Mataraja ya Taratibu Mpya!
1. Mabaki watakaookoka watakuwa na sehemu gani duniani katika utendaji wa hiyo Taratibu Mpya, na ni mpaka wakati wa tukio gani?
MIUJIZA hiyo iliyofanyika katika siku za mwanzo-mwanzo wa kundi la Kikristo ilikuwa ya ajabu kweli kweli. Walakini miujiza hiyo ilikuwa wonyesho mdogo tu wa miujiza itakayotimizwa kwa roho takatifu katika taratibu mpya ya Yehova. Twaweza kutarajia mabaki waliookoka washiriki katika utendaji huo wenye kusisimua mwanzoni mwa Taratibu Mpya. Lakini kwa muda gani? Hatujui kwa wakati huu kutokana na Maandiko Matakatifu. Wao wanaitazamia “ndoa”—ile ndoa ya kimbinguni ya Mwana-Kondoo ambayo anafanya pamoja na kundi lililo Bibi-arusi wake aliyekamilishwa. Wakati wa kutimizwa kwa jambo hilo wao wanaondoka duniani na kuthawabishwa na sehemu yenye furaha katika “ufufuo wa kwanza.” Kwa hiyo lazima wawe waaminifu mpaka kufa.
2. Je! “mkutano mkubwa” watauona ufufuo wa jamii ya Bibi-arusi, au wataona ufufuo wa akina nani?
2 Ufufuo wa jamii ya Bibi-arusi utakuwa usioweza kuonekana kwa macho ya “mkutano mkubwa” wa waokokaji wa dhiki, wanaotumainia kuishi milele katika paradiso iliyorudishwa duniani. Hata hivyo, kutakuwako ufufuo wa duniani utakaoonekana na macho ya “mkutano mkubwa” wakati wa “saa” ya Mungu ya kufufua wafu kupitia kwa Kristo.
3. Kwa habari ya wanadamu wafu waliokombolewa, kama ufufuo wao utawaongoza kwenye uzima wa milele au kwenye hukumu ya laana itategemea jambo gani?
3 Yesu Kristo mwenyewe anaingojea saa hiyo. Aliitabiri wakati alipokuwa alizungumza juu ya siku ya hukumu ya ulimwengu, akasema: “Saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo hukumu.” (Yohana 5:27-29) Kwa habari ya wote watakaofufuliwa kwa sababu ya ubora wa dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo, mwendo wao wa wakati ujao chini ya ufalme wa Kristo utaonyesha kama ufufuo wao waongoza mwishowe kwenye uzima wa milele katika dunia ya paradiso au waongoza mwishowe kwenye hukumu ambayo katika hiyo wanahukumiwa uharibifu wa milele. Wale wanaotii roho takatifu yenye kuenea pote na kuiacha iwe nguvu yenye kuongoza maisha zao watapata uzima wa milele katika Paradiso. Wale wenye kuipinga roho takatifu wakati huo, ambayo utendaji wake waonekana waziwazi, wapata hukumu ya kuitenda dhambi roho takatifu, yaani, mauti ya milele.
4. Mfalme Yesu Kristo anajiona kuwa na wajibu wa kutimiza ahadi gani aliyofanya katika siku ya kufa kwake, nayo “saa” ya jambo hilo kutukia itagonga wakati gani?
4 Mfalme wa kimbinguni Yesu Kristo bado anajiona kuwa na wajibu wa kuitimiza ahadi yake aliyofanya kwa yule mtenda mabaya mwenye huruma aliyekufa pamoja naye huko Kalvari katika siku hiyo yenye msiba ya Nasani 14, mwaka 33 W.K. Bila shaka, mtenda mabaya huyo aliyetundikwa bado angali mfu naye hakumbuki cho chote. (Mhu. 9:5, 10) Walakini Yesu Kristo aliyetukuzwa anakumbuka maneno yake aliyomwambia mtenda mabaya huyo aliyemhurumia: “Kweli mimi nakwambia leo, Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Luka 23:39-43, NW) Kwa sababu ya mtajo huu, “saa” ya Yesu ya kumwezesha huyo mtenda mabaya aliyemo katika kaburi la ukumbusho asikie sauti yake haitafika mpaka Paradiso iliyorudishwa duniani iwe imeendelea sana hivi kwamba mtenda mabaya huyo aliyefufuliwa aweza kuona mabadiliko ya mambo duniani. Kwa kupatanisha maisha yake na roho takatifu itokayo kwa Mungu, mtenda mabaya huyo aweza kufanya ufufuo wake uwe wa namna ambayo mwishowe waongoza kwenye uzima wa milele katika Paradiso ya duniani pote.
