Maswali Wanayouliza Watu Juu ya Kileo
“WATU wenye hekima hawanywi divai kabisa.” Ndivyo alivyotangaza kiongozi wa kidini Mnaijeria. Si muda mrefu uliopita, maneno kama hayo yangepuuzwa kuwa ni kutovumilia wengine na kuwa ya wale wanaoshika lao wenyewe. Lakini, leo mwelekeo wa kupinga utumiaji wa kileo unasitawi katika sehemu fulani-fulani za ulimwengu.
Uchunguzi wa karibuni wa maoni ya wachache kuwakilisha maoni ya wengi uliofanywa na Reader’s Digest/Gallup (U.S.), kwa mfano, ulifunua kwamba “Waamerika wameanza kunywa kiasi kidogo zaidi.” Jarida Time vivyo hivyo linaripoti kwamba “Amerika inapunguza [utumiaji wa kileo], na inafanya hivyo kwa mwendo wa haraka zaidi ya wakati mwingine wo wote tangu Katazo [la kutengeneza, kusafirisha, na kuuza vinywaji vyenye kileo] lilipoanza kutenda kazi katika 1920.” Ufaransa inaripoti upunguo katika utumiaji wa divai.
Ni nini sababu ya mwelekeo huu wa kuwa na kiasi? Wengine wamepiga makelele juu ya mauaji yenye kuogopesha yanayofanywa kwenye barabara kuu kwa sababu madereva wanaendesha gari wakiwa walevi. “Katika 1983,” kilidai kichapo Reader’s Digest, “kileo . . . kiligharimu [nchi ya Amerika] dola 89.5 bilioni katika kazi ya kuajiriwa iliyokosa kufanywa na bidhaa zilizokosa kutengenezwa, uangalizi wa afya, mali iliyopotezwa na uhalifu, pamoja na uharibifu usioweza kuhesabika kwa maisha ya jamaa za wale waliohusika.” Si ajabu, basi, kwamba Tengenezo la Afya Ulimwenguni la UM lilipendekeza hivi karibuni kwamba serikali ‘ziweke kizuizi juu ya upatikanaji wa kileo kwa masilahi ya afya na hali njema ya idadi za watu wao.’—New Nigerian, Machi 16, 1983.
Wengine hata wanatoa hoja ya kupendelea kutokunywa hata kidogo. Kiongozi wa kidini wa Naijeria aliyetajwa hapo juu anadai hivi: “Mithali 20:1 inasema waziwazi kwamba wale wanaokunywa divai si wenye hekima.” Na bado mhubiri mwingine anadai kwa nguvu nyingi: “Maandiko Matakatifu yanalaumu vikali kileo katika Kitabu cha Isaya,” akirejeza kwenye maandiko kwenye Isaya 5:11, 12, na Isa 5:22.
Kwa sababu ya madai hayo, watu wanauliza hivi: “Mistari kama hiyo ya Maandiko inamaanisha nini? Je! kweli kweli Biblia inakataza kabisa utumiaji wa vinywaji vyenye kileo? Je! Yesu mwenyewe hakunywa divai, au maji-maji ya zabibu yasiyo na kileo ndiyo yaliyohusika? Kwa sababu ya hatari zilizo wazi zinazohusika, je! ingekuwa bora Wakristo waepuke kabisa kunywa kileo? Majibu kwa maswali haya yanaweza kupatikana kwa kuangalia katika Biblia yenyewe.