Alipata Trakti Katika Njia ya Gari-Moshi
MWAKA ulikuwa 1921. Katika miinuko ya Transvaal, mkoa mmoja wa Afrika Kusini, kikundi cha warekebishaji njia ya gari-moshi kilifanya kazi kando ya njia ya gari-moshi kwa mwendo fulani. Msimamizi wa wafanya kazi, Mwafrikana jina lake Christiaan Venter, aliona kipande cha karatasi kimebanwa chini ya reli moja. Ilikuwa trakti iliyochapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society.
Baada ya kuagiza watu wake wasimame, Christiaan aliisoma trakti kwa upendezo mwingi sana. Alikimbia kukutana na mwana-mkwe wake, Abraham Celliers, na kutangaza hivi kwa msisimuko: “Abraham, leo nimeupata ukweli!”
Muda mfupi baada ya hapo, waliandikia wachapishaji wa trakti hiyo ili wapate habari zaidi. Kwa kujibu, tawi la Afrika Kusini la Watch Tower Society lilipeleka vitabu zaidi vya Biblia. Wanaume hao wawili walijifunza pamoja wakati wa mapumziko ya chakula cha mchana na hata muda mrefu sana saa za usiku. Upesi wakaanza kushiriki ukweli na marafiki na watu wageni.
Mwishowe, wote wawili Christiaan na Abrahamu wakawa Mashahidi wa Yehova waliojiweka wakfu. Kutokana na bidii na uaminifu wao, watu wengi wa Afrika Kusini walisaidiwa kuja kwenye maarifa ya ukweli. Zaidi ya hili, leo wazao wao zaidi ya mia moja ni Mashahidi watendaji wa Yehova! Mmoja wao anatumikia kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York, na mwingine kwenye ofisi za Watch Tower Society katika Afrika Kusini.
Leo, kama miaka 70 baadaye, trakti za Biblia zinaendelea kutimiza sehemu ya maana katika kueneza ujumbe wa Ufalme.