Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Matendo 12:15 yamaanisha nini wakati inapotaja habari ya mtume Petro na kusema: “Ni malaika wake”?
Hatuwezi kuwa na hakika, kwa maana masimulizi hayaendelei kueleza maana. Lakini pengine aliyesema hayo alikuwa akifikiria malaika mtakatifu mwenye kumsimamia Petro, anayeitwa na wengine “malaika mlinzi.”
Herode Agrippa wa Kwanza alikuwa amemkamata Petro akamtia gerezani. Mtume alikuwa huko akiwa “amefungwa minyororo miwili; walinzi mbele ya mlango.” Usiku malaika wa Yehova alimfungua Petro naye akaenda nyumbani kwa Mariamu, mama ya Yohana Marko.—Matendo 12:3-12.
“Naye alipobisha kilango cha lango, kijakazi, jina lake Roda, akaja kusikiliza. Alipoitambua sauti ya Petro, hakulifungua lango, kwa ajili ya furaha, bali alipiga mbio, akaingia ndani akawaambia kwamba Petro anasimama mbele ya lango. Wakamwambia, Una wazimu. Lakini yeye akakaza sana, akasema ya kwamba ndivyo hivyo. Wakanena, Ni malaika wake.”—Matendo 12:13-15.
Roda, ambaye yaelekea alikuwa Mkristo, alikuwa anamfahamu Petro. Labda wanafunzi walikataje maneno kwa sababu ya habari ya furaha na ajabu aliyowaeleza?
Neno la Kigiriki lililotumiwa hapo, aggelos, lamaanisha kwa halisi “mjumbe.” Ingawa nyakati nyingine hutumiwa kwa mjumbe wa kibinadamu, ndilo neno linalotumiwa katika Biblia kumaanisha mjumbe wa kiroho, malaika, kutoka mbinguni. (Yak. 2:25; Gal. 1:8) Kwa sababu linaweza kutumiwa kwa njia mbili, wafafanuzi wengine wamesema kwamba wanafunzi walimaanisha kwamba hapo langoni alikuwapo mtu aliyekuwa ametumwa na Petro kutoka gerezani alete ujumbe, akiwa mjumbe wa kibinadamu. Lakini, hilo latiliwa mashaka, kwa maana ikiwa Petro alikuwa amelindwa sana hivyo, angewezaje kutuma mjumbe? Tena maoni hayo hayawezi kueleza sababu gani Roda aliitambua sauti hiyo kuwa ya Petro.
Wafafanuzi wengine wa Jumuiya ya Wakristo wametoa maoni ya kwamba labda wanafunzi walidhani Petro alikuwa amekufa na hicho kilikuwa “kivuli” chake. Hata hivyo, hayo hayawezi kuwa maelezo ya kweli, kwa maana wanafunzi hao walijua kwamba mwanadamu hana nafsi isiyokufa inayoweza kuokoka mwili ufapo; yeye ni nafsi.—1 Kor. 15:45.
Namna gani mjumbe wa kiroho, malaika? Mungu alikuwa ametumia malaika mara nyingi alipokuwa akishughulika na waabudu wake na kuwaongoza. Kwa mfano, Yakobo alitaja habari za “Malaika aliyeniokoa na maovu yote.” (Mwa. 48:16) Wayahudi walijua hivyo. Vilevile, inaonekana kwamba imani ilikuwa imeenea kote kwamba malaika alipewa mgawo wa kulinda kila Mwisraeli, awe namna fulani ya malaika mlinzi, ingawa imani hiyo haikutegemea Biblia moja kwa moja.
Hatuwezi kusema kadiri ambavyo Wakristo hao Wayahudi waliokuwa nyumbani kwa Mariamu walijua jambo hilo au walivyolikubali, lakini ni wazi waliyajua maneno aliyosema Yesu juu ya wafuasi wake: “Angalieni msidharau mmojawapo wadogo hawa; kwa maana nawaambia ya kwamba malaika zao mbinguni sikuzote huutazama uso wa Baba yangu.” (Mt. 18:10) Kwa hiyo, baada ya kuacha kustaajabu, labda wanafunzi walikata maneno kwa makosa kwamba Yehova alikuwa ametuma malaika mjumbe kuwakilisha Petro na hata akasema kwa sauti kama yake.