza katika matukio hayo baada ya kuharibiwa kwa Babeli Mkuu inasimuliwa katika unabii gani? (b) Ni nani anayetajwa kama “Gogu,” na “nchi ya Magogu” ni nini?
4 Sehemu ambayo Ibilisi aliyefukuzwa anatimiza baada ya kuharibiwa kwa Babeli Mkuu katika kukusanya mabaki ya tengenezo lake la kidunia lionekanalo ili kupigana na Mwana-Kondoo wa Mungu inafananishwa waziwazi katika unabii wa Ezekieli 38:1 mpaka 39:16. Katika unabii huo yule Shetani Ibilisi aliyefukuzwa akiwa karibu na dunia anatajwa kama “Gogu, wa nchi ya Magogu.” Nchi hiyo inafananishwa ikiwa katika kaskazi ya mbali, katika “pande za mwisho za kaskazini,” na yafananisha hali ya kushushwa iliyo mbali sana na kibali ya Mungu, ujirani wa dunia yetu ambako Shetani Ibilisi na mashetani wake wamezuiwa kwa muda mfupi kabla ya kutupwa katika shimo refu la kutotenda kabisa. (Eze. 38:6, 15; 39:2; Ufu. 20:1-3) Kama Gogu wa nchi ya Magogu, Shetani Ibilisi anafananishwa kama akikusanya pamoja jeshi kubwa la vikosi kutoka kaskazini na kusini na kutoka Uajemi, mashariki ya mahali ilikokuwako wakati mmoja Babeli katika Mto Frati.
5, 6. (a) Shambulio la Gogu latukia wakati gani? (b) Ni “nchi” gani ambayo Gogu anashambulia, kama inavyotajwa katika Ezekieli 38:8, 9?
5 Wakati wa shambulio la Shetani Ibilisi kama Gogu wa nchi ya Magogu umewekwa na Yehova Mungu na watazamiwa kutukia “katika miaka ya mwisho,” “katika siku za mwisho.” (Eze. 38:8, 16) Hii inaonyesha wakati ulio karibu na mwisho wa tengenezo lionekanalo la Ibilisi duniani. Kwa hiyo yaonyesha kutukia kwa shambulio lake kama likija wakati wa muda wa kutosha baada ya kurudishwa kwa mabaki wenye kutubu wa Israeli wa kiroho kwenye hali yao ya kiroho yenye haki katika kibali ya Yehova. Hii yamaanisha miaka fulani baada ya mwaka wa 1919 W.K., wakati mabaki ya Waisraeli wa kiroho walipokombolewa kwa uwezo wa Mungu katika utumwa wa Babeli Mkuu wakarudishwa katika utumishi wake wenye uhuru wa Ufalme. Hawakurudishwa kwenye Jamhuri ya Israeli katika Mashariki ya Kati, bali kwenye hali ya kiroho iliyorudishwa ya “Israeli wa Mungu” wa Kikristo ndiko anamaanisha, anapomwambia Shetani Ibilisi, aitwaye Gogu wa nchi ya Magogu:
6 “Baada ya siku nyingi utajiliwa; katika miaka ya mwisho, utaingia nchi iliyorudishiwa hali yake ya kwanza, baada ya kupigwa kwa upanga, iliyokusanywa toka kabila nyingi za watu, juu ya milima ya Israeli, iliyokuwa ukiwa wa daima; lakini imetolewa katika kabila za watu, nao watakaa salama salimini wote pia. Nawe utapaa juu, utakuja kama tufani kama wingu kuifunika nchi, wewe, na vikosi vyako vyote, na kabila nyingi za watu pamoja nawe.”—Eze. 38:8, 9.
7, 8. (a) Shambulio hili juu ya mabaki ya Israeli wa kiroho litatukia kwa sababu gani? (b) Hali ya kiroho ya watu wa Mungu wakati huu inasimuliwaje katika Ezekieli 38:10, 11?
7 Itakuwa sababu gani ya shambulio hili la mwisho juu ya mabaki waliorudishwa wa Waisraeli wa kiroho? Itakuwa uhakika wa kwamba hali yao ya kiroho yenye ufanisi duniani chini ya baraka ya kimungu ni ushuhuda wa ulimwenguni pote wa enzi kuu ya ulimwengu wote ya Yehova Mungu. Kuongeza kwa hilo ni uhakika wa kwamba wamejitenga kwa ujasiri na ulimwengu huu wakishika kutokuwamo kabisa katika fitina za kilimwengu na hawazitegemei silaha za vita zenye kufisha za ulinzi. Pia, wanafurahia ibada na kumtumikia Yehova kwa bidii katika paradiso ya kiroho. Ndiyo sababu maneno yafuatayo yanawekwa katika kinywa cha Gogu:
8 “Nitapanda juu, niiendee nchi yenye vijiji visivyo na maboma; nitawaendea watu wanaostarehe, wanaokaa salama, wote wakikaa pasipo kuta, ambao hawana makomeo wala malango.”—Eze. 38:10, 11.
