Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 1/15 kur. 44-47
  • UHARIBIFU KATIKA HAR-MAGEDONI WA WAPENZI WA BABELI MKUU WALIOJITENGA

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • UHARIBIFU KATIKA HAR-MAGEDONI WA WAPENZI WA BABELI MKUU WALIOJITENGA
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 1/15 kur. 44-47

UHARIBIFU KATIKA HAR-MAGEDONI WA WAPENZI WA BABELI MKUU WALIOJITENGA

(Funzo la kitabu)

1. (a) Ni kwa njia gani peke yake mashahidi wa Yehova wa Kikristo wataweza kuokoka uharibifu wa Babeli Mkuu? (b) Bado watakuwa na kazi zaidi wakati huo ya kuzihubiri “habari njema hizi za ufalme” kwa ushuhuda? (c) Badala yake, ni hali gani itakayowakabili?

NI KWA kulindwa na Mungu Mwenye Nguvu Zote tu mashahidi wa Yehova wa Kikristo wataweza kuokoka wakati Babeli Mkuu atakapoondolewa usoni pa dunia kwa jeuri. Kwa kuwa wao wataokolewa watazame tukio hilo lenye kutikisa ulimwengu, watakuwa mashahidi wa tendo hilo “la ajabu” la Mungu wa ibada safi, na hiyo itawalazimisha waeleze wengine habari hizo baadaye. Wakati huo kazi yao ya kuhubiri “habari njema hizi za ufalme . . . katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote” itakuwa imekoma. Kazi yao ya utangazaji ya kwenda nyumba kwa nyumba, mlango kwa mlango, duka kwa duka, na katika barabara kama walivyoamriwa na Mwana wa Mungu itakwisha. (Mathayo 24:14; Marko 13:10, NW) Sasa itawapasa kusimama imara upande wa ufalme huo wa Mungu wa Kimasihi ambao wameendelea kuuhubiri wakijikaza kwa makumi ya miaka ya huu “mwisho wa taratibu ya mambo.” Kwa sababu gani? Kwa sababu sasa wataelekeana uso kwa uso na mamlaka za kisiasa zisizotaka kufuata dini, zinazowakilisha “falme zote za ulimwengu.”

2. Mamlaka za kisiasa za kilimwengu zitakata maneno gani vibaya?

2 Hali hiyo itakuwa yenye magumu sana! Mamlaka za kisiasa za kilimwengu, ambazo sasa zitakuwa zimetaliki dini yote ya Kibabeli, sasa zitabisha zaidi sana kwamba hakuna kitu kama “ufalme wa Mungu” wenye haki ya kutawala dunia. Wao hawaamini kuna serikali ya namna hiyo isiyoonekana, ya kimbinguni. Kwa sababu wataruhusiwa kuharibu milki ya ulimwengu ya Kibabeli ya dini ya uongo, hiyo itawafanya wakate maneno vibaya​—kwamba hakuna Mungu mmoja aliye hai na wa kweli na kwamba wao ni wenye nguvu zaidi kuliko cho chote kinachojidai kumwakilisha duniani na kwamba wanaweza hata kushambulia wenye kuzitangaza “habari njema hizi za ufalme” bila kuogopa kupata adhabu ya kimungu.

3. Ni jambo la akili kuamini watawala wa kisiasa wa ulimwengu watawazaje wakati huo?

3 Maoni yao yatakuwa ya kimwili kabisa, wakikumbuka mambo yaonekanayo, ya kimwili tu: Kwamba utawala wa dunia kuanzia hapo na kuendelea umepaswa kuwa wa watawala wa kibinadamu waonekanao peke yao. Kwamba dunia ni mali ya mwanadamu anayeikalia. Kwamba fundisho la kwamba wamekuwa chini ya utawala usioonekana wa Shetani Ibilisi na mashetani wake halisadikiki. Kwamba wao hawakupewa mamlaka yao ya kisiasa na Ibilisi ambaye ni mtawala asiyeonekana, nao hawakutawala dunia karne zote hizi kwa kuruhusiwa tu na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. Kwa hiyo wao hawatakubali kwamba Majira ya Mataifa yalikwisha 1914 W.K., wala hawatakubali kuachia Mungu wasiyeamini mamlaka yao ya kisiasa wala enzi kuu zao za kitaifa. Lazima wote walio hai duniani wafuate mawazo yao. Wote wasiofuata, wote wasiokubaliana nao, lazima waondolewe mbali, wafutiliwe mbali watoke duniani. Wakati waharabu wa kisiasa wa Babeli Mkuu watakaposema kuna watu wasiokubaliana nao, watakuwa wakimaanisha mashahidi wa Yehova watakaookoka.

