Yehova Ndiye “Msikiaji wa Sala”
Mtunga zaburi Daudi alimwita Yehova “Msikiaji wa sala,” nao ushuhuda ni mwingi unaoonyesha kwamba, kwa kweli, anajibu sala ya bidii. (Zab. 65:2, NW) Mfano wenye kutokeza juu ya jambo hili ni maono haya yanayofuata kutoka Ureno:
Mwaguzi wa kike aliyehitimu alikuwa mwenye kuheshimiwa sana na rafiki zake pamoja na wote waliomjua. Walakini ndoa yake ilikuwa imeharibika, na mwishowe mumewe alimwacha kwa sababu alikuwa mume mwasherati. Kwa kuwa alikuwa mwanamke mwenye kufuata sana dini, siku moja mwaguzi huyu wa kike alisali kwa bidii sana kwa kukata tamaa, akionyesha kwamba alitamani sana maisha yenye furaha na kumsihi Mungu amwonyeshe kama ana kusudi lenye kufaa.
Alasiri iyo hiyo, Mashahidi wa Yehova walifika mlangoni pa mwanamke huyu walipokuwa wakishiriki katika utendaji wao wa kuhubiri nyumba kwa nyumba. Alikuwa ndipo tu amemaliza kuoga mwili naye alikuwa angali anavalia mavazi yake ya kuogea. Walakini, hata kutokana na maneno machache ya utangulizi yaliyosemwa na mmoja wa wale Mashahidi, mwaguzi huyu wa kike aliona kwamba sala yake ilikuwa imejibiwa. Kwa hiyo aliwakaribisha Mashahidi hawa mume na mke nyumbani kwake, akauliza maulizo mengi na kufurahia majibu ya Kimaandiko. Funzo la Biblia lilianzishwa, naye mwanamke huyu akaanza upesi kuhudhuria mikutano kwa ukawaida.
Baada ya muda kupita, mwaguzi huyu wa kike akawa mtangazaji wa “habari njema” yeye mwenyewe na alikuwa akiongoza funzo la Biblia. Kabla ya muda mrefu kupita, alikuwa akipanga kubatizwa katika kuonyesha wakf wake kwa Yehova, “Msikiaji wa sala.”