Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w87 2/1 uku. 21
  • Unyofu Unaletea Yehova Sifa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Unyofu Unaletea Yehova Sifa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Habari Zinazolingana
  • Uwe Mnyofu Katika Mambo Yote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Uwe Mnyoofu Katika Mambo Yote
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Jinsi ya Kuendelea Kuwa Wanyoofu Katika Ulimwengu Usio na Unyoofu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Maana Yake Nini Kuwa Mfuataji Haki?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
w87 2/1 uku. 21

Ripoti ya Watangazaji Ufalme

Unyofu Unaletea Yehova Sifa

YEHOVA anataka kwamba watumishi wake wawe wanyofu, wenye haki, na wanaostahili kutumainiwa. Kwa mfano, Musa alishauriwa achague kuwa waangalizi wale ambao wangekuwa “wanaume wenye uwezo, wanaoogopa Mungu, wanaume wanaostahili kutumainiwa, wanaochukia faida isiyo ya haki.” (Kutoka 18:21, NW) Kama wanaume hao waliochaguliwa, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wana sifa ya kuwa wanyofu, kama vile inavyoonyeshwa na jambo lililoonwa linalofuata.

◻ Shahidi mmoja anayefanya kazi kwenye afisi ya tawi ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi katika Ghana alilipwa kwa makosa kiasi kilichozidi haki yake kwa dola 3,630 na mshughulikia-pesa katika benki. Kosa hilo halikuonwa na mshughulikia-pesa wala ndugu yule wakati huo. Ijapokuwa hivyo, ndugu alipofika nyumbani aliona kwamba alikuwa amelipwa kiasi kinachozidi haki yake na mara hiyo akarudi benki akiwa na pesa zile. Mshughulikia-pesa, alipomwona ndugu, alipaaza sauti ya mshangao: “Ni huyo! Amerudi kweli. David, mtu wako amezileta pesa!” Pesa hizo zilirudishwa kwa mwenye kuzishughulikia. David, ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova anayefanya kazi katika benki ile ile, alikuwa amemhakikishia mshughulikia-pesa na wengine waliolijua kosa lililotokea kwamba pesa hizo zingerudishwa mara tu ndugu yule akigundua kosa hilo.

“Tamasha hiyo ilipokuwa ikiendelea,” ripoti hiyo inasema, “macho yote” yalikazwa juu ya ndugu wale wawili. Yule mwenye kurudisha zile pesa alieleza hivi: “Ni kwamba mimi singaliweza kubaki na pesa hizi na bado niwe na dhamiri njema mbele za Mungu wangu, Yehova.” Kituko hicho kiliongeza heshima ambayo wakuu wa benki walikuwa nayo tayari kwa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi.

Unyofu unatokeza heshima, hasa katika ulimwengu ulio na ukosefu mwingi wa unyofu. Ndugu huyo alijua kwamba yeye alikuwa na wajibu wa kutoa hesabu kwa mmoja aliye juu zaidi ya wanadamu, Yehova Mungu. Unyofu kama huo unaletea Yehova sifa, maadamu yeye ni “Mungu wa uaminifu, ambaye pamoja naye hapana ukosefu wa haki.”​—Kumbukumbu 32:4, NW.

◻ Kuwa na unyofu na kudumisha dhamiri njema kuelekea Mungu kunaonwa pia katika jambo lililoonwa la mwanamume kijana katika Thailand. Yeye alikuwa amefanya andikisho kwa ajili ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! na alikuwa akianza kutumia mashauri ya Biblia aliyokuta katika majarida hayo. Yeye alikuwa ndiye mhasibu mkuu wa shirika alilofanyia kazi, na dhamiri yake ilianza kumsumbua, kwa kuwa ilikuwa desturi ya biashara nyingi kutumia vitabu viwili-viwili katika kuandikia mambo yao ili waepuke kulipa kodi. Yeye alipomfikia meneja kuhusu jambo hilo, meneja alicheka tu akamwambia aende zake. Ndipo makala nyingine ilipokuja katika moja la magazeti ikikazia uhitaji wa unyofu. Akiwa na dhamiri yenye kufadhaika, mhasibu huyo alimpelekea Yehova sala amsaidie kunyoosha jambo hilo la kodi pamoja na meneja wake. Kiasi kikubwa cha pesa kilihusika. Asubuhi iliyofuata yeye akaomba meneja ruhusa azilipe kodi zilizopasa kulipwa. Ajabu ni kwamba meneja alikubali bila ubishi zaidi.

Sasa mwanamume huyo ana furaha maadamu anaendesha maisha ya unyofu mbele za Mungu na wanadamu. Mwendo huo wa hekima unafurahisha Yehova, pia, kwa maana kama vile Mithali 27:11 (NW) inavyosema: “Uwe mwenye hekima, mwana wangu, na ufanye moyo wangu ufurahi sana, kwamba mimi nipate kutolea jibu huyo anayenifanyia madharau makali.”

[Picha katika ukurasa wa 21]

“Mimi singaliweza kubaki na pesa hizi na bado niwe na dhamiri njema”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki