“Hazina kwa Ulimi Usio wa Kweli ni Pumzi”
KUSEMA uwongo na kudanganya mara nyingi ni mambo yanayoonwa siku hizi kuwa halali—na mbinu za kibiashara—zenye kufanikiwa kabisa. Ndivyo ilivyokuwa katika nyakati za Biblia. Mtunga zaburi Asafu aliandika juu ya wale ambao “wamepata mali nyingi,” kwa wazi hiyo ikiwa kwa mbinu za udanganyifu. Watu kama hao wanaweza kuonekana “kustarehe sikuzote” kwa sababu ya mali nyingi ambazo matendo yao ya udhalimu yamewaletea.—Zaburi 73:8,12.
Wakristo leo, hata hivyo, lazima waepuke ‘kupenda pato la udanganyifu’ na kutumia matendo ya werevu ya kibiashara yasiyo ya unyofu au udanganyifu.(1 Petro 5:2, NW) Yaonya Mithali 21:6, NW: “Kule kupata hazina kwa ulimi usio wa kweli ni pumzi inayoendeshwa mbali, kwa habari ya wale wanaotafuta kifo.” Ndiyo, “hazina” yo yote inayopatikana kwa kusema uwongo na kudanganya haina budi kuwa ya kitambo tu kama “pumzi,” kama mvuke wa kitambo kidogo tu. “Hazina za [waovu] hazifaidii kitu” upitapo muda. (Mithali 10:2) Kwa kweli, mwenye kusema uwongo ‘anatafuta kifo’ kwa kufuatia mwendo wenye kuleta kifo. Uhai wake ungeweza kukatishwa mapema wakati mbinu zake za kusema uwongo zimrudiapo. (Linganisha Esta 7:10.) Au akiwa na muda mwingi kabisa, uhai wake utakomeshwa katika siku ya hukumu ya Mungu.