MATENDO HODARI YA KALE KUPITIA KWA ROHO TAKATIFU
(Funzo la Kitabu)
1. Roho takatifu iliyotumiwa kuandika Biblia imejionyeshaje kuwa yenye nguvu zaidi kuliko upanga wa viongozi wenye nguvu wa kijeshi?
1 Mtu ye yote asidharau maandiko matakatifu yaliyotokezwa na roho takatifu. Kalamu iliyoongozwa na roho takatifu ya Mungu iliyoshikwa na waandikaji wa Biblia imekuwa yenye nguvu zaidi kuliko upanga wa Kaisari, wa Napoleon Bonaparte, wa Adolf Hitler. Kwa kweli, roho takatifu imeweza kutimiza mambo ya kustaajabisha zaidi kuliko kuandika kwa kalamu ya wino. Watu wa kale wameandikwa kwamba walifanya mambo ya uhodari kwa kutumia nguvu hii hodari itokayo kwa Mungu Mwenye Nguvu Zote asiyeonekana.
2, 3. (a) Wakati Musa aliponyosha fimbo juu ya Bahari ya Shamu, nguvu hizo nyingi mno zilizotenganisha maji ya bahari zilitoka wapi? (b) Isaya 63:11-14 yahakikishaje jibu sahihi?
2 Kwa mfano, na tumchukue mwandikaji wa vitabu vitano vya kwanza vya Biblia, Musa. Huko nyuma mwaka wa 1513 K.W.K., alisimama katika ukingo wa magharibi wa Bahari ya Shamu. Alinyosha fimbo iliyokuwa katika mkono wake wa kuume juu ya bahari hiyo. Tazama! Maji yakajitenga na kuacha Waisraeli wavuke kabla Wamisri wenye kuwafuata hawajawafikia. Je! Musa alifanya mwujiza huo kwa nguvu nyingi mno zake? Haiwezekani! Hazikuwa za nabii Musa, bali kwa Chanzo cha mbinguni cha nguvu zote zilizo nyingi mno ndiko ilikotoka nguvu isiyozuilika iliyoweza kutenganisha maji yaliyokuwa yamezuia Waisraeli wasiokoke hatari kuu. (Kut. 14:21 mpaka 15:21) Kwa hiyo leo, wakati watu wa Yehova wanapotiwa adabu na kujikuta matatani, huo ndio wakati barabara wa kulikumbuka tendo la kale la Yehova na kuuliza hivi:
3 “Yuko wapi yeye aliyewapandisha toka baharini pamoja na wachungaji [Musa na Haruni] wa kundi lake? Yuko wapi yeye aliyetia kati yao [roho yake takatifu]? aliyewaongoza kwa mkono wake mtukufu [wenye nguvu], kwa mkono wa kuume wa Musa? aliyeyatenga maji [ya bahari] mbele yao, ili ajifanyie jina la milele? aliyewaongoza vilindini, kama farasi jangwani, wasijikwae? Kama ng’ombe washukao bondeni, [roho ya Yehova ikawastarehesha]; ndivyo ulivyowaongoza watu wako, ili ujifanyie jina lenye utukufu.”—Isa. 63:11-14.
4. Vivyo hivyo, Mungu huyo anakaribiaje kujifanyia “Jina lenye utukufu” katika karne yetu ya 20?
4 Mistari hiyo ya unabii wa Isaya yaelekeza nyuma wakati watu wa Musa walipokombolewa na utumwa wao kwa Wamisri wa kale. Huko, katika masika ya mwaka 1513 K.W.K., Mungu alijifanyia jina lisiloweza kutoweka, jina lisilo na kifani cha uzuri wake. Lakini sasa, pia, katika karne yetu ya 20, wakati umefika wa Mungu ‘kujifanyia jina lenye utukufu.’ Atafanya ukombozi mkubwa zaidi unaofanana na ule alioufanya katika Bahari ya Shamu. Wenye furaha watakuwa watu wote ambao wakati huo jina la Mungu Yehova litakuwa ‘tukufu’ kwao.
5. Kama inavyoonyeshwa katika Waebrania 11:29, ni kulingana na sifa gani ya Musa mambo hayo yalitukia’
5 Kwa hiyo na tusidharau nguvu nyingi mno za nguvu ya utendaji ya Yehova iliyo takatifu. Ina nguvu leo sawa na ilivyokuwa karne 35 zilizopita. Nabii Musa hakudharau uwezo wa nguvu hiyo. Alikiamini Chanzo cha Kimungu cha roho yenye kufanya miujiza. Kulingana na imani ya Musa ndivyo mambo yalivyotukia: “Kwa imani wakapita katika Bahari ya Shamu, kama katika nchi kavu; Wamisri walipojaribu kufanya vivyo wakatoswa.” (Ebr. 11:29) Kwa njia hiyo ilionyeshwa kwamba Mungu huwathawabisha wale wanaomwamini. (Ebr. 11:6) Angalia tena yaliyoandikwa katika Hesabu 11:16, 17, 24-29 juu ya Musa mwaminifu na roho hiyo.