4. Kwa sababu gani mashahidi wa Yehova hawataacha cheo chao wakati huo wafuatane na ulimwengu?

4 Jambo litakalofanya mashahidi wa Yehova wa Kikristo wasifuatane na mamlaka hizo wakati huo wa hatari ni kumtambua Mungu Aliye Juu Zaidi Yehova kama Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote. Kwa kuwa ndiye Muumba, dunia na mbingu ni mali Yake. Akiwa ndiye Mfalme-Mfanyizaji halali amemweka Mwanawe Yesu Kristo aliyemfufua atawale dunia miaka elfu kwa ajili ya wanadamu aliofia akiwa dhabihu ya ukombozi. Wakati wa utawala huo wa mileani wa Kristo umekaribia, na mashahidi wa Yehova wanaungoja wakiamini kabisa Maandiko Matakatifu. Hata hali ziweje wao hawataikana serikali hiyo ya kitheokrasi ambayo wamekuwa mabalozi na wajumbe wake duniani “wakati wa mwisho.” Hivyo hawakuwa “wa ulimwengu,” na sasa wanakataa kulazimishwa wawe wa ulimwengu unaokaribiwa na Har–​Magedoni, ambapo suala juu ya Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote litaamuliwa kabisa kwa kupigana!

5. (a) Kwa sababu ya msimamo wa mashahidi wa Yehova wa Kikristo, nia ya mamlaka za kisiasa zenye kuamini vitu vionekanavyo tu itakuwa nini juu yao wakati huo? (b) Yanayotabiriwa juu ya Gogu wa nchi ya Magogu wa nchi ya Magogu yanaonyeshaje vile maoni yao yatakavyokuwa?

5 Mamlaka za kisiasa zenye kuamini vitu vionekanavyo tu zitachukia kuzuiwa zisidai utawala wa ulimwengu. Nia yao itakuwa kukiondolea mbali kizuizi chenyewe. Tena, kikundi kidogo cha mashahidi wa Yehova wa Kikristo kina vitu gani vya kujitetea navyo isipokuwa Biblia Takatifu, kitabu tu kilichoandikwa na mkono wa wanadamu. Majeshi yao ya kuwatetea yako wapi, silaha zao za kimwili za kumpigania Mungu wao na Mfalme wao wa Kimasihi ziko wapi? Wakiwaza kama Gogu wa nchi ya Magogu katika unabii wa Ezekieli, watakata maneno kwamba mashahidi wa Yehova hawana kinga, wako hoi, kwa sababu hawana silaha wala nguvu za kisiasa. (Ezekieli 38:10-12) Kwa maoni ya kimwili, inaelekea itakuwa vyepesi sana kuwaharibu, kufutilia mbali paradiso yao ya kiroho, kuwaharibia dai lao kwamba wanawakilisha “ufalme wa mbinguni”!

6. Wakati wanachama wa Umoja wa Mataifa watakapokwenda kushambulia mashahidi wa Yehova, watakuwa wakionyesha nani hasa ukaidi wao?

6 Haya! songeni mbele mkashambulie, enyi washiriki wenye umoja wa kitaifa wa tengenezo la ulimwengu la amani na usalama wa mataifa yote! Naam, songeni mbele mkidhani mwaenda kushambulia mashahidi wenye kuokoka wa Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova; na kumbe mwaenda kushambulia Kiongozi wao wa kimbinguni, Yesu Kristo, “Mwana-kondoo wa Mungu” aliyetolewa kama dhabihu wakati mmoja! Hiyo ni kwa sababu, kwa habari ya mamlaka za kisiasa zilizolipa tengenezo la ulimwengu la kutawala wanadamu “nguvu na mamlaka” zao za kidunia, imeandikwa hivi: “Hawa watafanya vita na Mwana-Kondoo, na Mwana-Kondoo atawashinda, kwa maana Yeye ni Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa Wafalme; na hao walio pamoja naye ndio walioitwa, na wateule, na waaminifu.”​—Ufunuo 17:13, 14.

7, 8. (a) Watakapokabiliwa na shambulio hilo, watumishi wa Yehova hapa duniani watapaswa kukumbuka nyakati gani? (b) Zaburi ya 27 yawezaje kuwatia moyo?

