Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Katika miaka ya majuzi nimesoma habari za watoto wanaozaliwa baada ya kutayarishwa kwanza wakiwa ndani ya vijumba vya kioo vya uchunguzi wa kisayansi, badala ya kuwa kuwa katika tumbo la uzazi la mama. Ni nini maoni ya Kibiblia juu ya njia inayotumiwa kufanya hivyo?
Kwanza, acheni tuangalie kifupi mambo ambayo yanasemwa kuwa yametukia, kama inavyoonyeshwa na kile kisa cha kwanza, kilichotukia katika Uingereza.
Mwanamke mwenye kuhusika alikuwa hawezi kuchukua mimba kwa njia ile ya kawaida kwa sababu mirija yake ya uzazi, ambamo yai lazima lipite ndipo liweze kufikia tumbo la uzazi, ilikuwa na tatizo. Basi wanasayansi walifanya upasuaji mdogo wakatoa moja la mayai yake yaliyoiva na kulitia katika chombo cha maabara (mahali pa uchunguzi) pamoja na vitu vya kulisha yai hilo ili likue. Shahawa za mume wake zilitiwa hapo pia kisha lile yai likapata mimba. Baada ya hesabu fulani ya siku kile kikundi cha chembe zenye kukua (zinazoitwa “blastosisti”) kiliingizwa kwa uangalifu ndani ya tumbo la uzazi la mama huyo halafu chembe hizo zikakua kama kawaida, kisha mtoto akazaliwa.
Katika kisa hicho ile chembe ya shahawa na lile yai vilitokana na mume na mke huyo. Jambo hilo linastahili kuangaliwa kulingana na maoni ya Kibiblia. Kwa sababu gani? Kwa sababu ya sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli wa kale: “Haikupasi kamwe kumpa mke wa mwenzako umajimaji wenye kukutoka ukiwa shahawa hata uwe mchafu kupitia huo.” (Mambo ya Walawi 18:20, 29, NW) Sheria hiyo ilitolewa kabla zile njia za kutoa shahawa za mwanamume na kutunga mimba yai la mwanamke likiwa nje ya tumbo lake la uzazi hazijaanza kutumika; hata hivyo inaonyesha namna Mungu anavyolifikiria jambo hilo.
Kutokana na Biblia ni lazima tukate shauri kwamba ikiwa utungaji mimba unafanywa kwa kutumia chembe ya shahawa na yai ambalo halikutokana na watu wawili waliooana (mume na mke), tendo hilo lingekuwa ni uzinzi au uasherati. Maandiko yanaonyesha wazi kabisa maoni ya Mungu juu ya mambo ya namna hiyo: “Waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.” (Waebrania 13:4; Mathayo 19:9) Lakini namna gani kama watu wawili waliooana ambao wamejaribu kupata watoto wakashindwa wanashauriwa kwamba wakikubali kufuata njia iliyotangulia kutajwa watafanikiwa? Yanayofuata ni mambo fulani ya kufikiriwa:
Je! hatua zote zinazohusika katika kutumia mashine—hata kutungwa kwa mimba katika chombo cha maabara ya uchunguzi—zisingefanya jambo hilo lionekane sana kutokuwa la kawaida ya binadamu au lililo kinyume kabisa cha tabia njema hata lisistahili kukubaliwa nao?
Lile yai lililo katika chombo (kabla na baada ya kutungwa mimba) linakuzwa na vitu vyenye kulilisha. Angaa katika visa fulani ambavyo vimekwisha kutukia, umajimaji mwembamba wa damu ulio mwangavu ulitumiwa kulisha yai ili likue. Kwa njia hiyo inaonekana kwamba sheria ya Mungu juu ya damu inapasa kufikiriwa.—Matendo 15:28, 29; Mambo ya Walawi 17:13, 14.
Habari mbalimbali zinasema kwamba katika visa fulani baada ya mimba kutungwa wanasayansi wameliangamiza yai lililotungwa mimba kwa sababu walihakikisha kwamba lisingeweza kukua vizuri, au lingekuwa na kasoro za mwili kutokana na chembe za urithi. Kama hivyo ndivyo, je! kufanya hivyo kusingekuwa sawa na kutoa mimba?a Na ni kwa kadiri gani hao wenye kuitwa wazazi ati wangekuwa na mamlaka ya kusimamia jambo hilo au daraka la kukomesha uhai ulioanza kukua karibuni?
Kuongezea hilo, wanasayansi wengine wanakuwa na wasiwasi kwamba kasoro za hali ya urithi zinaweza kutokea, ama wakati wa ukuzi katika tumbo la uzazi ama baadaye.
Hayo ni mambo ambayo ingempasa Mkristo ayafikirie, ingawa atatambua kwamba mwishowe itakuwa lazima ajifanyie uamuzi wa kibinafsi.
[Maelezo ya Chini]
a Angalia The Watchtower la Agosti 1, 1977, kurasa 478-480.