‘Wamejiweka Wakfu Milele kwa Yule Mungu Mkuu Yehova’
KATIKA Aprili 1935, mhudumu na msemaji Mwamerika anayejulikana sana alizuru Hawaii. Hilo lilikuwa jambo la upendezi wa pekee kwa Mashahidi wa Yehova, ambao walikuwa 12 tu wakati huo, kwa kuwa mtu huyo mashuhuri mwenye kuzuru alikuwa Joseph F. Rutherford, msimamizi wa pili wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Biblia na Trakti. Hotuba “Nani Atatawala Ulimwengu?” ilizungumzia Ufalme wa Mungu unaokuja kutawala ulimwengu. Hotuba hiyo ilitolewa katika jumba la shule ya sekondari ya huko, na ilitangazwa sana.
Jina la Mungu na Ufalme wake kimekuwa ndicho kichwa cha utendaji wa mahubiri ya Mashahidi wa Yehova tangu mwanzisho wao wa ki-siku-hizi. Kwa hiyo inapendeza kwa wote wanaothamini na kutumia jina la kibinafsi la Mungu aliye mweza yote, Yehova, kwamba jina linganifu la Kihawaii, Iehova, lilitumiwa kikawaida na waabudu Wahawaii wa mapema. Moja la makanisa ya kwanza kujengwa na wahudumu wa Jumuiya ya Wakristo katika Hawaii, lile kanisa la mawe lililoko Kawaiahao katika Honolulu, lilipigwa msingi wa jiwe lake la pembeni katika 1839. Yaliyonakishiwa katika jiwe hilo la wakfu ni maneno haya: “Kwa Iehova Mungu wetu milele na milele.”
Tangu 1935, wakati Jaji Rutherford alipozuru, kazi ya Mashahidi wa Yehova katika Hawaii imekua kutoka Mashahidi watendaji 12 kufikia zaidi ya 5,400 leo. Kweli kweli wao ‘wamejitoa wakfu milele kwa yule Mungu mkuu Yehova.’