7 Kupitia kwa maneno hayo ya unabii Yehova Mungu aonyesha wazi ana hakika mashahidi wake wa Kikristo atakaohifadhi waone wakati huo wa maana sana wakuwako kwao duniani watakuwa waaminifu. Hata shambulio liwe la namna gani ulimwenguni pote, hata lije kwa njia gani, litajaribu imani na kujitoa kwa mabaki yake yaliyotiwa mafuta na “mkutano mkubwa” wa wenzi wao waaminifu. Itawapasa kukumbuka nyakati nyingine zilizoandikwa katika Biblia Takatifu ambazo Mungu Mwenye Nguvu Zote aliacha adui washambulie kwa pamoja watu wake walioelekea kuwa hoi, lakini akawakomesha adui kwa kuwaua katika njia zao. Itawafaa wakumbuke maneno ya Mfalme Daudi:

8 “[Yehova] ni nuru yangu na wokovu wangu, nimwogope nani? [Yehova] ni ngome ya uzima wangu, nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, wanile nyama yangu, watesi wangu na adui zangu, walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, hata hapo nitatumaini. Neno moja nimelitaka kwa [Yehova], nalo ndilo nitakalolitafuta, nikae nyumbani mwa [Yehova] siku zote za maisha yangu. Niutazame uzuri wa [Yehova], na kutafakari hekaluni mwake. Mradi atanisitiri bandani mwake siku ya mabaya, atanisitiri katika sitara ya hema yake, na kuniinua juu ya mwamba. Na sasa kichwa changu kitainuka juu ya adui zangu wanaonizunguka. Nami nitatoa dhabihu za shangwe hemani mwake; nitaimba, naam, nitamhimidi [Yehova].”​—Zaburi 27:1-6.

9. Mataifa yasiyomcha Mungu yatakuwa yamempa Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote sababu gani za kuyaharibu?

9 Mbingu zote takatifu na watakatifu wote walio duniani wanatazama linalotukia sasa! Sasa hatimaye imefikiwa hatua ya mwisho ya mataifa ya dunia kukaidi kwa ufidhuli enzi kuu ya ulimwengu wote ya Mungu Aliye Juu Zaidi, Mfanya mbingu na dunia! Sasa Mdai wa kimbinguni wa Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote lazima aamue ni maoni ya nani yanayofaa, ya mashahidi wake wa Kikristo duniani au ya mataifa yenye kujitukuza ya viumbe-wanadamu wenye kufa. Si kwamba mataifa ‘yameharibu dunia’ tu kwa kuchafua na kuvunja sheria za Muumba, bali pia sasa yanajipanga yaharibu watu Wake “walio mali ya pekee.” (Ufunuo 11:18; 1 Pet. 2:9, NW) Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote anahitaji sababu gani zaidi ya kuyaharibu mataifa yasiyomcha Mungu? Hakuna!

10. (a) Mataifa yameonyeshaje kwamba yamekataa kutii shauri lililoongozwa na Mungu liandikwe katika Zaburi 2:10-12? (b) Kwa hiyo, kupatana na Zaburi 2:5-9, wakati unafika wa hatua gani kuchukuliwa?

10 Kwa ushupavu, wakati wote wa kushuhudiwa kwa ‘habari njema za ufalme’ ulimwenguni pote tangu mwaka wa 1914 W.K., mataifa yamekataa kutii shauri hili lililoongozwa na Mungu: “Na sasa, enyi wafalme, fanyeni akili, enyi waamuzi wa dunia, mwadibiwe. Mtumikieni [Yehova] kwa kicho, shangilieni kwa kutetemeka. [Mbusuni Mwana, Masihi], ili [Yehova] asije akafanya hasira nanyi mkapotea njiani, kwa kuwa hasira yake itawaka upesi.” (Zaburi 2:7, 10-12) Mataifa yameendelea kukataa kumbusu Mfalme ambaye Yehova amemtangaza katika ulimwengu wote kuwa Mwanawe mzaliwa wa pekee, kwa sababu mataifa hayakufanya lo lote kumsihi ili wapatane. Yamekataa kumwachia enzi kuu zao zinazosimamia maeneo wanayodai kuwa yao. Saa ya Mungu yaonyesha ni wakati Wake wa ‘kusema na mataifa kwa hasira yake, na kuwafadhaisha kwa ghadhabu yake.’ Kwa hiyo sasa acheni utawala wa “fimbo ya chuma” ufanye kazi. Acheni Mwana wa Yehova aliyetawazwa kuwa mfalme ayavunje mataifa, ayaponde vipande vipande kama nyungu ya mfinyanzi. (Zaburi 2:5-9) Mara moja, basi, acheni Mwana wa Mungu atie majeshi ya adui piganoni akiwa na fimbo ya chuma!

