Walijua Jina la Mungu
KICHAPO cha kwanza kinachojulikana kuwa kilikuwa kimeandikwa na kutangazwa kwa chapa katika koloni za Uingereza za Amerika kilikuwa kile Kitabu cha Zaburi cha Ghuba. Chapa yacho ya awali ilichapwa na Stephen Daye katika Koloni ya Ghuba ya Massachusetts katika mwaka wa 1640. Kichapo hicho cha mapema kilikuwa na kitabu cha Biblia cha Zaburi, kilichotafsiriwa kutoka Kiebrania hadi lugha ya Kiingereza iliyosemwa na kuandikwa wakati huo.
Sehemu yenye kutokeza ya hicho Kitabu cha Zaburi cha Ghuba ilikuwa utumizi wa jina la kimungu katika baadhi ya mistari. Kwa hiyo, yeyote ambaye angesoma kichapo hicho miaka 350 hivi iliyopita angeweza kujua jina la Muumba wetu. Kwa mfano, katika chapa hiyo, Zaburi 83:17, 18 husomwa hivi: “Na wafadhaike wote, na kutaabika sana: naam, acheni waaibishwe, na kuangamizwa. Ili watu wajue; kwamba wewe uitwaye jina lako IEHOVAH ndiwe pekee, uliye juu ya dunia yote, wa mbele kotekote ukiwa wa juu zaidi.”
Pasipo shaka, Mungu aliye juu zaidi hutaka zaidi ya utambuzi wetu wa kwamba jina lake ni Yehova (Iehovah). Katika kile Kitabu cha Zaburi cha Ghuba, Zaburi 1:1, 2 husema kwamba “mtu aliyebarikiwa” hatembei katika shauri la waovu, “lakini yeye hutamani sana, sheria ya Iehovah.” Na Zaburi za New England za 1648 zilizosahihishwa husema hivi: “Lakini yeye hupendezwa sana na sheria ya Yehova.”
Hapo New World Translation of The Holy Scriptures ya karne ya 20 husomwa hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye hakutembea katika shauri la waovu, na katika njia ya wenye dhambi hakusimama, na katika kiti cha wenye dhihaka hakuketi. Bali kupendezwa kwake ku katika sheria ya Yehova, na katika sheria yake husoma kwa sauti ndogo mchana na usiku.”
Ili mtu awe mwenye furaha kweli kweli, ni lazima akatalie mbali shauri la waovu. Ni lazima asifuate mfano wa watenda dhambi na hawezi kushirikiana na wenye dhihaka wasiomcha Mungu. Miongoni mwa mambo mengine, yeye anahitaji kuepukana na ushirika wa wale ambao shauri na mwenendo wao ungeweza kumvuta katika ukosefu wa maadili katika ngono, utumizi mbaya wa dawa za kulevya, na utendaji mwingine mbalimbali unaopinga sheria ya Mungu. Naam, furaha ya kweli hutegemea kujifunza kuhusu Mungu wa kweli, ambaye jina lake ni Yehova, na kutumia sheria yake kama ilivyofunuliwa katika Biblia.