Je! Sayansi Yaweza Kukanusha Miujiza?
Je! miujiza ya Biblia ilitukia kwelikweli? Kuna wengi, kutia na wanasayansi wengi na viongozi wa kidini, wanaojibu hapana. Wao huona kwamba imani katika miujiza ni jambo la enzi ya ushirikina na kwamba sayansi ya kisasa imekanusha uwezekano wa miujiza kutukia. Kwa hiyo, barua ifuatayo iliyotangazwa kwa chapa katika The Times ya London na kutiwa sahihi na wanasayansi wengi inastahili kuangaliwa. Yasema hivi:
“Si halali kiakili kutumia sayansi kuwa hoja dhidi ya miujiza. Kuamini kwamba miujiza haiwezi kutukia ni kitendo cha imani kama ilivyo kuamini kwamba yanaweza kutukia. . . . Miujiza ni matukio yasiyo na kifani. Hata mitindo ya kifalsafa ya kisasa iwe nini au funuo za kukagua mambo kwa kupata maoni ya watu zidokeze nini, ni jambo la muhimu kusema kwa uthabiti kwamba sayansi (inayotegemea mambo yaliyotangulia kutukia) haiwezi kuwa na lolote la kusema juu ya jambo hilo. ‘Sheria’ yazo ni mambo yaliyoamuliwa kwa kuangalia kijuujuu tu mambo ambayo tumeyaona. Imani inategemea msingi mwingine.” (Italiki ni zetu) Kwa kweli, sayansi ya kisasa haiwezi kwa njia yoyote kukanusha masimulizi ya miujiza iliyoandikwa katika Biblia.