“Lisifu Jina la Yehova”
Septemba 2, 1986, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Ujeremani (Ujeremani Mashariki) ilitoa mfululizo wa stampu zikionyesha sarafu za kihistoria za Ujeremani. Ya kwanza katika mfululizo huo inaonyeshwa hapa chini. Sarafu inayoonyeshwa ina tarehe 1633. Hata hivyo, lililo la kupendeza hasa ni zile herufi nne za Kiebrania zenye kung’aa zinazoonyeshwa zikiwa zimepigwa chapa juu ya sarafu. Zamaanisha nini? Briefmarkenwelt, jarida la Ujeremani linaloweka na kupanga aina mbalimbali za stampu linatoa elezo hili: “Malaika wawili, wakiwa wamening’inia juu ya sura ya mji, wanabeba katikati yao jina Yehova.”
Wakati wa karne za 16 na 17, ilikuwa jambo la kawaida sana kufanyiza sarafu kama hizo katika Ulaya. Ensaiklopidia ya kale ya Kijeremani yenye tarehe 1838 inasema hivi: “Ule usemi sarafu-za-Yehova unatia ndani sarafu zote na medali ambazo huonyesha lile neno יהוה, Yehova, ziking’aa, ama zikiwa peke yazo au pamoja na neno Yesu, . . . mara nyingi zikiwa na usemi unaorejeza kwenye hilo; kwa kuwa hilo linapatikana kwa msingi juu ya [sarafu nyingi za fedha zilizotolewa na nchi mbalimbali za Ujeremani kati ya karne za 15 na 19], zimepangwa pamoja chini ya jina sarafu-Yehova.”
Huenda ikawa, kwamba watu walio wengi wanaotumia stampu hizo hawajui kwamba herufi hizo za Kiebrania zinawakilisha jina la Mungu. Lakini Mashahidi wa Yehova wanafurahia kuonyesha sehemu hii yenye kupendeza juu ya stampu na kuendelea kueleza maana na umaana wa jina la Yehova. Hivyo kutokana na upande usiotazamiwa wanasaidiwa ‘kulisifu jina la Yehova.’—Zaburi 135:1, NW.