6, 7. (a) Kwa sababu gani bila shaka watu hao wa kale waliomwamini Mungu walikuwa na kiasi fulani cha roho takatifu? (b) Ni wanaume gani watatu wenye imani wanaotajwa katika Waebrania 11:4-7, na hapo wanasemwa kuwaje?.
6 Imani ni sehemu ya “matunda ya roho.” Ndivyo Wagalatia 5:22, 23, NW inavyosema. Ni wazi kwamba wale wanaomwamini Mungu lazima wawe na kiasi fulani cha roho yake. Orodha fupi ya wanaume na wanawake wenye imani wa kale tumepewa katika Waebrania, sura ya 11. Wao ni sehemu ya ‘wingu kubwa la mashahidi wanaotuzunguka.’ (Ebr. 12:1) Orodha ya mashahidi yarudi nyuma mpaka kwa shahidi wa kwanza wa Yehova Mungu anayeripotiwa, yaani, Habili, ndugu mdogo wa Kaini mwana wa Adamu na Hawa. Walikuwako mashahidi wengine wa Yehova siku hizo kabla ya gharika ya dunia yote iliyotokea 2370-2369 K.W.K. Majina ya mashahidi watatu wa Mungu Aliye Juu Zaidi walioishi kabla ya gharika yalitolewa katika Waebrania 11:4-7. Twasoma hivi:
7 “Kwa imani Habili alimtolea Mungu dhabihu iliyo bora kuliko Kaini; kwa hiyo alishuhudiwa kuwa ana haki; Mungu akizishuhudia sadaka zake, na kwa hiyo, ijapokuwa amekufa, angali akinena. Kwa imani Henoko alihamishwa, asije akaona mauti, wala hakuonekana kwa sababu Mungu alimhamisha: maana kabla ya kuhamishwa alikuwa ameshuhudiwa kwamba amempendeza Mungu. Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao. Kwa imani Nuhu akiisha kuonywa na Mungu katika habari ya mambo yasiyoonekana bado, kwa jinsi alivyomcha Mungu, aliunda safina, apate kuokoa nyumba yake. Na hivyo akauhukumu makosa ulimwengu, akawa mrithi wa haki ipatikanayo kwa imani.”
8. Kutokana na mambo ya hakika, kwa sababu gani ni wazi kwamba kila mmoja wa wanaume hao watatu alikuwa na kiasi fulani cha roho takatifu?
8 Habili, Henoko na Nuhu wanatajwa kwa njia ya pekee kwa sababu walionyesha imani zaidi. Halafu, alikuwako mke wa Nuhu na wana wake watatu na binti wakwe zake walioingia katika safina pamoja na Nuhu wakaokolewa kupita gharika ya dunia yote. (1 Pet. 3:19, 20) Bila shaka Habili alikuwa na kiasi fulani cha roho takatifu, kwa maana alikuwa na mojwapo la matunda yake, yaani, imani. Hakuwezi kuwa na shaka kwamba Henoko mwana wa Yaredi pia alikuwa na kiasi fulani cha roho takatifu, kwa maana, kulingana na tunayoambiwa na Yuda 14, 15, Mungu alimtumia Henoko kutoa unabii wa kwanza ulioandikwa uliopata kutolewa na mwanadamu. (Mwa. 5:18-24) Nuhu alitumiwa pia kama nabii wa Yehova. Alikuwa “muhubiri wa haki.” (2 Pet. 2:5, ZSB; Mwa. 9:24-29) Ni nani awezaye kukana kwamba Nuhu hakufanya tendo hodari katikati ya ulimwengu wa watu wasiomcha Mungu? Hata hivyo, hakulifanya kwa nguvu zake mwenyewe. Nguvu ya utendaji iliyo takatifu ya Mungu ilimwongoza.
9, 10. (a) Ni sifa gani ya Mungu iliyokuwa ikitumiwa safina ya Nuhu ilipokuwa ikijengwa? (b) Kulingana na Mwanzo 6:1-3, Mungu alikuza nia afanye nini, na kwa sababu gani?
