Ni Nini Kitakachopapata Mahali Patakatifu Pa Jumuiya ya Wakristo
WATANGAZAJI wa kitabu Holy Places of Christendom, cha mwanaakiolojia Stewart Perowne, wauliza hivi: “Ni nani, bila kujali anatoka katika mapokeo gani ya Kikristo, aweza kusimama kwenye Kalvari katika Kanisa la Ufufuo [au, Kanisa la Kaburi Takatifu] katika Yerusalemu bila kuhisi kicho: kwani humo katika mahali palipotolewa kicho cha kiibada na hata kupiganiwa kwa muda wa karne nyingi, ndicho kitovu hasa cha Jumuiya ya Wakristo.”
Hakuna yeyote ambaye ameweza kuthibitisha kwamba kanisa hilo lilijengwa kwenye Kalvari, ambapo Yesu Kristo aliuawa. Kwa kweli, kabla ya maliki Mroma Konstantino kuamua kujenga kanisa hapo, hekalu la kipagani lilikuwa mahali hapo. Isitoshe, Yesu alisema hivi: “Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.” (Yohana 4:24) Waabudu kama hao hawatolei mahali “patakatifu” pa kimwili kicho cha kiibada.
Wakati mmoja, Yerusalemu ilikuwa mahali pa hekalu la Mungu na hivyo ilikuwa kitovu cha ibada safi. Hata hivyo, kwa sababu ya kutoamini kwa wenyeji wa mji huo, Yehova Mungu aliliacha, kama Yesu alivyosema angefanya. (Mathayo 23:37, 38) Yesu alitabiri pia kufanywa ukiwa kwa kitovu hicho cha kidini, ambacho wengi waliendelea kukiona kuwa mahali patakatifu. Maneno yake yalitimizwa wakati Waroma walipoharibu Yerusalemu na hekalu layo katika 70 W.K.—Mathayo 24:15, 21.
Unabii wa Yesu utakuwa na utimizo mkubwa zaidi hivi karibuni juu ya milki yote ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo, ambaye anadai kuwa mahali patakatifu. Jumuiya ya Wakristo na mahali payo mbalimbali patakatifu sasa pakabili kuharibiwa na jeshi lipingalo dini liitwalo “chukizo la uharibifu.” (Danieli 11:31) Mashahidi wa Yehova watafurahi kukuambia zaidi kuhusu tukio hilo lenye kushtua.
[Picha katika ukurasa wa 32]
Chapeli (kanisa ndogo) ndani ya Kanisa la Kaburi Takatifu
[Hisani]
Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.