9. Mistari hiyo inayofuata katika unabii huo ina ushuhuda gani kuonyesha kwamba waabudu wa Yehova duniani wanafurahia wakati huo paradiso ya kiroho?
9 Akishuhudia paradiso ya kiroho ya waabudu wake waliorudishwa, Yehova anamwambia Gogu wa nchi ya Magogu hivi: “Ili kuteka mateka, na kuwinda mawindo; uugeuze mkono wako juu ya mahali palipoharibika, ambapo sasa panakaliwa na watu, na juu ya watu waliokusanyika toka mataifa, waliopata ng’ombe na mali, wakaao katikati ya dunia.” Ndiyo sababu watazamaji walimwengu humwuliza Gogu wa nchi ya Magogu mwenye kushambulia hivi: “Je! umekuja kuteka mateka? umekusanya jeshi lako, ili kuwinda mawindo? kuchukua fedha na dhahabu, kuchukua ng’ombe na mali, kuteka mengi sana?”—Eze. 38:12, 13.
10. Sababu gani si mali za kimwili za wakazi wa paradiso ya kiroho ndizo zinazokaribisha shambulio hili la mataifa yote?
10 Mabaki waliorudishwa wa Waisraeli wa kiroho na “mkutano mkubwa” wa wakazi wenzao wa paradiso ya kiroho hawana mali za kimwili zikilinganishwa na mali nyingi mno za kimwili na ufanisi wa Babeli Mkuu ambazo imekusanya kwa karne nyingi. Wamefuata shauri la Yesu Kristo wakautafuta kwanza ufalme wa Mungu na haki Yake kuliko mali za kimwili za ulimwengu huu wenye kupenda mno vitu vya kimwili. (Mt. 6:33) Hivyo wangekaribisha shambulio hilo la mataifa yote la majeshi chini ya amri isiyoonekana ya Gogu wa kisasa wa nchi ya Magogu kwa njia gani ya mali za kidunia?
11. (a) Hasa paradiso ya kiroho ya mashahidi wa Kikristo wa Yehova inafananisha nini, na namna gani hivyo? (b) Mataifa ya ulimwengu yamekaza moyo kufanya nini juu ya hili?
11 Si mali za kimwili, bali kile kinachofananishwa na paradiso ya kiroho ya mashahidi wa Kikristo wa Yehova ndicho kitu chenye thamani kinachokaribisha shambulio la ulimwenguni pote kwa njia ya tengenezo la kidunia lionekanalo la Shetani Ibilisi baada ya kuharibiwa kwa Babeli Mkuu. Paradiso yao ya kiroho ambayo Yehova Mungu amepanda duniani yafananisha haki ya Mungu ya kuwa na enzi kuu juu ya dunia yote. Lakini enzi kuu juu ya dunia ndiyo mataifa ya kilimwengu yanajidai kuwa haki yao, kila taifa ambalo ni mwanachama katika Umoja wa Mataifa likiendelea bado kudai enzi yake ya kitaifa. Wakazi wa paradiso ya kiroho wanafanyiza msingi wa “nchi mpya,” jamii mpya ya kidunia; kwa sababu hiyo, mataifa ya kilimwengu chini ya Gogu wa kisasa wa Magogu yanataka kuuteka msingi huo wa “nchi mpya” na kwa njia hiyo waendeleze jamii ya kale ya kidunia kwa faida zayo za kichoyo, pasipo kumtegemea Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu. Kutimiza hili kunamaanisha zaidi kuliko fedha na dhahabu na mali za kimwili kwa mataifa yenye kujitawala.
12. (a) Shambulio la majeshi ya Gogu laweza kutazamiwa kuleta matokeo gani juu ya mashirika halali yanayotumiwa na mashahidi wa Kikristo wa Yehova na mali za mashirika hayo? (b) Je! hii yamaanisha kwamba mashahidi wa Kikristo wa Yehova watakoma?
12 Wakati huo matukio duniani yatajulisha kwa nguvu kutakavyomaanisha kwa mashahidi wa Kikristo wa Yehova kuja kwa vikosi vya Gogu katika “nchi ya Israeli” baada ya kuharibiwa kwa Babeli Mkuu. Haitashangaza ikiwa matawi 96 ya Sosaiti yatafungwa hata mali zake kunyang’anywa na serikali zenye kuchukia dini. Wakati ujao utafunua litakaloyapata maelfu ya Majumba ya Ufalme ambayo mashahidi wa Kikristo wa Yehova wamejenga kuzunguka dunia ambamo hukutana ili wapate elimu ya kiroho. Yaelekea wakati huo serikali za kitaifa zilizoruhusu na kukubali kuandikishwa kwa mashirika mbalimbali ambayo mashahidi wa Yehova wanatumia kama vyombo vya kuchapia na kugawa Biblia na vitabu vya kusaidia kujifunza Biblia hazitatazamiwa kukubali au kuruhusu mashirika hayo. Lakini, serikali za kisiasa zenye uadui haziwezi kuvunja mashahidi wa Kikristo wa Yehova ulimwenguni pote, kwa maana hawa hawakufanywa kama shirika kwa sheria za “Kaisari” zilizotungwa na wanadamu katika nchi yo yote.
13. Ni kwa sababu gani serikali za kisiasa hazitaweza kuvunja “mtumwa mwaminifu mwenye akili” na baraza yake inayoongoza?
13 Vilevile, serikali za kitaifa chini ya uongozi wa Gogu wa Magogu wa kisasa haziwezi kuvunja jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ambayo Mfalme Yesu Kristo ameona kuwa yenye kutegemeka na ameiweka “juu ya vitu vyake vyote” duniani. Haziwezi kufanya hivyo, kwa maana “mtumwa” huyu, shirika, halikufanywa kamwe kwa sheria za serikali yo yote ya kisiasa ya ulimwengu. (Mt. 24:45-47; Luka 12:42-44) Jamii hii ya “mtumwa” imekuwako tangu karne ya kwanza W.K., wakati Bwana wa kifalme, Yesu Kristo, alipoianzisha, nayo imeendelea kwa bidii katika utumishi wake mpaka wakati huu na inapasishwa naye si na “Kaisari” wala Gogu wa nchi ya Magogu. Ni sawasawa, pia, na baraza inayoongoza ya Maandiko ya jamii iliyotiwa mafuta ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” Serikali za kisiasa za yule “mnyama” zikitaka zaweza kulivunja shirika la Watch Tower Bible and Tract Society la Pennsylvania na Baraza ya Wakuu yake na pia mashirika mengine ya halali ya mashahidi wa Kikristo wa Yehova katika nchi mbalimbali, lakini haziwezi kuvunja au kutangua kuwekwa kwa kitheokrasi kwa baraza inayoongoza inayowakilisha jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili.”
14. Je! litakuwa Jambo jipya kwa mashahidi wa Kikristo wa Yehova kupigwa marufuku wasiendeshe shughuli zao waziwazi?
14 Halitakuwa jambo jipya kwa mashahidi wa Kikristo wa Yehova kupigwa marufuku wasiendeshe shughuli zao za kiroho waziwazi. Katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida, kulingana na historia, Wakristo waaminifu walikutana pamoja katika mapango ya kuzikia wafu ya Milki ya Kirumi wakati ilipokuwa ikitesa kinyama. Katika karne hii ya ishirini mashahidi wa Kikristo wa Yehova wameendesha matendo yao ya kufanya wanafunzi ijapokuwa marufuku na kuharimiwa, wakifanikiwa na mpango wa kuendesha shughuli zao kisiri-siri.
15. (a) Hata wapigwe marufuku, watu wa Yehova watafanya nini, kwa sababu gani kufikiriana? (b) Je! shambulio hilo la Gogu wa Magogu litatokeza uharibifu wa paradiso ya kiroho?
15 Sasa kwa makumi ya miaka, wameendelea na ibada na utumishi wao wa Mungu wao katika nchi za Ukomunisti. Hata ikiwa, wakati wa shambulio la vikosi vya Gogu wa Magogu, inakuwa lazima wapigwe marufuku ulimwenguni pote, wataendelea kuungana. Watajaribu kupashana habari mmoja na mwenzake. Hasa wataombeana wakati watakapotawanywa wasiwe pamoja na waabudu wenzao wa Yehova. Wataendelea kufurahi katika paradiso yao ya kiroho, kwa maana wanajua kwamba kuteswa vikali mikononi mwa Gogu wa Magogu hakumaanishi wamepoteza kibali ya kimungu, ukubali na baraka. Sifa zao za kiroho zitang’aa zaidi kuliko zamani, nao hawataruhusu maisha zao za kiroho ziharibiwe na wanadamu wanaoweza kuuua mwili tu, lakini, baada ya hapo, wasiweze kumtenda zaidi Mkristo mwaminifu anayeshika ukamilifu wake kwa Yehova Mungu.—Luka 22:4; Mt. 10:28.
16. Unabii unaotolewa kupitia kwa Ezekieli waonyeshaje kwamba kutakuwako shambulio halisi chini ya Gogu wa Magogu?
16 Kadiri ambavyo Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote ataviruhusu vikosi vilivyo chini ya Gogu wa Magogu wa kisasa kuendelea, inawapasa mashahidi wa Yehova wangoje waone. Kwamba kutakuwako shambulio, unabii uliopewa kupitia kwa Ezekieli waonyesha. “Itakuwa katika siku hiyo, Gogu atakapokuja kupigana na nchi ya Israeli, asema Bwana [Yehova], ghadhabu yangu itapanda katika mianzi ya pua yangu. Kwa maana katika wivu wangu, na katika moto wa ghadhabu yangu, nimenena, Hakika katika siku ile kutakuwako tetemeko kubwa katika nchi ya Israeli; hata samaki wa baharini, na ndege wa angani, na wanyama wa kondeni, na vitu vyote vitambaavyo juu ya nchi, na wanadamu wote walio juu ya uso wa nchi, watatetemeka mbele ya uso wangu; nayo milima itatupwa chini, na magenge yataanguka, na kila ukuta utaanguka chini.”—Eze. 38:18-20.
17. Mashahidi wa Kikristo wa Yehova wataonaje watakaposhambuliwa na majeshi yenye silaha ya Gogu wa Magogu, na kwa sababu gani?
17 Wajaposhambuliwa vikali na “jeshi” la Gogu wa Magogu, mashahidi wa Kikristo wa Yehova watakuwa na usalama wa kiroho, wakiwa katika upendo wake na chini ya kibali yake. Kulingana na unabii, wakiwa ‘wanakaa salama, wote wakikaa pasipo kuta na hawana makomeo wala malango,’ waabudu hawa wa Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu hawatainua mkono katika tendo lenye jeuri juu ya majeshi yenye silaha ya Gogu wa Magogu. Watamwacha Mungu wao aonyeshe uwezo wake wenye ulinzi juu yao. Watakumbuka na kuyaamini maneno ya nabii yaliyosemwa katika shida ya shambulio linalofanana na hili juu ya waabudu wa Yehova: “Msiogope, wala msifadhaike kwa ajili ya jeshi kubwa hili; kwani vita si yenu bali ni ya Mungu.” (2 Nya. 20:15) Tumaini lao katika Mungu Mwenye Nguvu Zote halitakuwa la bure. Yeye ataifanya iwe vita Yake, maana vita hiyo kweli, si juu yao, bali ni juu ya Yeye Mungu wao. Sasa ana hasira kweli kweli, naye ana haki kabisa katika kuonyesha hasira yake!
18. (a) Ni “mahali” gani panapotajwa katika Biblia kama Har–Magedoni? (b) Katika wakati wake uliowekwa, Yehova amtumia nani afanye vita juu ya adui zake za kidunia?
18 Sasa ile “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” imefika, na ndio wakati wa “vita” hiyo itakayoonyesha siku ya kuthibitisha haki ya enzi kuu ya ulimwengu wote ya Yehova. “Mahali” hapo pa mfano, hali hiyo yenye kutokeza uadui kati ya Mungu Mwenyezi na majeshi ya Gogu, iitwayo kwa Kiebrania Har–Magedoni, imefikiwa. (Ufu. 16:14, 16) Si mashahidi wa Kikristo wa Yehova duniani, bali Yehova mwenyewe aanza vita juu ya adui za kidunia ambao sasa wamejipanga tayari kwa vita. Yehova amkonyezea Amiri-Jeshi Mkuu wake, Askari Mkuu wake Yesu Kristo. Mara anapoitikia konyezo hilo, katika jina la Yehova yeye na majeshi yake ya kimbinguni wajitia kwa nguvu vitani kana kwamba wanapanda farasi wa vita. Ile vita yenye maana ya ulimwengu wote inayofuata, na linaloyapata majeshi ya vita yaliyojipanga ulimwenguni pote chini ya Gogu wa Magogu wa kisasa, yanatolewa kwetu kwa njia ya mfano katika kitabu cha mwisho cha Maandiko Matakatifu yaliyoongozwa na Mungu.
(Itaendelezwa katika toleo litakalofuata)
—Kutoka Kitabu Man’s Salvation Out of World Distress at Hand!, sura ya 14.