5. Kati ya wale watakaopokewa tena kutoka kwa wafu, kutakuwako “wingu” gani linalotajwa katika Maandiko?
5 Sisi ambao tutakuwa duniani wakati huo tutawapokea tena kutoka kwa wafu si watu wa jamaa zetu na rafiki zetu tu bali pia wanaume na wanawake waaminifu wa nyakati za kale waliokuwa mashahidi wa Yehova na ambao walipata kuongozwa na roho takatifu. Hawa watatia ndani “wingu kubwa la mashahidi,” ambao waanza na Yohana Mbatizaji na kurudi nyuma mpaka shahidi wa kwanza wa Yehova aliyefia imani, yaani, Habili. (Ebr. 11:2 mpaka 12:1) Inaelekea kwamba hawa watakuwa na sehemu yenye maana sana katika hiyo Taratibu Mpya.
6. Wanaume kutoka katika “wingu” hilo watapewa cheo gani pamoja na wengine, nao huenda wakatumikia kama njia ya kupashana habari namna gani?
6 Kutoka kwa hao Mfalme Yesu Kristo atachagua wanaume ambao ‘ataweka kama wana wa kifalme katika dunia yote.’ (Zab. 45:16, NW) Tayari kutakuwako “wana wa kifalme” duniani kabla yao. Akina nani? Watakuwa wanaume kutoka kwa ule “mkutano mkubwa” wa waokokaji wa “dhiki” ambao watakuwa wamekwisha wekwa mwanzoni mwa hiyo Taratibu Mpya. (Ufu. 7:9-17; Isa. 32:1, 2) Walakini hawa “wana wa kifalme” watakuwa mawakili waonekanao wa kidunia wa “mbingu mpya,” ile serikali mpya ya kimbinguni ya Yesu pamoja na wale 144,000 warithi wa shirika wa Yesu Kristo. Bila shaka, hao “wana wa kifalme” watatumikia kama njia ya kupashana habari kati ya ufalme usioonekana na jamii ya kidunia ionekanayo ya wanadamu waliokombolewa, ile “nchi mpya.”a
7. Katika Taratibu Mpya Yesu Kristo atatimizaje cheo chake kama “Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa Amani”?
7 Taratibu Mpya itakuwa na amani isiyokatizwa kuizunguka dunia. Itakuwa chini ya utawala wa kifalme wa yeye ambaye Baba yake wa kimbinguni alimweka awe na majina ya cheo kama vile, “Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani,” na “Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe.” (Isa. 9:6, 7) Yeye atakuwa, Baba wa. Milele, kwa kuwa “enzi” yake itakuwa ya kibaba yenye kutoa uzima kwa raia zake watiifu wakiwa watoto wake. Atakuwa Mungu mwenye nguvu, kwa kuwa yeye atakuwa Hakimu aliye kama Mungu; walakini hataabudiwa na hao watoto wake wa kidunia wenye kufaidika.—Zab. 82:1-6; Yohana 1:1; 10:33-36.
8. Ni nani peke yake atakayeabudiwa wakati huo kama Mungu?
8 Yehova peke yake ndiye atakayeabudiwa wakati huo kwa kuwa kwa habari ya Taratibu Mpya imeandikwa hivi: “Tazama maskini ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskini yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao.” (Ufu. 21:3, 4) Shetani Ibilisi, “mungu wa taratibu hii ya mambo,” hatakuwa mungu katika hiyo Taratibu Mpya. (2 Kor. 4:4, NW) Ibada ya Ibilisi, ibada ya mashetani itakomeshwa. Yehova ndiye atakayeabudiwa kama Mungu.
9. Ni tunda gani litakaloongezeka sana katika hiyo Taratibu Mpya, walakini ni akina nani watakaoonekana mwishoni mwa utawala wa Kristo wa miaka elfu?
9 Roho takatifu itaenea pote katika hiyo Taratibu Mpya. (Zab. 139:7-10) Paradiso ya dunia itafanywa kuwa nzuri sana kufaa “tunda” la roho, kama vile upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujiweza. (Gal. 5:22, 23) Hali kama hiyo yenye kuzaa matunda kiroho itasitawi mpaka kufikia mwisho wa utawala wa Kristo wa miaka elfu moja. Kisha? Aja Shetani na mashetani zake kutoka lile shimo lisilo na mwisho, hawa wakifunguliwa “muda mchache.” Kwa kutumia hila hawa watajaribu kuitawala dunia yote tena kwa ile ‘roho itendayo kazi katika wana wa kuasi.’ Je! watafaulu kadiri gani wakishindana na roho ya Mungu yenye kuenea pote? —Ufu. 20:3.
