Kuwa Mwenye Busara Kunafaidi
Asubuhi moja mhubiri wa Ufalme katika Orotava, Kisiwa cha Tenerife alitembelea nyumba moja naye mwanamume mmoja aliyekuwa na usingizi mwingi akamfungulia. Shahidi huyo alipoona kwamba alikuwa amemwamsha kutoka kwa usingizi aliomba msamaha na kwa kifupi akamtolea magazeti ya Kikristo, ambayo yalikubaliwa.
Baadaye, Shahidi huyu wa kike pamoja na mumewe walimtembelea yule mwanamume, aitwaye Isidro. Yeye alitaja kwamba, ijapokuwa alikuwa akisoma Biblia mara kwa mara, hakuweza kuifahamu. Isidro alikubali kuchukua nakala ya kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele.
Ijapokuwa mwanzoni Isidro hakuwa na kitu cho chote katikati ya kurasa za Biblia yake wakati wale Mashahidi wawili walipomtembelea mara ya kwanza, waliporudi mara ya pili waliona kwamba Biblia yake pamoja na kitabu Kweli vilijaa picha za kidini katikati ya kurasa. Wakati wa mazungumzo, mojawapo ya zile picha ilianguka chini. Huyo Shahidi aliyekuwa amemtembelea aliichukua, akaiwekelea juu ya meza.
Baadaye, Isidro alimwambia yule Shahidi kwamba huo Ulikuwa mtego, kwa kuwa alikuwa amesikia kwamba Waprotestanti walichoma moto picha za kidini walipotembelea nyumba za watu. Bila Shaka, Mashahidi wa Yehova si Waprotestanti, walakini Isidro kwa wazi alitaka kujua wangefanya nini? Walakini, baada ya kujifunza sura fulani katika kitabu Kweli, wao wenyewe, Isidro na mke wake waliondoa vitu vyote vya ibada ya uongo nyumbani mwao.
Lakini, kabla ya muda mrefu kupita, Isidro pamoja na mke wake walikuwa wamefanya maendeleo ya kiroho nao walikuwa wakifanya mipango wabatizwe wawe Wakristo wa kweli. Vilevile, kupitia kwa jitihada zao watu sita katika watu wa ukoo wao walianza kujifunza Biblia. Watatu walikuwa wakizungumza Biblia na Isidro mwenyewe—yule mtu mwenye busara aliyekuwa ameamshwa kutoka katika usingizi mzito asubuhi moja na kufaidika kwa kutendewa kwa busara.