9 Katika siku za Nuhu roho ya Mungu ilikuwa ikitenda kazi pia juu ya wanadamu. Wakati huo wa kujenga safina “uvumilivu wa Mungu” ulionekana. (1 Pet. 3:20) Mungu alikuwa akijiweza, akivumilia, hiyo ikatoa nafasi wanadamu wapotovu watubu walipoona safina ikiendelea kujengwa na kumsikia Nuhu ‘akihubiri haki.’ Lakini ni nani walioitikia utendaji wa roho ya Mungu? Ni Nuhu na mkewe na wana wao Shemu, Hamu, na Yafethi pamoja na wake zao watatu peke yao. Mungu hakukusudia kujitahidi mno kwa ajili ya wanadamu kwa wakati usiojulikana, Mwanzo 6:1-3 watuambia uamuzi aliofanya Mungu na hali zilizokuwako duniani zikamfanya aufanye:
10 “Ikawa wanadamu walipoanza kuzidi usoni pa nchi na wana wa kike walizaliwa kwao, wana wa Mungu waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wo wote waliowachagua. [Yehova] akasema, Roho yangu haitashindana na mwanadamu milele, kwa kuwa yeye ni nyama; basi siku zake zitakuwa miaka mia na ishirini.”
11. Wakati ulipokwisha, Mungu angefanya nini kuwapa wanadamu mwanzo mpya?
11 Ndoa hiyo ya watu wenye asili mbali-mbali, “wana wa Mungu” wa kweli na “binti za wanadamu” ilikuwa ya kutisha looo! Tukio hilo halikupaswa kuendelea kwa wakati usiojulikana! Ndivyo Mungu alivyoamua. Kwa hiyo roho yake ingesubiri wanadamu miaka mingine 120 tu. Wakati ambapo muda huo ungemalizika, angeleta badiliko la ajabu! Angeacha kujizuia alivyokuwa amefanya muda mrefu. Ndoa kati ya malaika Waliovaa miili na wanawake wenye nyama ingekomeshwa na gharika ya dunia yote ambayo ingefunika hata vilele vya milima! Nuhu na jamaa yake ya wanadamu safi, wasiochafuliwa wangepita gharika hiyo wakiwa wameelea majini katika safina isiyopenywa na maji, wawape wanadamu mwanzo mzuri. Ulimwengu huo wa watu wasiomcha Mungu usingeruhusiwa tena kuudhi, kuhuzunisha roho ya Mungu. Asingekosa kuwaadhibu.—Angalia Waefeso 4:30; Isaya 63:10; Waebrania 10:29.
12, 13. (a) Zaidi ya karne nane baada ya Nuhu kujenga safina, ni mpango gani mwingine wa ujenzi ambao Mungu aliunga mkono? (b) Safina ya Nuhu ilikuwa na ukubwa gani ikilinganishwa na hema takatifu na nyua zake?
12 Hivyo Mungu alitumia waokokaji wenye kumcha yeye wa wanadamu wasio na uzaliwa wa michanganyiko kuipa jamaa ya kibinadamu mwanzo mpya, wenye haki, Kwa kusudi hilo Mungu aliunga mkono ujenzi wa Nuhu. Zaidi ya karne nane baadaye Mungu aliunga mkono ujenzi mwingine wa maana. Katika orodha ya sheria aliyompa nabii Musa juu ya Mlima Sinai, Mungu aliagiza hema takatifu ijengwe.
13 Katika hema hii takatifu ya kukutania makabila 12 ya wafu wa Musa, taifa la Israeli, walipaswa kukutana kwa kawaida pamoja na Mungu wao, na makuhani wake walipaswa kutumikia kutoa dhabihu zenye kulipia dhambi za taifa lote. Hema hiyo na ua wake uliokuwa ndani haikuwa jengo kubwa kama safina ya Nuhu. Safina ya Nuhu ilikuwa kubwa sana hata ingeweza kuchukua nyua tisa, nyua tatu za hema katika kila mojawapo ya orofa tatu za safina ya Nuhu. Ujenzi wa safina ya Nuhu ulihitaji ufundi mwingi wa mitambo, naye Mungu aliweza kumpa Nuhu na wanawe ufundi huo. Hema ya Israeli ilihitaji ufundi mwingi.
14. Ni kwa njia gani iko wazi kutokana na Kutoka 31:1-6 kwamba Mungu aliunga mkono ujenzi wa hema kwa roho yake?
14 Kwa kuwa Mungu aliagiza hema ya ibada ya Israeli ijengwe, aliunga mkono ujenzi wake. Kwa njia gani? Fungua Kutoka 31:1-6 upate jibu na kuona mitajo ya nguvu ya utendaji ya Mungu:
“[Yehova] akanena na Musa, na kumwambia, Angalia, nimemwita kwa jina lake Bezalell mwana wa Uri, mwana wa Huri, wa kabila ya Yuda; nami nimemjaza roho ya Mungu, katika hekima, na maarifa, na ujuzi, na mambo ya kazi ya kila aina, ili abuni kazi za ustadi, kuwa fundi wa dhahabu, na wa fedha, na wa shaba, na kukata vito kwa kutiwa mahali, na kuchora miti, na kufanya kazi ya ustadi iwayo yote. Tena, tazama, nimemchagua, awe pamoja naye, huyo Oholiabu, mwana wa Ahisamaki, wa kabila ya Dani; nami nimetia hekima katika mioyo ya wote wenye moyo wa hekima, ili wapate kufanya vyote nilivyokuagiza.”
Hivyo fundi mkuu Bezaleli alijawa na roho ya Mungu.
15, 16. (a) Ni utendaji wa kitu gani kitokacho kwa Mungu uliokamilisha hema kwa wakati wake? (b) Ni wakati gani na kwa njia gani Bezaleli na Oholiabu waliona kibali ya Mungu juu ya kazi yao?
15 Kwa kuwa nguvu hizo nyingi za Chanzo cha nguvu zote zilizo nyingi mno ziliongoza wafanya kazi, ujenzi wa hema takatifu na vifaa vyake vyote bila shaka ungemalizwa. Mwishoni mwa mwaka mfupi vitu vyote vilikuwa tayari kukusanywa, nayo hema ilikuwa tayari kusimamishwa. Kutoka 38:22, 23 yaeleza jambo hilo lenye kusisimua, ikisema: “Na Bezaleli mwana wa Uri, mwana wa Huri, wa kabila ya Yuda, akafanya yote [Yehova] aliyomwagiza Musa. Na pamoja naye alikuwa na Oholiabu, mwana wa Ahisamaki, wa kabila ya Dani, aliyekuwa fundi wa kuchora nakshi, mfanyaji wa kazi mwerevu, naye alikuwa mwenye kutia taraza za nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na nyekundu, na kifani nzuri.” Bila shaka siku ya kwanza ya mwaka mpya mfupi (Nisani 1, 1512 K.W.K.) ilifurahisha mioyo ya Bezaleli na Oholiabu. Siku hiyo “maskani ya hema ya kukutania” ilisimamishwa kwa amri ya Yehova, nao Bezaleli na Oholiabu wakaona mwujiza:
16 “Ndipo lile wingu likaifunikiza hema ya kukutania, na huo utukufu wa [Yehova] ukaijaza maskani.” Kwa Bezaleli na Oholiabu huo ulikuwa ushuhuda kwamba walifanya kazi yao vizuri na kwamba Yehova aliikubali. Roho yake ilikuwa imetenda kazi kupitia kwao.—Kut. 40:1-34.
17, 18. (a) Hema hiyo ilitimiza kusudi la Mungu kwa muda gani! (b) Ni kwa njia gani iko wazi kwamba roho takatifu iliunga mkono kujengwa na kukamilishwa kwa hekalu la Sulemani!
17 Maskani hiyo ya hema ya kukutania ilidumu ikitimiza kusudi lake kwa miaka 485, mpaka Mfalme Sulemani alipomaliza kujenga hekalu Yerusalemu mwaka 1027 K.W.K. na kulizindua litumiwe kwa ibada ya Mungu.
18 Ujenzi wa hekalu hilo lililojengwa na Sulemani mwana wa Daudi uliungwa mkono pia na roho ya Mungu, kwa maana Daudi alipewa habari za michoro ya jengo hilo jipya na Mungu. Ni kama vile 1 Mambo ya Nyakati 28:11-19 inavyosema: “Hayo yote, akasema Daudi, yamenielea kwa maandiko kutoka kwa mkono wa [Yehova], naam, kazi zote za mfano huu.” Wakati hekalu hilo lenye fahari lilipozinduliwa juu ya Mlima Moria katika Yerusalemu, Yehova alionyesha amelikubali jengo hilo jipya litumiwe kwa ibada yake: nyumba ya [Yehova], hata makuhani hawa-“Ndipo nyumba ikajawa na wingu, naam kuweza kusimama ili kufanya huduma yao, kwa sababu ya lile wingu; kwa kuwa nyumba ya Mungu imejaa utukufu wa [Yehova].”—2 Nya. 5:13, 14.
19. Basi, ni nini kinachoongoza ibada safi ya Mungu?
19 Kwa hiyo, na tuhakikishe jambo hilo la lazima: Roho takatifu inaendesha ibada safi ya Yehova. Inatenda kazi sana kwa ajili ya wale wanaozoea na kuunga mkono ibada safi ya Mungu mmoja wa kweli. Mifano ya jambo hilo ilionekana wakati waamuzi waliochaguliwa kwa njia ya pekee walipoongoza Israeli katika Nchi ya Ahadi. —Kutoka Holy Spirit—the Force Behind the Coming New Order sura ya 4.