Moto Wachochea Programu ya Ujenzi
“Moto! Moto! Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova limewaka moto!” Kilio hicho chenye kushtusha kilivuma Ijumaa moja alasiri katika Oktoba 1989 huko Heerenveen, mji ulio katika sehemu ya kaskazini mwa Uholanzi.
Mashahidi wa Yehova walikuwa wametumia Jumba la Kusanyiko hilo zuri kwa miaka 11. Karibu kila mwisho-juma, mamia walikuwa wamekusanyika hapo ama kwa ajili ya kusanyiko la mzunguko wa siku mbili ama kwa ajili ya siku ya kusanyiko la pekee la siku moja. Palikuwa pamekuwa mahali pa starehe pa mafunzo ya Biblia.
Aksidenti ilikuwa imetokea wakati kazi ilipokuwa ikiendelea kwenye paa ya jumba. Katika dakika chache hivi, aksidenti hiyo iligeuza jumba hilo kuwa magofu yenye moshi. Hata hivyo, kwa kushukuru, hakuna yeyote aliyeumia.
Wakihuzunika kwa ajili ya hasara hiyo lakini bila kuvunjika moyo, Mashahidi hao walifanya mipango ya jumba jipya katika mahali pengine. Walipata mahali palipofaa huko Swifterbant, katika wilaya ya Flevoland. Hiyo ni polda (bara lililotwaliwa kutoka bahari) kubwa katika ile iliyokuwa sehemu ya bahari iliyoitwa Zuider Zee, ambayo ni meta 5 chini ya usawa wa bahari.
Kufikia Januari 1991 habari ilitolewa juu ya kuanza kujenga Jumba la Kusanyiko jipya. Hilo lingejengwa katikati ya Mei na Septemba 1991. Mamia ya Mashahidi walijitolea kufanya kazi mahali hapo, na vijana wengine waliona mradi huo kuwa hatua moja kuelekea kumtumika Yehova Mungu wakati wote. Wafanyi kazi walikuja kutoka Ubelgiji na Uingereza.
Jengo lenye kubuniwa vizuri likajengwa. Jumba kuu na kafeteria yalo vilitenganishwa kwa ukumbi wenye paa ya kioo. Jumba kuu laweza kutoshea watu 1,008, na wengine 230 waweza kutazama programu kwenye viwambo vya televisheni katika jumba la karibu.
Leo, maelfu husema: ‘Njoni, twende juu milimani kwa Yehova, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.’ (Isaya 2:2, 3) Jumba la Kusanyiko hilo jipya ni mojawapo tu mahali pengi ambapo mafundisho hayo ya kiroho hutolewa. Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la kwenu ni mahali pengine. Hapo utapata ukaribishaji mchangamfu.