Hatari za Utajiri na za Umaskini
JE! Biblia inapuuza utajiri na kutia moyo kuwa maskini? Watu wengi wanafikiri hivyo. Lakini mithali mbili zinazohusiana zinasaidia kuelewesha wazi jambo hili.
Mithali 10:15 inasema: “Mali ya mtu tajiri ni mji wa nguvu; uangamivu wa maskini ni umaskini wao.” Ndipo mstari 16 unapoongezea hivi: “Kazi yake mwenye haki [mwadilifu, NW] huelekea uzima; mazao ya wabaya huuelekea dhambi.” Angalia jinsi mithali hizo mbili zinavyokamilishana.
Mstari 15 unashuhudia kwamba utajiri una faida fulani, umaskini mambo fulani ya ukosefu. Huenda mali zikasaidia kulinda mtu na kadiri fulani ya mashaka-mashaka ya maisha. Ingawa hivyo, huenda mtu maskini akawa na matatizo ya ziada kwa sababu hawezi kukabiliana kifedha na matukio yasiyotazamiwa. Katika jambo hilo Biblia inasema jinsi hali ilivyo hasa.—Mhubiri 7:12.
Hata hivyo, mstari 15 unaweza pia kufahamiwa kuwa unadokezea hatari inayohusu utajiri au umaskini. Matajiri wengi wanatia tumaini lao kamili katika pesa zao; wao wanaziona hizo tu kuwa ndizo himaya wanayohitaji. (Mithali 18:11) Hata hivyo, mali haziwezi kuwasaidia wapate jina jema pamoja na Mungu wala kuwapa furaha yao inayodumu. Kwa kweli, mali zinaweza kufanya iwe vigumu zaidi kupata jambo hilo. Mfano wa Yesu juu ya tajiri aliyejenga maghala makubwa zaidi lakini hakuwa tajiri kuelekea Mungu unaonyesha wazi hilo. (Luka 12:16-21; 18:24, 25) Kwa upande mwingine, maskini wengi wanafuata kwa makosa maoni ya kwamba umaskini wao unafanya wakati ujao wao usiwe na tumaini.
Angalia jinsi mstari 16 unavyolimalizia vizuri jambo hilo. Kama mtu mwadilifu ana pesa nyingi au chache, kazi yake inaweza kumletea furaha. Yeye haachi pato la kifedha kutokana na kazi yake livuruge msimamo mwema alio nao mbele za Mungu. Bali, jitihada za mtu mwadilifu katika maisha zinamletea uhakikisho wa kupata uzima wa milele wakati ujao, zaidi ya kupata furaha sasa. (Ayubu 42:10-13) Ingawa hivyo, mwovu hawi na manufaa hata akipata pesa nyingi. Badala ya kuthamini kwamba pesa zina ubora wa kutoa himaya na aishi kulingana na mapenzi ya Mungu, yeye anatumia mali zake kuendeleza maisha ya dhambi.