Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
● Mungu alikuwa na maana gani alipomwambia Yona kwamba mji wa Ninawi ulikuwa na watu zaidi ya 120,000 “wasioweza kupambanua katika mkono wao wa kulia na mkono wao wa kushoto”?
Yehova Mungu alimtuma nabii Yona aende Ninawi kutangaza kwamba mji huo ulikuwa ukikaribia kuangamizwa. Ndipo watu wote walipotubu, kwa hiyo Mungu akaamua kuuachilia mji huo. Yona alisikitika sana kuona hivyo, naye Mungu akamwuliza: “Mimi, je! haikunipasa kuuhurumia Ninawi, mji ule mkubwa; ambao ndani yake wamo watu zaidi ya mia na ishirini elfu, wasioweza kupambanua katika mkono wao wa kulia na mkono wao wa kushoto; tena wamo wanyama wa kufugwa wengi sana?”—Yona 4:11.
Wafafanuzi fulani wameelewa kutokana na maneno hayo kwamba walikuwamo watoto 120,000 mjini (labda walio chini ya miaka mitano au saba), kwa hiyo wanakadiri kwamba mji huo ulikuwa na jumla ya wakaaji 600,000. Wafafanuzi hao wanautaja wakati ambao Mungu alimwambia Musa kwamba watu wa pekee ambao wangeiingia Nchi ya Ahadi ni “wadogo wenu” au “wana wenu, wasiokuwa leo na maarifa ya mabaya wala mema.” (Kum. 1:39) Vilevile, imesemekana kwamba ikiwa Yehova alikuwa na nia ya kuuachilia Sodoma kama wangalipatikana watu kumi tu wenye haki, bila shaka rehema yake ingemwongoza aliachilie jiji lenye watoto 120,000 ambao hawakuwa wamejua kupambanua mkono huu na huu.—Mwa. 18:22-32.
Lakini, jambo la kufahamu ni kwamba hata vijana wa kufika miaka kumi na tisa walikuwa kati ya wanaotajwa kuwa “wadogo wenu” katika Kumbukumbu la Torati 1:39. (Hes. 14:29) Tena, katika Yona 4:11 wale watu 120,000 hawakuitwa “wadogo” bali adam, ambalo ni neno la Kiebrania linalomaanisha “wanadamu.” Vilevile, ni hakika kwamba Sodoma ulikuwa na watoto zaidi ya kumi; kwa hiyo, Mungu alikuwa na maana ya kwamba kama wangalipatikana watu kumi wazima, wenye haki, angaliuachilia mji huo. Basi, labda katika Yona 4:11 Yehova alikuwa akisema kwamba Waninawi wasiokuwa wanaweza kupambanua mkono wao wa kulia na wa kushoto walikuwa jumla ya wanadamu 120,000.
Kwa kusema hivyo Mungu hakumaanisha kwamba walikuwa wapumbavu sana akilini hata wasiweze kutofautisha mikono yao miwili, kwa maana vitu fulani vimechimbuliwa katika ardhi kuonyesha kwamba Waninawi walifanya mambo ya ufundi. Bali, Mungu alikuwa akimaanisha kwamba Waninawi hawakuwa na kanuni nzuri ya kuamulia mema na mabaya kulingana na maoni Yake. Yona alipowaeleza ujumbe wa Mungu, wakati huo waliweza kupambanua mema na mabaya kisha wakatubu, wakayaacha mabaya.