Wafundishe Watoto kwa Kutumia Habari Zilizorekodiwa Katika Tepe
Akili za watoto ni kama sifongo. Zinafyonza mambo zinayoyasikia, kisha zinarudia kutaja mambo hayo. Ni jambo zuri kama nini wakati watoto wanapotaka kusikiliza mambo yanayofaa na yenye kufaidi! Wazazi ambao wamejipatia tepe za kaseti za Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia wanafurahia sasa kuona jambo hilo likitendeka. Hakika tepe za kichapo hicho kilicho kizuri sana zinavuta fikira za watoto, kama vile anavyoeleza mama mmoja wa New York State.
“Mwanangu mwenye umri wa miezi 17 anafurahia sana kuzisikiliza. Wakati wo wote utepe unapofika mwisho yeye anaanza kulalamika na kuelekeza kidole kwenye mashine ya utepe ili aendelee kusikiliza.
“Binti yangu, ambaye amekuwa na umri wa miaka mitatu hivi karibuni tu, amefaidika sana kutokana na tepe hizo. Yeye anaweza kusimulia yaliyotukia kati ya Daudi na Goliathi; hata anatoa sauti kali katika sehemu inayotaja maneno yaliyosemwa na Goliathi, sawasawa na vile msemaji aliye katika utepe anavyofanya. Tena yeye anaweza kunieleza hadithi nyingine nyingi zilizomo, nami nashangazwa na jambo hilo kila siku.
“Sasa ninapowasomea Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, mwanangu mwenye umri wa miezi 17 anasikiliza kisha binti yangu mwenye umri wa miaka mitatu anazitamka sentensi zenyewe pamoja nami. Anafanya yote hayo kwa sababu anakumbuka mambo yaliyo katika tepe za Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. “
Kwa kuwa tepe za masimulizi ya Biblia 116 ya Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia zinampa msikilizaji wazo fulani juu ya yaliyomo katika Biblia, hakika hii ni njia nzuri sana ya kufundishia watoto!
Tafadhali mnipelekee pakiti yenye gamba laini la rangi ya hudhurungi yenye tepe za kaseti nne za Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia. Ninyi mtanilipia malipo ya kuzipeleka kwa njia ya posta. Mimi nimewapelekea Kshs. 100/- (Tshs. 175/-).