“Mielekezo ya kufaulu kulea mtoto mwenye furaha na mafanikio”
CHINI ya kichwa hicho, gazeti Medical Aspects of Human Sexuality lilichapisha makala ambamo Dakt. Irene Jakab, profesa wa chuo kikuu wa utibabu wa akili, alipangilia mambo ambayo yeye alihisi yalihitajiwa kabisa ili mtoto alelewe kuwa mtu mzima mwenye mafanikio. Miongoni mwa “mielekezo” yake ulikuwamo uhitaji wa wazazi kupenda mtoto wao, kumwongoza juu ya yafaayo na yasiyofaa, na kumzoeza kufanya maamuzi. Mwanamke huyo alihisi kwamba “mielekezo” hiyo haipasi kabisa kutia ndani hasira ya haraka kwa upande wa wazazi, kutaka mambo yafanywe kikamilifu, hangaiko la wasiwasi wa kupita kiasi, au uendekevu.
“Mielekezo” ya Dakt. Jakab ni timamu sana kwa kadiri hiyo. Kwa kweli, maelfu ya miaka iliyopita, Biblia iliwapa wazazi shauri kama hilo. (Ona, kwa kielelezo, Mithali 4:1; 13:24; 22:6; Wakolosai 3:21.) Hata hivyo, Biblia hutia ndani jambo ambalo Profesa Jakab aliacha nje: umuhimu wa kufundisha watoto kupenda Muumba wao na kuzoelea sana Neno lake. Mtume Paulo aliandika hivi: “Nyinyi, akina baba, msiwe mkiwaudhi watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.”—Waefeso 6:4, NW; Kumbukumbu 6:4-7, UV.
Bila mazoezi hayo, huenda watoto wakakua bila nanga ya kiadili. Tokeo lingeweza kuwa lenye msiba katika ulimwengu huu usiofuata maadili na wenye ufisadi.