11. (a) Ni nani anayetoa ishara majeshi ya kimbinguni yaelekee kwenye Har–​Magedoni? (b) Masimulizi ya Ufunuo yanasimuliaje uwanja wa pigano siku hiyo ya machinjo?

11 Kama vile Mfalme Daudi katika uwanda wa Gibeoni alivyongoja Yehova ampe ishara ya kupigana, ndivyo Mfalme-shujaa “atakayewachunga mataifa yote kwa fimbo ya chuma” amengoja Amiri-Jeshi Mkuu wa kimbinguni ampe ishara. (Ufunuo 12:5) Tazameni! Ishara hiyo! Mara moja Jemadari Mkuu wa Kifalme afyatua farasi wake mweupe, akielekeza majeshi yake ya kimbinguni yaliyopanda farasi weupe wa vita kufukuza na kushinda adui wote walioungana kupigana naye katika uwanja wa Har–​Magedoni duniani. Waone wafalme hao maadui na majeshi yao na wafuasi wao kama zabibu zilizokusanywa zipondwe. Uone uwanja huo wa Har–​Magedoni kama shinikizo la mvinyo! Hapo mwache Mfalme wa wafalme akanyage “shinikizo la mvinyo ya ghadhabu ya hasira ya Mungu Mwenyezi.” Acha damu yenye uhai ya “zabibu” hizo iinuke zaidi na zaidi katika pipa la shinikizo, naam, “mpaka kwenye hatamu za farasi.” (Ufunuo 19:11-16; 14:18-20) Acha hasira ya ghadhabu ya Mungu aliyokuwa ameifungia muda mrefu ijitokeze kabisa. Asiwe na haja tena ya kuleta taabu kama hiyo ya mataifa wakati mwingine.​—Nahumu 1:6-9.

12. Isaya 34:1-6 yaelezaje litakalotukia wakati huo?

12 Hakika huu ndio wakati wa mbingu zote na dunia kuangalia! “Maana [Yehova] ana ghadhabu juu ya mataifa yote, na hasira kali juu ya jeshi lao lote; amewaangamiza kabisa, amewatoa waende kuchinjwa. Watu wao waliouawa watatupwa nje, na uvundo wa maiti zao utapaa juu, na milima itayeyushwa kwa damu yao. Na jeshi lote la mbinguni litafumuliwa, na mbingu zitakunjwa kama karatasi, na jeshi lao lote litanyauka kama vile jani la mzabibu linyaukavyo na kupukutika, na kama jani la mtini linyaukavyo na kupukutika. Maana upanga wangu umekunywa na kushiba mbinguni; tazama, utashukia Edomu, na juu ya watu wa laana yangu, ili kuwahukumu. Upanga wa [Yehova] umeshiba damu.” (Isaya 34:1-6) Yehova hakuongoza maneno hayo ya unabii yaandikwe akicheza tu. Wakati wa kutimizwa kwayo wakaribia. Lazima taratibu ya mambo ya zamani ife!

13. Kila mmoja wetu sasa akabiliwa na uamuzi gani wa haraka?

13 Je! sisi tutakufa pamoja na taratibu ya mambo ya zamani? Je! tunachagua kuuawa pamoja na watawala wa kisiasa, majeshi yao na wafuasi wao katika “siku” hiyo wakati Yehova Mungu atakapotumia Mwanawe shujaa Yesu Kristo kupunga upanga wake wa hukumu aue adui wote duniani? Bila shaka wakati ni mfupi sana tulioruhusiwa kufanya uamuzi wa kipekee unaoonyesha kama tutapata uzima au mauti wakati Bwana Mungu Mwenye Enzi Kuu amalizapo mambo yake na taratibu hii ya mambo ya zamani. Kama tutaachiliwa hai au kama tutauawa kama walimwengu waliohukumiwa itategemea tunachagua sasa kusimama upande gani. Huu ndio wakati wa kuamua ulizo hili, Mimi nitajikuta upande wa nani taabu kuu ya ulimwengu ifikiapo upeo wa kuogofya? Kwa hekima na akili nzuri sote na tuchague uzima katika taratibu mpya ya mambo ya Mungu!

​—Kutoka Kitabu Man’s Salvation Out of World Distress at Hand!, sura ya 18.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki