Je! Unakumbuka?
Je! umesoma matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi kwa uangalifu? Ikiwa ndivyo, bila shaka utayakumbuka mambo haya:
● Unabii wa Simeoni ulitimizwaje aliposema kwamba Mariamu ‘angeingizwa upanga moyoni mwake’?—Luka 2:35.
Mariamu alihuzunika sana watu wengi walipomkataa Yesu. Lakini, wakati alipopigiliwa misumari katika mti kama mhalifu mbaya zaidi, Mariamu alijisikia kama kwamba upanga umeingizwa moyoni mwake.—M 1/1/78 10.
● Kwa sababu gani si lazima shauri lililo katika 1 Wakorintho 11:4-6, linalosema mwanamume asali bila kufunika kichwa na mwanamke afanye hivyo akiwa amefunika kichwa, lihusu sala za watu bi nafsi?
Shauri lililo katika 1 Wakorintho 11:4-6 linahusu mikutano ya kundi, kwa hiyo linahusu sala ya watu wengi. Jambo hilo liko wazi kwa sababu kutabiri (kutoa unabii) kunatajwa pamoja na sala. Ni wazi kwamba mtu hawezi kutoa unabii akiwa pekee katika chumba chake anamotolea sala.—M 9/1/77 406, 407.
● Ili kuamua uhalali wa ndoa, je! uamuzi wa wakuu wa serikali peke yake ndio utakaofuatwa?
Hapana. Maoni ya wakuu wa serikali yanatofautiana nchi na nchi. Huenda hata yakawa yanapingana. Nyakati nyingine maoni ya wakuu wa serikali yanatofautiana na Biblia. Kwa Wakristo wa kweli, mamlaka iliyo kamili ni kanuni ya Mungu ya ndoa iliyowekwa katika Neno lake.—M 8/15/77 376, 377, 380.
● Katika Ezekieli 31:4, ni nini kinachofananishwa na ‘maji yaliyousitawisha mwerezi wa mfano katika Lebanoni’?
Katika Maandiko, maji yanafananisha ‘jamaa, makutano na mataifa.’ (Ufu. 17:1, 15) Kwa hiyo, maji hayo yanafananisha watu au nguvu na mali za kibinadamu zinazosaidia mwerezi wa mfano.—M 10/1/77 446, 447, 451.