Je! Kwa Kweli Jina Hilo Ni La Maana?
HILO ndilo ulizo ambalo wengi wanauliza kunapokuwa mazungumzo juu ya jina la Mungu. “Mungu ni Mungu,” ndivyo wanavyosema. “Kwa hiyo kwa sababu gani tuhitaji jina?”
Kitabu The Illustrated Bible Dictionary, kilichochapishwa katika 1980 na Tyndale House Publishers, kinatoa maelezo haya juu ya umaana wa jina katika nyakati za Biblia: “Uchunguzi juu ya neno ‘jina’ katika AK [Agano la Kale] unaonyesha jinsi [Jina] linavyomaanisha mengi katika Kiebrania. Jina si kibandiko tu, lakini ni lenye maana ya utu halisi wa mwenye [Jina] hilo. Laweza kutokana na hali za kuzaliwa kwake (Mw. 5:29), au kuonyesha tabia yake (Mw. 27:36), na wakati mtu anapoliweka ‘jina’ lake juu ya kitu au mtu mwingine yeye anakuja chini ya uongozi na ulinzi [wa mwenye jina] hilo.”
Halafu, kuhusu jina la Mungu, Dictionary (Kamusi) hiyo inasema: “Kwa hiyo, Yahweh, tofauti na Elohim [Mungu], hasa ni jina la mtu, ingawa Mtu huyo ni wa kimungu. Ikiwa ndivyo, linatoa mawazo fulani; linamwonyesha Mungu kuwa Mtu, na kwa hiyo linamwingiza kwenye uhusiano na watu wengine, wa kibinadamu . . . , naye anazungumza na Wazee wa Ukoo kama rafiki mmoja anavyozungumza na mwenzake.”
Kwa hiyo njia pekee ambayo mtu anaweza kumkaribia Mungu na kuwa na uhusiano wa kibinafsi naye ni kwa kumjua yeye kwa jina lake, Yahweh, au Yehova, na kwa kujifunza kutumia jina hilo kwa njia ya heshima katika kumwabudu yeye. (Yohana 17:26) Kwa hakika, wao ‘watakuja chini ya uongozi na ulinzi wake,’ maana Yehova mwenyewe anasema, “Nitamlinda kwa sababu amepata kulijua jina langu.”—Zaburi 91:14, NW.