10. (a) Ni mashambulio gani ambayo Shetani na mashetani zake wanafanya juu ya roho takatifu katika hiyo Taratibu Mpya? (b) Yehova anaondolewaje lawama milele?
10 Kwa kadiri ya kuishawishi hesabu fulani tu ya wanadamu waliorudishwa watende roho takatifu dhambi asiyeweza mtu kusamehewa. Hivyo wanajitenga wao wenyewe na Yehova Mungu, aliye Chanzo cha kimbinguni cha roho ya uzima. Hiyo yamaanisha mauti ya milele kwao, ile “mauti ya pili.” Lakini namna gani juu ya umati mkubwa wa wanadamu walioko katika makao yao mazuri ya Paradiso? Aha, kwa upande wao roho takatifu yaleta ushindi mkubwa. Kwa upendo wa milele wa roho takatifu watayashinda majaribu ya Shetani yenye kudanganya. Bila kuyumbayumba wataendelea kuwa washikamanifu kwa Enzi Kuu yenye kufaa ya ulimwengu wote ya Yehova, Mungu wao. Kupita kwao kwa uaminifu jaribu hilo la mwisho kunamwondolea Yehova lawama milele. Kunamaliza kabisa kabisa suala juu ya ukamilifu usio na choyo wa viumbe vya Yehova kuelekea kwake akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, suala lililoshindaniwa vikali sana kwa muda wa vizazi vingi. Shtaka la uongo la Shetani lahakikishwa kabisa kabisa kuwa la uongo, naye Yehova ahakikishwa kabisa kuwa wa kweli mwanzo, mwisho na kwa wakati wote. (Rum. 3:4) “Muda mchache” wa kufunguliwa Shetani sasa wamalizika. Hivyo, basi, mwache yeye pamoja na “uzao” wake wote wapondwe-pondwe na kuondolewa mbali kabisa katika utimizo wa ahadi ya Yehova katika Edeni. (Mwa. 3:15; Ufu. 20:7-15) Haleluya!
11. Wakati ujao wa wanaume na wanawake hao wanaoendelea kujawa na roho takatifu utakuwa wa furaha milele namna gani?
11 Je! sisi wenyewe tutakuwapo tushuhudie uovu wote ukiondolewa milele mbinguni na duniani na kisha tuendelee kuishi tukiwa na wakati ujao mbele yetu? Wakati huo ujao usio na mwisho utakuwa wenye furaha kweli kweli kwa wanaume na wanawake watakaokuwa wameendela kujawa na roho takatifu katika kujitoa kwao kusikovunjika kwa Mungu na Baba ya Yesu Kristo Bwana wetu! Wakihukumiwa na Yeye kuwa wastahili kupokea zawadi ya uzima wa milele, wataendelea kujifurahisha daima ujana katika ukamilifu wa kibinadamu katika Paradiso ya uzuri usionyauka ikiwa na mipango isiyoshindwa ya kuleta maisha yenye furaha. Itawapasa kuishi sikuzote kulingana na roho takatifu ambayo wakati wote imekuwa ikitegemeza hiyo taratibu mpya yenye kumletea Mungu heshima. Ee, na tujithibitishe wenyewe kuwa tunastahili kuishi katika hiyo taratibu mpya! Kupatana na tamaa hiyo ya moyoni, sala yetu na iwe sikuzote kama ile ya mtunga zaburi Daudi aliyemwambia Mungu hivi akiwa katika ulimwengu wenye uadui:
“Ee [Yehova], uniponye na adui zangu; nimekukimbilia Wewe, unifiche. Unifundishe kuyatenda mapenzi yako, kwa maana ndiwe Mungu wangu; [roho yako njema iniongoze] kwenye nchi sawa.”—Zab. 143:9, 10.
12. Tumalizapo, twaambiaje wale ambao hata sasa wanatamani kuishi kupatana na roho ya Mungu?
12 Basi, kwa unyofu wote wa moyo, tumalizapo twaambia hivi watu wote ambao hata sasa wanatamani kuishi kulingana na hiyo nguvu ya utendaji ya Mungu yenye kutakasa: “Neema ya Bwana Yesu Kristo, na pendo la Mungu, na ushirika wa [roho takatifu], ukae nanyi nyote.” —2 Kor. 13:14.—Kutoka Holy Spirit—The Force Behind the Coming New Order, Sura ya 9.
[Maelezo ya Chini]
a Linganisha Ezekieli 44:3; 45:7-22; 46:2-18; 48:21, 22.